Yeremia 21 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Muji Yerusalema utashindwa 1 Neno hili lilimufikia Yeremia kutoka kwa Yawe, wakati mufalme Zedekia alipowatuma Pashuri mwana wa Malkia, na kuhani Zefania mwana wa Masea kwa kumwambia Yeremia hivi: 2 Tafazali, utuombee kwa Yawe, maana Nebukadneza mufalme wa Babeli anaanza kupigana vita nasi. Labda Yawe atatufanyia mumoja wa miujiza yake na kumurudisha Nebukadneza aache kutushambulia. 3 Yeremia akawajibu wale wajumbe: Muende kumwambia Zedekia kwamba: 4 Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Zedekia, nitakugeuzia wewe mwenyewe silaha unazozitumia kwa kupigana na mufalme wa Babeli na waaskari wake wanaozunguka inje ya kuta za muji wenu. Nitazikusanya silaha zile katikati ya muji huu. 5 Mimi mwenyewe nitapigana nawe kwa mukono wangu wenye nguvu na uwezo, kwa hasira, ukali na kasirani kubwa. 6 Nitawaua wakaaji wa muji huu: wanadamu na nyama vilevile. Watakufa kwa magonjwa makali sana. 7 Kisha, wewe Zedekia, mufalme wa Yuda, pamoja na wakubwa wa serikali yako na watu wa muji huu ambao watakaoponyoka magonjwa hayo makali pamoja na vita na njaa, nitawatoa katika mikono ya Nebukadneza, mufalme wa Babeli na katika mikono ya waadui zenu wanaovizia maisha yao. Nebukadneza atawaua kwa upanga wala hatawahurumia au kuwaachilia au kuwasamehe. –Ni ujumbe wa Yawe. 8 Nawe Yeremia utawaambia watu hawa kwamba: Yawe anasema hivi: Musikilize! Mimi ninaweka mbele yenu njia ya uzima na njia ya kifo. 9 Mutu atakayebaki katika muji huu atauawa kwa vita au kwa njaa au kwa magonjwa makali. Lakini mutu atakayetoka inje ya muji huu na kujitoa kwa Wababeli wanaozunguka ukuta wake, ataishi; kweli ataokoa maisha yake. 10 Nimeamua kuleta hasara juu ya muji huu wala siyo mema. –Ni ujumbe wa Yawe.– Nitautoa katika mikono ya mufalme wa Babeli, naye atauteketeza kwa moto. Hukumu juu ya jamaa ya kifalme ya Yuda 11 Utaiambia jamaa ya mufalme wa Yuda hivi: Musikilize neno la Yawe! 12 Enyi jamaa ya Daudi, Yawe anasema hivi: Kila asubui muamue maneno kufuatana na sheria yangu, muwakomboe wote walionyanganywa mali zao toka katika mikono ya watesaji. Kama si vile, hasira yangu itawaka kama moto, wala hakuna atakayeweza kuizimisha, kwa sababu ya matendo yenu maovu. 13 Sasa mimi nitapigana nanyi: ninyi munaoishi katika bonde, munaokaa kwenye mawe katika uwanja, ninyi munaosema: Nani atasubutu kutushambulia? Nani anayeweza kuingia katika makao yetu? 14 Nitawaazibu kadiri ya matendo yenu. Nitawakisha moto katika pori lenu nao utateketeza kila kitu kinachokuwa kando yenu. –Ni ujumbe wa Yawe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo