Walawi 25 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mwaka wa saba ( Kumb 15.1-11 ) 1 Yawe alimwambia Musa kule juu ya mulima Sinai: 2 Uwaambie Waisraeli hivi: Mutakapofika katika inchi ninayowapa mimi Yawe, kila mwaka wa saba inchi itapumzishwa isilimwe kwa heshima ya Yawe. 3 Kwa muda wa miaka sita mutalima udongo, mutapanda, mutakata matawi ya mizabu yenu na kuvuna mazao yenu. 4 Lakini mwaka wa saba utakuwa ni Sabato ya mapumziko, ni Sabato ya Yawe. Musipande chochote wala kukata matawi ya mizabibu yenu. 5 Chochote kinachoota peke yake musikivune wala kuchuma zabibu kutoka miti isiyokatwa matawi. Huo utakuwa mwaka wa kupumzisha udongo. 6 Hata hivyo mwaka huo wa mapumziko ya inchi utawapatia chakula ninyi wenyewe, watumwa wenu na wajakazi, watumishi na wageni wanaokaa kati yenu. 7 Inchi itakulisha nyama wenu wa kufugwa na nyama wa pori wanaokaa kati yenu. Sikukuu ya miaka makumi tano 8 Mutahesabu miaka saba mara saba na jumla yake ni miaka makumi ine na tisa. 9 Kisha, katika siku ya kumi ya mwezi wa saba ambayo ni siku ya kufanyiwa upatanisho mutatuma mutu kupiga baragumu katika inchi yote. 10 Mwaka wa makumi tano mutauheshimu kwa kutangaza uhuru kwa watumwa wote katika inchi. Mwaka huo utakuwa ni sikukuu ya ukumbusho wa miaka makumi tano. Kila mumoja wenu atarudilia mali yake na jamaa yake. 11 Kwa sababu mwaka huo ni wa sikukuu ya ukumbusho wa miaka makumi tano, musipande mbegu au kuvuna chochote kinachoota chenyewe wala kuchuma zabibu kutoka miti musiyokata matawi. 12 Mwaka huo ni wa sikukuu kwenu, utakuwa mwaka mutakatifu. Hivyo mutakula yale yanayoota yenyewe katika mashamba. 13 Katika mwaka huo chochote ambacho kiliuzishwa kinapaswa kirudishwe kwa mwenyeji. 14 Unaponunua au kuuzisha shamba kwa mwenzako usimupunje. 15 Bei ya shamba inapaswa kulingana na miaka mbele ya kurudishwa kwa mwenyeji. 16 Kama miaka ni mingi utaongeza bei na kama miaka hiyo ni michache utapunguza bei, maana bei yake itapimwa kulingana na mazao anayokuuzishia. 17 Musipunjane, lakini, mutamwogopa Mungu wenu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. 18 Kwa hiyo, mutafuata masharti yangu na kutimiza maagizo yangu, kusudi mupate kuendelea kuishi kwa usalama katika inchi. 19 Inchi itatoa mazao yake nanyi mutakula na kushiba na kuishi mule kwa usalama. 20 Lakini labda mutafikiri: Tutakula nini katika mwaka wa saba ijapokuwa haturuhusiwi kupanda wala kuvuna mazao yetu? 21 Basi! Mimi nitabariki inchi katika mwaka wa sita nayo itawapa mazao ya kuwatoshelea kwa miaka mitatu. 22 Mutakapopanda katika mwaka wa nane mutakuwa munakula mazao ya zamani na mutaendelea kula tu hata mwaka wa tisa mutakapoanza tena kuvuna. Madaraka ya kukomboa shamba 23 Musiuzishe mashamba kabisa, maana hiyo ni mali yangu na ninyi ni wageni na wasafiri katika inchi yangu. 24 Ndiyo maana katika inchi yote mutakuwa na utaratibu wa kukomboa mashamba. 25 Kama ndugu yako anakuwa masikini, akiuzisha shamba lake, basi, ndugu yake wa karibu mwenye madaraka ya kulikomboa, atalikomboa. 26 Ikiwa mutu yule hana ndugu mwenye madaraka ya kulikomboa, lakini nyuma akakuwa tajiri na kupata uwezo wa kulikomboa shamba lake, 27 basi, atahesabu miaka tangu alipoliuzisha na kulipa garama zake. Yule mutu aliyelinunua anapaswa kumurudishia. 28 Lakini ikiwa hana uwezo wa kulikomboa, basi, litabaki katika mikono ya yule aliyelinunua mpaka mwaka wa sikukuu ya ukumbusho wa miaka makumi tano. Katika mwaka huo, mali hiyo iachiliwe na kurudishiwa kwa yule mutu aliyeiuzisha. 29 Kama mutu akiuzisha nyumba yake ya kukaa inayokuwa ndani ya muji uliojengewa ukuta, ataweza kuikomboa katika kipindi cha mwaka mumoja tangu alipoiuzisha. Kwa mwaka huo muzima atakuwa na haki ya kuikomboa. 30 Kama nyumba inayokuwa katika muji uliojengewa ukuta haikukombolewa kwa muda wa mwaka mumoja, basi, itakuwa mali ya yule aliyeinunua milele katika vizazi vyao vyote, wala haitarudishwa katika mwaka wa sikukuu ya kukumbuka miaka makumi tano. 31 Lakini nyumba za vijiji ambavyo havikuzungushiwa ukuta zitakuwa chini ya sheria ileile ya mashamba. Nyumba hizo zinaweza kukombolewa katika mwaka mumoja lakini ni lazima zirudishwe kwa wenyeji katika mwaka wa kukumbuka miaka makumi tano. 32 Hata hivyo, nyumba zinazokuwa katika miji Walawi wanayorizi zinaweza kukombolewa wakati wowote. 33 Ikiwa mumoja wa Walawi hatumii haki yake ya kukomboa, basi, nyumba iliyouzishwa ni lazima irudishwe kwa mwenyeji katika mwaka wa kukumbuka miaka makuni tano, maana nyumba zinazokuwa katika miji Walawi wanayorizi wamepewa kama sehemu yao kutoka kwa watu wa Israeli. 34 Lakini mashamba Walawi wanayorizi kwa pamoja, yasiuzishwe, maana huo ni urizi wao wa kudumu. Kuwakopesha wamasikini 35 Kama ndugu yako amekuwa masikini hata asiweze kujitunza mwenyewe akiwa pamoja nawe, unapaswa kumutunza aendelee kuishi nawe ndivyo utakavyomutendea mugeni au musafiri anayekuwa kwako. 36 Usimwombe akulipe faida ya namna yoyote. Lakini umwogope Mungu, naye ndugu yako apate kuishi pamoja nawe. 37 Usimukopeshe feza kwa kupata faida au kumupa chakula kusudi akulipe faida. 38 Mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyekutoa kutoka inchi ya Misri kwa kukupa inchi ya Kanana, na kusudi nami nikuwe Mungu wako. 39 Kama ndugu yako anayeishi karibu nawe amekuwa masikini, akijiuzisha kwako, usimufanye akutumikie kama mutumwa. 40 Atakaa nawe kama mutumishi wa kulipwa au kama musafiri. Atakutumikia mpaka kwa mwaka wa kukumbuka miaka makumi tano. 41 Kwa mwaka huo unapaswa kumupa uhuru wake arudi kwa jamaa yake na urizi wa wazee wake, umwache pamoja na jamaa yake. 42 Kwa sababu Waisraeli ni watumishi wangu ambao niliwatoa katika inchi ya Misri, basi, wasiuzishwe kama watumwa. 43 Usimukamate ndugu yako kwa kinguvu, lakini utamwogopa Mungu wako. 44 Juu ya watumwa na wajakazi, unaweza kuwanunua kutoka kwa watu wa mataifa mengine jirani. 45 Unaweza vilevile kununua watumwa kutoka kwa wageni wanaokaa pamoja nawe na jamaa zao waliozaliwa katika inchi yenu, nao watakuwa mali yako. 46 Hao watumwa unaweza kuwapatia watoto wako wakuwe mali yao milele. Hao unaweza kuwafanya watumwa wako, lakini kuelekea ndugu yako Mwisraeli, usimutawale kwa kinguvu. 47 Kama mugeni au musafiri anayekaa kati yenu amekuwa tajiri na ndugu yako akiwa masikini na kujiuzisha kwa huyo mugeni au huyo musafiri au kwa mumoja wa jamaa zao, 48 anaweza kukombolewa kisha kujiuzisha, mumoja wa wandugu zake anaweza kumukomboa. 49 Mujomba wake anaweza vilevile kumukomboa, au binamu yake au ndugu wa karibu katika ukoo wake. Anaweza vilevile kujikomboa yeye mwenyewe kama akiwa tajiri. 50 Yeye akishirikiana na yule aliyemununua, atahesabu miaka tangu alipojiuzisha mpaka mwaka wa kukumbuka miaka makumi tano. Malipo ya kuachiliwa huru kwake italingana na miaka aliyomutumikia. Muda ambao amekuwa mutumwa wa bwana wake utapimwa kama muda wa mutumishi wa kulipiwa. 51 Kama hesabu ya miaka mpaka mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano ni kubwa zaidi, basi atarudisha sehemu kubwa ya bei aliyolipiwa. 52 Kama miaka michache imepunguka mbele ya kufikia kwa sikukuu ya ukumbusho wa miaka makumi tano, atahesabu sehemu ya bei iliyobaki kulingana na miaka hiyo na kumulipa hayo malipo. 53 Muda wote anapokuwa kwa bwana wake anapaswa kutendewa kama mutumishi wa mushahara kila mwaka. Huyo aliyemununua asimutendee kwa kinguvu. 54 Lakini ikiwa mutu huyu na jamaa yake hakukombolewa kwa njia hizo, basi apewe uhuru wake katika mwaka wa ukumbusho wa miaka makumi tano. 55 Waisraeli ni watumishi wangu, maana niliwatoa katika inchi ya Misri. Mimi ni Yawe, Mungu wenu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo