Walawi 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Sadaka za kuteketezwa 1 Yawe akamwita Musa na kuongea naye katika hema la mukutano, akamwambia: 2 Uwaambie Waisraeli kwamba kama mutu anapenda kumutolea Yawe sadaka ya nyama, nyama huyo atamuchagua kutoka kundi lake la ngombe, kondoo au mbuzi. 3 Kama sadaka mutu anayotoa ni ya kuteketezwa kwa moto, atamuchagua nyama dume asiyekuwa na kilema kutoka kundi lake, atamutolea mbele ya mulango wa hema la mukutano kusudi apate kukubaliwa na Yawe; 4 ataweka mukono wake juu ya kichwa cha nyama wa sadaka ya kuteketezwa kwa moto, ambayo itakubaliwa kwa ajili ya kumufanyia huyo mutu upatanisho. 5 Kisha, atamuchinja huyo ngombe mbele ya Yawe. Nao makuhani wazao wa Haruni wataichukua damu na kuinyunyizia mazabahu inayokuwa kwenye mulango wa hema la mukutano, pande zake zote. 6 Huyo mutu atachuna huyo nyama wa sadaka ya kuteketezwa na kumukata vipandevipande. 7 Hao makuhani wazao wa Haruni watazipanga kuni juu ya mazabahu na kuwasha moto. 8 Kisha makuhani hao watatwaa vile vipande vya nyama, kichwa na mafuta, na kuviweka juu ya kuni juu ya mazabahu. 9 Lakini matumbotumbo na miguu ya nyama yule vitasafishwa kwa maji. Kuhani atateketeza sadaka yote juu ya mazabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. 10 Kama sadaka yake ya kuteketezwa ataitwaa katika kundi la kondoo au mbuzi, basi atachagua dume asiyekuwa na kilema. 11 Atamuchinjia upande wa kaskazini wa mazabahu, mbele ya Yawe, hao makuhani wazao wa Haruni watainyunyizia mazabahu damu pande zake zote. 12 Kisha yule mutu atamukata vipandevipande, akivitenga kichwa pamoja na mafuta yake, na kuhani ataviweka kwenye moto juu ya mazabahu. 13 Lakini matumbotumbo na miguu yake atavisafisha kwa maji. Kuhani ataiteketeza yote juu ya mazabahu. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. 14 Ikiwa anamutolea Yawe sadaka ya kuteketezwa ya ndege, basi, ataleta sadaka yake ya hua au kitoto cha njiwa. 15 Kuhani ataleta ndege huyo kwenye mazabahu, atakongonyoa kichwa chake na kukiteketeza juu ya mazabahu. Damu yake itanyunyiziwa kwenye ubavu wa mazabahu. 16 Kibofu chake pamoja na uchafu wake ataviondoa na kuvitupa upande wa mashariki wa mazabahu ambako majivu yanawekwa. 17 Atamushika mabawa na kumupasua, lakini asimwachanishe vipande viwili. Kisha, kuhani atamuteketeza kwenye mazabahu, juu ya kuni. Hiyo ni sadaka ya kuteketezwa kwa moto yenye harufu nzuri ya kumupendeza Yawe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo