Walawi 27 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Sheria juu ya matoleo 1 Yawe akamwambia Musa: 2 Uwaambie Waisraeli hivi: Mutu akifanya kiapo cha kumutolea Yawe mwanadamu, mutu huyu anaweza kuondoa kiapo chake kwa kulipa kipimo cha feza kinachokadiriwa kama hivi: 3 Mwanaume wa miaka makumi mbili mpaka miaka makumi sita atakombolewa kwa feza shekeli makumi tano kulingana na kipimo cha Pahali Patakatifu. 4 Kama ni mwanamuke, atakombolewa kwa feza shekeli makumi tatu. 5 Kama mutu huyu ni wa miaka kati ya mitano na makumi mbili atakombolewa kwa feza shekeli makumi mbili kama ni kijana na shekeli kumi za feza kama ni binti. 6 Ikiwa ni mutoto wa umri wa kati ya mwezi mumoja na miaka mitano atakombolewa kwa shekeli tano za feza kama ni kijana na shekeli tatu za feza kama ni binti. 7 Ikiwa mutu huyu umri wake ni zaidi ya miaka makumi sita, bei yake itakuwa ni shekeli kumi na tano za feza, kama ni mwanaume na shekeli kumi za feza kama ni mwanamuke. 8 Lakini ikiwa mutu huyu ni masikini na hawezi kulipa malipo yake, basi, mutu yule atapelekwa kwa kuhani. Kuhani atapima bei yake kulingana na uwezo wa huyo aliyefanya kiapo. 9 Ikiwa kiapo chenyewe kinaelekea nyama wa namna ambayo watu wanamutolea Yawe sadaka, basi nyama huyo anakuwa kitu kitakatifu. 10 Hairuhusiwi kumubadilisha nyama huyo na mwingine yeyote, muzuri kwa mubaya au mubaya kwa muzuri. Kama akimubadilisha na nyama mwingine, wote wawili watakuwa watakatifu. 11 Kama kiapo hicho kinaelekea nyama muchafu wa aina ambayo hairuhusiwi kumutolea Yawe, basi, mutu aliyemutoa, atamuleta kwa kuhani, 12 naye kuhani ataamua bei yake kulingana na uzuri au ubaya wake. Jinsi kuhani atakavyoamua, ndivyo itakavyokuwa. 13 Lakini ikiwa mwenyeji anataka kumukomboa, basi, ataongeza asili mia makumi mbili ya bei ya nyama huyo. 14 Mutu akitakasa nyumba yake kuwa takatifu kwa Yawe, kuhani ataamua bei yake kulingana na uzuri au ubaya wake. Jinsi atakavyoamua, ndivyo itakavyokuwa. 15 Kama huyo mutu aliyeitakasa akitaka kuikomboa hiyo nyumba, basi, ataongeza asili mia makumi mbili ya bei yake, nayo itakuwa mali yake. 16 Mutu akitakasa shamba lake, ambalo ni urizi wake, kwa ajili ya Yawe, basi, bei yake itapimwa kulingana na mbegu zinazotumiwa kwa kupanda shamba hilo. Kwa kila kilo makumi mbili za shayiri bei yake itakuwa shekeli makumi tano za feza. 17 Kama akitakasa shamba lake katika mwaka wa kukumbuka miaka makumi tano, bei yake ilingane na vipimo vyenu. 18 Lakini kama akilitakasa kisha mwaka huo, basi, kuhani ataamua bei yake kulingana na miaka inayobaki kufikia mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano na bei yake ipunguzwe. 19 Kama mwenyeji akitaka kulikomboa, basi, aongeze asili mia makumi mbili ya bei ya shamba hilo, na kisha litakuwa mali yake. 20 Lakini kama hataki kulikomboa au amemwuzishia mutu mwingine, basi, shamba hilo lisikombolewe tena. 21 Katika mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano shamba hilo litaachiliwa na kuwa la Yawe milele. Kuhani ndiye atakayelirizi. 22 Kama mutu akitakasa shamba alilonunua, ni kusema sio lake kwa urizi, 23 kuhani ataamua bei ya shamba hilo kwa kulingana na miaka inayobaki kufikia mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano na mutu huyo atalipa bei yake kama ni kitu kitakatifu kwa Yawe. 24 Lakini katika mwaka wa ukumbusho wa miaka makuni tano, shamba hilo lirudishiwe yule mutu aliyeliuzisha. 25 Kila bei itapimwa kwa kipimo cha uzito cha shekeli kulingana na kipimo cha Pahali Patakatifu: uzito wa gera makumi mbili ni sawa na uzito wa shekeli moja. 26 Hairuhusiwi kumutakasa muzaliwa wa kwanza wa nyama. Kufuatana na sheria, huyo ni wa Yawe, akuwe ni ngombe au kondoo. 27 Kama ni nyama muchafu, mwenyeji atamununua kwa kulingana na jinsi munavyomupima na ataongeza asili mia makumi mbili ya bei ya nyama huyo. Kama hakombolewi, basi atauzishwa kulingana na vipimo vyenu. 28 Lakini kitu chochote kilichotakaswa kwa Yawe, kama ni mutu au nyama au kitu kilichopatikana kwa urizi, hakitauzishwa wala kukombolewa. Chochote kilichotakaswa kwa Yawe ni kitakatifu kabisa. 29 Mutu yeyote aliyetakaswa kwa Yawe asikombolewe. Sharti auawe. 30 Zaka za mazao ikuwe ni ngano au matunda ya miti, yote ni mali ya Yawe. Yote ni takatifu kwa Yawe. 31 Kama mutu akitaka kukomboa zaka yake, atalipa bei yake na kuongeza asili mia makumi mbili ya bei ya zaka hiyo. 32 Kuelekea mifugo, kila nyama wa kumi ni mutakatifu kwa Yawe. 33 Mutu yeyote hana ruhusa ya kuuliza kama nyama huyo ni muzuri au mubaya wala nyama huyo hatabadilishwa na mwingine. Kama akibadilishwa na mwingine, nyama wote wawili watakuwa watakatifu. Hawatakombolewa. 34 Hizo ndizo amri ambazo Yawe alimwamuru Musa kusudi awaambie Waisraeli kwenye mulima Sinai. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo