Wakolosayi 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Kwa kuwa mumefufuliwa pamoja na Kristo, mutafute mambo yanayokuwa juu, pahali Kristo anapoikaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu. 2 Mushugulikie sana mambo yanayokuwa juu, lakini musishugulikie mambo yanayokuwa katika dunia. 3 Kwa maana ninyi mumekufa na uzima wenu umefichwa pamoja na Kristo katika Mungu. 4 Kristo ndiye uzima wenu wa kweli, naye atakapoonekana tena, basi ninyi mutaonekana pamoja naye katika utukufu wake. Maisha ya zamani na maisha ya sasa 5 Basi mutupilie mbali mambo yote ya kidunia yanayokuwa ndani yenu: uasherati, uchafu, nia mbaya, tamaa mbaya na tamaa ya mali inayokuwa sawa vile kuabudu sanamu. 6 Kwa sababu ya makosa haya, kasirani ya Mungu itawaangukia wale wanaomwasi. 7 Zamani, ninyi muliishi kwa namna ile mulipokuwa mukitawaliwa na mambo hayo ya zambi. 8 Lakini sasa mutupilie mbali mambo haya yote: kasirani, chuki, uovu, masingiziano na musiseme neno lolote baya. 9 Musiambiane uongo ninyi kwa ninyi, kwa maana mumeondoa utu wenu wa zamani pamoja na matendo yake 10 na kuvaa utu mupya. Utu ule unaendelea kufanywa upya kila mara kufuatana na mufano wa Mungu anayekuwa muumba wake, kusudi mupate kumujua hakika. 11 Kwa hiyo hakuna tena tofauti kati ya watu wa mataifa mengine na Wayuda, wenye kutahiriwa na wasiotahiriwa, wageni, washenzi, watumwa na watu huru. Lakini Kristo ni yote naye yuko katika wote. 12 Ninyi ni watu wa Mungu, yeye amewapenda na kuwachagua kwa ajili yake mwenyewe. Kwa hiyo, mukuwe na moyo wa huruma, wema, unyenyekevu, upole na uvumilivu. 13 Muvumiliane na kusameheana ninyi kwa ninyi wakati wowote mutu anapokuwa na neno la kumushitaki mwingine. Munapaswa kusameheana kama vile Bwana alivyowasamehe ninyi. 14 Zaidi ya mambo haya yote, mukuwe na upendo, maana upendo unaunganisha kila kitu katika umoja unaokuwa mukamilifu. 15 Amani ya Kristo itawale katika mioyo yenu; maana ni kwa ajili ya hiyo ninyi mumeitwa kuwa katika mwili mumoja. Mukuwe wenye shukrani. 16 Habari za Kristo zikae ndani yenu kwa uwingi. Mufundishane na mushauriane kwa hekima. Mumwimbie Mungu kwa moyo wenu wote na kumushukuru kwa zaburi na nyimbo za kiroho. 17 Kila kitu munachofanya au kusema, mufanye yote kwa jina la Bwana Yesu, kwa kumushukuru Mungu Baba kwa njia yake. Maonyo katika maisha mapya 18 Wake muwatii waume wenu kama vile inavyostahili mbele ya Bwana. 19 Waume muwapende wake wenu nanyi musiwatendee kwa ukali. 20 Watoto muwatii wazazi wenu katika mambo yote, kwa maana jambo hili linamupendeza Bwana. 21 Ninyi wababa musiwakasirikishe watoto wenu, kusudi musiwavunje moyo. 22 Ninyi watumwa, muwatii wabwana wenu katika mambo yote hapa katika dunia. Musiwatii tu wakati wanapowaangalia ninyi kama mungetaka tu kujipendeza mbele yao, lakini muwatii kwa moyo mwema, kwa sababu munamuheshimu Bwana. 23 Na kila kitu munachofanya, mukifanye kwa moyo wenu wote, kama vile wenye kumutumikia Bwana wala si watu. 24 Mukumbuke kwamba Bwana atawapa ninyi zawadi ile anayowawekea watu wake. Kwa maana Kristo ndiye Bwana wa kweli munayemutumikia. 25 Lakini yule anayefanya mabaya, atalipwa kufuatana na mabaya aliyotenda, kwa sababu Mungu hana upendeleo. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo