Yeremia 18 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yeremia katika nyumba ya mufinyanzi 1 Yawe akanitolea ujumbe, akisema: 2 Yeremia, simama uende kwa nyumba ya mufinyanzi, na huko nitakuambia maneno yangu. 3 Basi, nikatelemuka mpaka kwenye nyumba ya mufinyanzi, nikamukuta mufinyanzi akifanya kazi yake kwenye gurudumu la kufinyangia udongo. 4 Na wakati chombo alichokitengeneza kilipoharibika katika mikono yake, yeye alifinyanga upya chombo kingine kwa kadiri ilivyomupendeza. 5 Kisha neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: 6 Enyi Waisraeli! Mimi siwezi kuwafanya ninyi kama mufinyanzi huyu anavyofanya? –Ni ujumbe wa Yawe.– Mujue kwamba kama vile udongo unavyokuwa katika mikono ya mufinyanzi, ndivyo ninyi munavyokuwa katika mikono yangu. 7 Wakati wowote ninaweza kukusudia juu ya taifa au ufalme kwamba nitaliongoa, kulipindua na kuliangamiza. 8 Lakini taifa hilo likigeuka na kuacha uovu wake, basi, mimi nitaacha kulitendea mambo yale niliyokusudia. 9 Vilevile inaweza kunifikia kukusudia wakati wowote juu ya taifa au ufalme fulani kwamba nitalijenga na kulistawisha. 10 Lakini taifa hilo likifanya uovu mbele yangu na kukataa kunitii, basi, mimi nitaacha kulitendea mema hayo niliyokusudia. 11 Basi Sasa, uende kuwaambia watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema kwamba: Yawe anasema hivi: Mimi nimekwisha kukamata mipango juu yenu, na nimekusudia kuleta hasara juu yenu. Basi kila mumoja arudi kutoka katika njia mbaya, abadilishe mwenendo wake na matendo yake. 12 Lakini wao watasema: Hiyo ni bure tu! Tutafuata mipango yetu wenyewe na kila mumoja wetu atatenda kufuatana na ugumu wa moyo wake mwovu. Watu wanamukataa Mungu 13 Basi, Yawe anasema hivi: Muulize habari kwa mataifa yote: Nani amekwisha kusikia jambo kama hili? Kitendo Waisraeli walichokifanya ni cha kuchukiza sana. 14 Teluji ya Lebanoni inatoweka kwenye mawe ya milima ile? Maji ya milima inayoshuka toka kule yanakauka? 15 Lakini watu wangu wamenisahau mimi, wanaifukizia miungu ya uongo ubani. Wamejikwaa katika njia zao, wameacha barabara zao za zamani. 16 Wameifanya inchi yao kuwa kitisho, kuwa kitu cha kuzomewa siku zote. Kila mutu anayepita huko anashangaa na kutikisa kichwa chake. 17 Nitawasambaza mbele ya waadui zao, kama upepo mukali toka mashariki. Nitawageuzia mugongo pahali pa kuwaelekezea uso siku hiyo watakapopatwa na hasara yao. Shauri la kuua Yeremia 18 Kisha, watu wakasema: Tuende tufanye shauri baya juu ya Yeremia, maana hatukosi makuhani wa kutufundisha. Vilevile hatukosi watu wenye hekima wa kutushauria na manabii wa kututangazia ujumbe wa Mungu! Mukuje tumushitaki kufuatana na maneno yake mwenyewe, wala tusiyatilie maana mambo yote anayosema. 19 Basi, mimi nikaomba nikisema: Unitegee sikio ee Yawe, usikilize ombi langu. 20 Mutu analipwa mabaya kwa mema? Lakini, wamenichimbia shimo. Kumbuka jinsi nilivyosimama mbele yako, nikasema mema kwa ajili yao, kusudi niepushe hasira yako mbali nao. 21 Kwa hiyo uwaache watoto wao wakufe kwa njaa, uwaache wakufe kwa vita. Wake zao wakuwe tasa na wajane. Waume zao wakufe kwa magonjwa makali na vijana wao wachinjwe kwa upanga katika vita. 22 Kilio kisikilike katika nyumba zao, utakapowaletea kundi la wanyanganyi kwa rafla. Maana wamechimba shimo waninase; wameitegea miguu yangu mitego. 23 Lakini wewe, ee Yawe, unajua mashauri yao ya kuniua. Usiwasamehe uovu wao, wala kufuta zambi zao. Waanguke chini mbele yako; uwapige wakati wa hasira yako. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo