Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Walawi 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kutenda mema

1 Yawe akamwambia Musa:

2 Uwaambie Waisraeli wote pamoja hivi: Mukuwe watakatifu maana mimi Yawe, Mungu wenu, ni mutakatifu.

3 Kila mumoja wenu anapaswa kuheshimu mama yake na baba yake, na kushika Sabato zangu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu.

4 Musigeukie sanamu za miungu, wala musijitengenezee sanamu za kuyeyushwa za miungu. Mimi ni Yawe, Mungu wenu.

5 Munaponitolea mimi Yawe sadaka za amani, mutanitolea kama vile inavyotakiwa kusudi mupate kukubaliwa.

6 Sadaka hiyo inapaswa kuliwa siku hiyohiyo inapotolewa au kesho yake. Chochote kinachobaki mpaka kwa siku ya tatu kinapaswa kuteketezwa kwa moto.

7 Kama sehemu ya nyama yake ikikuliwa siku ya tatu, tendo hilo ni chukizo na sadaka hiyo haitakubaliwa.

8 Naye atakayekula nyama hiyo anapaswa kubeba lazima ya uovu wake kwa sababu amechafua kitu kitakatifu cha Yawe. Mutu huyo atatengwa na watu wake.

9 Utakapovuna mavuno ya inchi yako, usivune kabisa mpaka kwenye mupaka wa shamba wala usirudi nyuma kukusanya mabaki.

10 Musirudie kukusanya kila kitu katika shamba la mizabibu, wala usiokote zabibu zilizoanguka chini. Utawaachia wamasikini na wageni. Mimi ni Yawe, Mungu wenu.

11 Musiibe, musidanganye wala kuambiana uongo.

12 Musiape uongo kwa jina langu na kuchafua jina la Mungu wenu. Mimi ni Yawe.

13 Usimutese mwenzako wala kumwibia. Usikae na mushahara wa mutumishi wako usiku kucha mpaka asubui.

14 Usimulaani kiziwi wala kuweka kizuizi mbele ya kipofu, lakini umwogope Mungu wako. Mimi ni Yawe.

15 Unapotoa hukumu uamue kwa haki, usimupendelee masikini wala kumwogopa mwenye cheo. Lakini hukumu mwenzako kwa haki.

16 Usipitepite hata kidogo ukiwachongea watu wa jamaa yako. Usitie maisha ya mwenzako katika hatari ya kifo kwa maneno yako. Mimi ni Yawe.

17 Usimuchukie ndugu yako ndani ya moyo wako, lakini upatane siku zote na mwenzako kusudi usitende zambi.

18 Usijilipize kisasi au kuwa na kinyongo juu ya wazao wa watu wako lakini umupende mwenzako kama vile unavyojipenda wewe mwenyewe. Mimi ni Yawe.

19 Unapaswa kuyashika masharti yangu. Usiiache mifugo yako ipandiwe na nyama wa aina nyingine. Usipande mbegu za aina mbili katika shamba lako. Usivae nguo iliyofumwa kwa aina mbili za nguo.

20 Mwanaume akilala na mwanamuke mujakazi ambaye amechumbiwa na mwanaume mwingine, lakini bado hajakombolewa wala kupewa uhuru, uchunguzi ufanywe. Lakini wasiuawe kwa sababu mwanamuke huyo hakukuwa bado huru.

21 Mwanaume huyo ataleta mbele ya hema la mukutano sadaka yake ya kondoo dume kwa ajili ya kosa na kunitolea mimi Yawe.

22 Kuhani atamufanyia ibada ya upatanisho kwa kutumia kondoo huyo mbele ya Yawe kwa ajili ya zambi aliyotenda, naye atasamehewa zambi hiyo aliyotenda.

23 Mutakapofika katika inchi ya Kanana na kupanda aina zote za miti ya matunda, matunda hayo hamutayakula. Hamutaruhusiwa kuyakula kwa muda wa miaka mitatu.

24 Katika mwaka wa ine matunda yake yote yatakuwa matakatifu, yatatolewa kuwa sadaka ya sifa, kwa Yawe.

25 Lakini matunda ya kuanzia mwaka wa tano hayo munaweza kuyakula na mavuno yenu yataongezeka. Mimi ni Yawe, Mungu wenu.

26 Musikule nyama yoyote pamoja na damu. Musifanye ulozi wala kuaguza.

27 Musikate kwa kiviringo nywele za pembeni ya kichwa wala kunyoa pembe za ndevu zenu.

28 Musijitie chanjo juu ya mwili wenu kwa ajili ya kuomboleza au kujikatakata chanjo yoyote juu ya mwili. Mimi ni Yawe.

29 Usimuchafue binti yako kwa kumufanya kahaba, inchi nzima isipate kuangukia katika ukahaba na hivyo kujaa uovu.

30 Mutashika Sabato zangu na kuheshimu Pahali pangu Patakatifu. Mimi ni Yawe.

31 Musiwaendee waaguzi wa mizimu wala wachawi kwa kuwaomba wawaaguzie. Mukifanya hivi, mutajichafua. Mimi ni Yawe, Mungu wenu.

32 Unapokuwa mbele ya muzee unapaswa kusimama kwa kumupa heshima yake, nawe umwogope Mungu wako. Mimi ni Yawe.

33 Kama kuna mugeni katika inchi yako usimutendee vibaya.

34 Huyo mugeni anayekaa nawe atakuwa kwako kama vile mwenyeji nawe utamupenda kama vile unavyojipenda mwenyewe, kwa sababu nawe ulikuwa mugeni katika inchi ya Misri. Mimi ni Yawe, Mungu wenu.

35 Usikose kuamua kwa haki juu ya vipimo vya urefu, uzito na ujazo.

36 Munapaswa kutumia mizani ya kweli na vipimo vinavyokuwa vya kweli. Mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatoa katika inchi ya Misri.

37 Munapaswa kushika na kutimiza masharti yangu na maagizo yangu. Mimi ni Yawe.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan