Yeremia 20 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Pashuri anamufunga Yeremia 1 Kuhani Pashuri mwana wa Imeri, ambaye alikuwa musimamizi mukubwa wa nyumba ya Yawe, alimusikia Yeremia akitangaza unabii huo. 2 Basi, Pashuri akamupiga nabii Yeremia na kumutia katika minyororo iliyokuwa upande wa mulango wa juu wa kuingilia katika nyumba ya Yawe, ulioitwa mulango wa Benjamina. 3 Kesho yake asubui, Pashuri akamufungua Yeremia toka minyororo ile. Yeremia akamwambia hivi: Yawe hakuiti tena jina lako “Pashuri”, lakini “Kitisho Kila Pahali”. 4 Maana, Yawe anasema hivi: Nitakufanya ukuwe kitisho kwako wewe mwenyewe na kwa warafiki zako wote. Wao watauawa katika vita kwa upanga wa waadui zao, wewe ukiwa ukiangalia. Nitawatoa watu wote wa Yuda katika mikono ya mufalme wa Babeli, naye atawapeleka kuwa watumwa mpaka Babeli na kuwaua kwa upanga. 5 Zaidi ya hiyo, utajiri wote wa muji, mapato yake yote, vitu vyake vyote vya bei kali pamoja na akiba zote za wafalme wa Yuda, nitavitoa katika mikono ya waadui, ambao watavinyanganya na kuvipeleka Babeli. 6 Na kwa upande wako, wewe Pashuri, pamoja na watu wote wanaokaa ndani ya nyumba yako, mutapelekwa katika utumwa. Hakika mutakwenda Babeli na huko ndiko utakapokufia na kuzikwa, pamoja na warafiki zako wote uliowatabiria uongo. Yeremia anamulalamikia Mungu 7 Ee Yawe, wewe umenidanganya, nami kweli nimedanganyika; wewe una nguvu kuliko mimi, nawe umeshinda. Nimekuwa mutu wa kuchekelewa kila siku, kila mutu ananizarau. 8 Kila mara ninaposema kitu, ninalalamika, ninapandisha sauti kwa kutangaza mateso na uharibifu. Kutangaza neno la Yawe kunaniletea kuzomewa na kuzarauliwa kila siku. 9 Lakini ninaposema “Sitamutaja tena Yawe, wala sitasema tena kwa jina lake”, ndani yangu kunawaka kitu kama moto uliofungiwa ndani ya mifupa yangu. Ninajaribu sana kuuzuia humo, lakini ninashindwa. 10 Ninasikia watu wengi wakinisingizia uongo, nao wananipanga jina la Kitisho Kila Pahali! Wengine wanasema: Tumushitaki, Tumushitaki! Rafiki zangu wapenzi wote wanangojea kwa hamu nianguke! Wanasema: Labda atadanganyika, tupate kumunasa na kumulipiza kisasi. 11 Lakini wewe Yawe uko pamoja nami. Kwangu wewe ni kama shujaa wa kutisha. Kwa hiyo watesaji wangu watajikwaa, nao hawataweza kunishinda. Watafezeheka kabisa, kwa sababu hawatashinda. Haya yao itadumu hata milele, nayo haitasahauliwa. 12 Ee Yawe wa majeshi, wewe unayemupima mutu wa haki, unayechunguza mioyo na akili ya watu, nione kisasi chako juu yao maana ninakutegemea kwa kunitetea. 13 Mumwimbie Yawe, mumusifu Yawe, kwa maana anaokoa maisha ya mukosefu kutoka katika mikono ya watu waovu. 14 Ilaaniwe siku niliyozaliwa! Siku hiyo mama aliponizaa, isitakiwe baraka! 15 Alaaniwe mutu aliyemujaza baba yangu furaha kwa kumupelekea ujumbe kwamba amepata mutoto mwanaume. 16 Mutu huyo akuwe kama miji Yawe aliyoiangusha bila huruma. Mutu huyo asikie kilio asubui, na muchana asikie kelele za vita, 17 kwa sababu hakuniua ndani ya tumbo la mama yangu; mama yangu angekuwa kaburi langu, mimba yake ingekuwa ya siku zote. 18 Kwa nini nilitoka katika tumbo la mama yangu? Nilitoka kusudi nipate taabu na huzuni na kuishi maisha ya haya? |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo