Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Yeremia 14 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Ukosefu mukali wa maji

1 Yawe akanitolea mimi Yeremia ujumbe juu ya ule ukosefu wa maji, akisema:

2 Watu wa Yuda wanaomboleza, miji yake inateketea. Watu wake wanaomboleza wakiikaa katika udongo na kilio cha Yerusalema kinapanda mpaka juu.

3 Wakubwa wake wanawatuma watumishi wao maji; watumishi wanakwenda kwenye visima, lakini hawapati maji; wanarudi na vyombo vitupu. Kwa ajili ya haya na mahangaiko wanaangalia chini.

4 Walimaji wanahuzunika kwa kuona jinsi udongo unavyokauka kwa ajili ya ukosefu wa mvua.

5 Hata kulungu anazaa katika pori na kuacha kitoto chake, kwa sababu hakuna majani.

6 Punda wa pori wanasimama kwenye vichwa vya vilima vyenye kukauka, wakivuta hewa kama mbweha; macho yao yanafifia kwa ukosefu wa majani.

7 Nao watu wanasema: Ingawa zambi zetu zinatoa ushuhuda juu yetu, utusaidie ee Yawe kwa ajili ya heshima ya jina lako. Maasi yetu ni mengi, tumetenda zambi mbele yako.

8 Wewe unayekuwa tumaini la Waisraeli, wewe unayetuokoa wakati wa taabu, namna gani unajifanya kama mugeni katika inchi, kama musafiri anayelala kwa usiku mumoja tu?

9 Namna gani unakuwa kama mutu aliyechanganyikiwa, kama shujaa asiyeweza kusaidia mutu? Ingawa hivyo wewe ee Yawe unakaa katikati yetu; nasi tunajulikana kwa jina lako, usituache.

10 Yawe anasema hivi juu ya watu hawa: Kweli wamependa sana kutangatanga, wala hawakujizuia; kwa hiyo mimi Yawe sipendezwi nao. Sasa nitayakumbuka makosa yao, na kuwaazibu kwa ajili ya zambi zao.

11 Yawe akaniambia hivi: Usiwaombee watu hawa uheri.

12 Hata wakifunga, sitayasikiliza maombi yao, na hata wakinitolea sadaka za kuteketeza kwa moto na sadaka zingine, mimi sitazikubali. Lakini nitawaangamiza kwa vita, njaa na ugonjwa mukali.

13 Kisha mimi nikasema: Ee Bwana wangu Yawe! Manabii wanawaambia watu hawa kwamba hakutakuwa vita wala njaa, kwa sababu umeahidi kwamba kutakuwa tu amani katika inchi hii.

14 Naye Yawe akaniambia: Hao manabii wanatoa unabii wa uongo kwa jina langu. Mimi sikuwatuma, wala sikuwaamuru, wala sikusema nao. Wanawatabiria maono ya uongo, maaguzi yao hayana maana yoyote, wao wanajitungia uongo wenyewe.

15 Kwa hiyo, Yawe anasema hivi juu ya hao manabii: Wanatabiri kwa jina langu, ingawa mimi sikuwatuma. Wanasema kwamba hakutakuwa vita wala njaa katika inchi hii: Manabii hao wataangamia kwa vita na kwa njaa.

16 Na hao ambao waliowatabiria mambo hayo, maiti zao zitatupwa katika barabara za Yerusalema wakiuawa kwa njaa na vita, wala hakutakuwa mutu wa kuwazika wao wenyewe, wake zao, wabinti zao na wana wao. Mimi nitawabebesha lazima ya uovu wao wenyewe.

17 Hivi ndivyo utakavyowaambia: Heri macho yangetoa machozi usiku na muchana, wala yasikome kutiririka, maana, watu wangu wamepata hasara kubwa, wameumizwa kidonda kikubwa sana.

18 Nikienda inje katika mbuga, ninaiona maiti ya waliouawa kwa vita; nikiingia ndani katika muji, ninaona tu maiti ya waliokufa kwa njaa! Manabii na makuhani wanashugulikia mambo yao katika inchi, lakini hawajui wanalofanya.

19 Ee Yawe, umekataa Yuda kabisa? Moyo wako umechukizwa na Sayuni? Kwa nini umetupiga vibaya kama hivi, hata hatuwezi kupona tena? Tulitazamia kupata amani, lakini hakuna kitu kizuri. Tulitazamia kupona, lakini tumepatwa na vitisho.

20 Tunakubali uovu wetu, ee Yawe, tunakubali uovu wa babu zetu, maana, tumekukosea wewe.

21 Usitutupe, kwa ajili ya heshima ya jina lako; usikizarau kiti chako cha kifalme chenye utukufu. Ukumbuke agano ulilofanya nasi, wala usilivunje.

22 Katikati ya miungu ya uongo ya mataifa nani anayeweza kunyesha mvua? Au, ni mbingu ndiyo inaweza kutoa manyunyu? Si ni wewe ee Yawe, Mungu wetu? Tunakuwekea wewe tumaini letu, maana ni wewe unayefanya haya yote.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan