Yeremia 17 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Zambi na azabu ya watu wa Yuda 1 Zambi ya watu wa Yuda, haiwezi kufutikana, imeandikwa kwa kalamu ya chuma; kwa chongo ya almasi. Imechorwa ndani ya mioyo yao na kwenye pembe za mazabahu yao. 2 Watoto wao wanakumbuka mazabahu zao na sanamu za mungu muke, Ashera, zilizowekwa kando ya miti mibichi, juu ya vilele vya vilima 3 na juu ya milima katika mbuga. Mali yenu na akiba zenu zote nitazitoa zitekwe kwa kulipia zambi zenu mulizotenda kila pahali katika inchi yenu. 4 Itawabidi kuiacha hiyo inchi yenu niliyowapa, nami nitawafanya muwatumikie waadui zenu katika inchi musiyoijua, kwa sababu hasira yangu imewaka kama moto usiozimika hata milele. Misemo mbalimbali 5 Yawe anasema hivi: Alaaniwe mutu anayemutegemea mwanadamu, mutu ambaye anategemea nguvu za mwanadamu, mutu ambaye moyo wake umegeuka mbali nami Yawe. 6 Huyo ni kama kichaka katika jangwa, hataona mazuri yoyote. Ataishi pahali penye kukauka katika jangwa, kwenye udongo ulioharibiwa na chumvi, na usiokaliwa na watu. 7 Abarikiwe mutu anayenitegemea mimi Yawe, mutu ambaye mimi Yawe ndiye tegemeo lake. 8 Huyo ni kama muti uliopandwa kando ya maji, unaopenyeza mizizi yake karibu na chemichemi. Hauogopi wakati wa jua kali, majani yake yanabaki mabichi. Hauhangaiki katika mwaka wa ukosefu wa mvua, nao haukosi kuzaa matunda. 9 Moyo wa mutu ni mudanganyifu kuliko vitu vyote; hauwezi kuponyeshwa, hakuna anayeweza kuuelewa! 10 Mimi Yawe ninapima akili na kuchunguza moyo wa mutu. Na hivyo ninamutendea kila mumoja, kulingana na mwenendo wake, kadiri ya matendo yake. 11 Mutu anayepata mali isiyokuwa ya usawa ni kama kwale anayelalia mayai ambayo hakutaga. Mali yanamwishia angali kijana, na kwa mwisho anageuka sawa mupumbafu. 12 Kuna kiti cha kifalme chenye utukufu kinachoinuka juu tangu mwanzo wa vyote, ndipo pahali petu patakatifu. 13 Ee Yawe, tumaini la Waisraeli, wote wanaokukataa wafezeheshwe. Wanaokuacha wewe watatoweka, kama majina yaliyoandikwa chini katika mavumbi, kwa maana wamekuacha wewe Yawe, unayekuwa chemichemi ya maji ya uzima. Maombi ya Yeremia 14 Uniponyeshe, ee Yawe, nami nitapona; uniokoe, nami nitaokoka; maana, wewe ndiwe sifa yangu. 15 Angalia jinsi watu wanavyoniambia: Vile vitisho vya Yawe viko wapi? Vifike basi! 16 Sikukukaza kutenda mabaya, wala sikutamani ile siku ya hasara ifike. Wewe mwenyewe unajua maneno niliyosema mbele yako. 17 Usiniletee hofu; maana wewe ndiwe kimbilio langu siku ya hasara. 18 Uwapatishe haya wale wanaonitesa, lakini usiniache mimi kupata haya. Uwafezeheshe watu hao, lakini usiniache mimi kufezeheka. Uwaletee ile siku ya hasara, uwaangamize kabisakabisa! 19 Yawe aliniambia hivi: Kwenda usimame kwenye Mulango wa Wanainchi, ambako wafalme wa Yuda wanapitia wanapoingia au kutoka Yerusalema. Uende vilevile kwenye milango yake yote ingine na kutangaza hivi: 20 Musikie neno la Yawe, enyi wafalme wa Yuda, ninyi watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema ambao wanaopitia kwenye milango hii. 21 Uwaambie kwamba: Yawe anasema hivi: Mufanye angalisho kwa ajili ya maisha yenu. Musibebe muzigo siku ya Sabato, au kuingiza muzigo katika Yerusalema kupitia kwenye milango ya muji. 22 Musibebe muzigo kutoka nyumba zenu siku ya Sabato wala kufanya kazi yoyote. Lakini muihesabu siku ya Sabato kuwa takatifu kama nilivyowaamuru babu zenu. 23 Ingawa hivyo babu zenu hawakunisikiliza wala kunitegea sikio, lakini walifanya vichwa vyao kuwa vigumu, wakakataa kusikia na kufuata maagizo yangu. 24 Lakini ninyi munisikilize mimi. Muache kuingiza muzigo wowote kupitia kwenye milango ya muji huu siku ya Sabato, muihesabu kuwa takatifu na kutofanya kazi. 25 Halafu, wafalme na wana wao watakaotawala nyuma juu ya kiti cha kifalme cha Daudi, wanaopanda juu ya farasi na magari yenye kukokotwa pamoja na watu wa Yuda na wakaaji wa Yerusalema, wataendelea kuingia ndani ya muji huu wakipitia kwenye milango hii. Nao muji huu utaikaliwa na watu siku zote. 26 Watu watakuja kutoka miji ya Yuda na maeneo ya kandokando ya Yerusalema, kutoka inchi ya kabila la Benjamina, kutoka Shefela, kutoka inchi ya milima na kutoka Negebu, wakileta sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka zingine za kawaida, sadaka ya mavuno na ya ubani wenye harufu nzuri pamoja na matoleo ya shukrani. Hivyo vyote watavileta katika nyumba ya Yawe. 27 Lakini musiponisikiliza na mukiacha kuihesabu siku ya Sabato kama siku takatifu, musipoacha kubeba mizigo na kuingia nayo kupitia milango ya Yerusalema siku ya Sabato, basi nitawakisha moto katika milango yake, nao utateketeza nyumba zote nzuri za Yerusalema, wala hautazimika. –Ni ujumbe wa Yawe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo