Waroma 12 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kumutumikia Mungu kwa kweli 1 Basi wandugu zangu, kufuatana na vile Mungu alivyoonyesha huruma yake kwetu, ninawasihi mujitoe wenyewe kwake kuwa sadaka yenye uzima, takatifu na yenye kumupendeza. Hii ndiyo njia ya kweli ya kumwabudu. 2 Musifuate mwenendo wa siku hizi, lakini muache Mungu awabadilishe kwa kugeuza upya nia zenu, hata mukuwe na mawazo mapya. Kwa hiyo mutaweza kutambua mapenzi ya Mungu. Mutajua mambo gani yanayokuwa mema, yanayomupendeza Mungu na yanayokuwa makamilifu. 3 Kufuatana na neema niliyopewa na Mungu, ninawaambia ninyi wote: mutu asijiwazie kuwa na ukubwa kupita vile inavyomustahili. Lakini mukuwe na mawazo ya ukadirifu, kila mumoja kulingana na kipimo cha imani aliyopewa na Mungu. 4 Katika mwili mumoja kuna viungo vingi, lakini viungo hivi vyote havina kazi moja. 5 Hivi vilevile, sisi tunaokuwa wengi tumekuwa mwili mumoja katika kuungana kwetu na Kristo, na sisi wote ni viungo kila mumoja kwa mwingine. 6 Tuko na zawadi mbalimbali kwa kadiri ya neema tuliyopewa na Mungu. Aliyepewa zawadi ya unabii, anapaswa kutabiri kwa kadiri ya imani yake. 7 Aliyepewa zawadi ya utumishi, atumike. Aliyepewa zawadi ya kufundisha, afundishe. 8 Aliyepewa zawadi ya kuonya wengine, awaonye. Aliyepewa zawadi ya kutoa, atoe kwa moyo mweupe. Anayesimamia wengine, awasimamie kwa bidii. Aliyepewa zawadi ya kuhurumia wengine, afanye vile kwa furaha. 9 Upendo wenu ukuwe pasipo udanganyifu. Muchukie chochote kinachokuwa kibaya, mushikamane na kinachokuwa chema. 10 Mupendane ninyi kwa ninyi kwa kweli kama vile wandugu, nanyi muheshimiane ninyi kwa ninyi. 11 Musikuwe wavivu katika kazi lakini mukuwe na bidii, mukimutumikia Bwana kwa juhudi. 12 Mufurahi mukiwa na tumaini, muvumilie katika mateso, mudumu katika kuomba. 13 Muwasaidie watu wa Mungu katika mahitaji yao na muwakaribishe wageni. 14 Mumwombe Mungu awabariki wale wanaowatesa; muwaombee baraka wala musiwalaani. 15 Mufurahi pamoja na wenye kufurahi. Mulie pamoja na wenye kulia. 16 Mukuwe na masikilizano kati yenu. Musikuwe na nia ya kujitukuza, lakini mukubali kuishi katika unyenyekevu. Musijiwazie kuwa wenye akili sana. 17 Musimurudishie mutu ubaya kwa ubaya. Mukuwe na roho ya kufanya mema mbele ya watu wote. 18 Kama ikiwezekana, kwa upande wenu, muishi katika amani na watu wote. 19 Wandugu wapendwa, musilipize kisasi ninyi kwa ninyi, lakini mumwachie Mungu wakati wa kutenda kufuatana na kasirani, maana imeandikwa katika Maandiko Matakatifu: “Ni kazi yangu kulipiza kisasi. Ni mimi nitakayelipiza.” 20 Lakini kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Adui yako akisikia njaa, umupe chakula; kama akisikia kiu, umupe kinywaji. Maana kwa kufanya hivi utamupatisha haya kama vile ungemubebesha makaa ya moto juu ya kichwa.” 21 Usijiachilie kushindwa na ubaya, lakini ushinde ubaya kwa kutenda mema. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo