Wakolosayi 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Ninataka mujue jinsi ninavyofanya kazi kwa bidii kwa ajili yenu, kwa ajili ya waamini wa Laodikia na kwa ajili ya wote ambao hawajapata kuniona bado. 2 Ninapigana kusudi wapate kuwa na bidii na kuungana katika upendo. Na zaidi ya hii wapate kuwa na uhakika kabisa unaotokana na ufahamu mukamilifu. Hivi wataweza kujua siri ya Mungu, maana yake kumujua Kristo mwenyewe, 3 kwa maana hazina zote za hekima na elimu zimefichwa ndani yake. 4 Ninawaambia ninyi maneno haya kusudi mutu asiwadanganye kwa maneno matamu ya kupotosha. 5 Ijapokuwa mimi ni mbali nanyi kwa mwili, lakini mimi ni pamoja nanyi kwa roho, nami ninafurahi kuona namna munavyoishi katika utaratibu muzuri na kusimama imara katika imani mbele ya Kristo. Kujenga maisha juu ya Kristo 6 Basi kwa sababu mumemukubali Kristo kuwa Bwana wenu, muishi katika kuungana naye. 7 Mukuwe na mizizi ndani yake, mujijenge juu yake na kusimama imara katika imani sawa vile mulivyofundishwa. Na zaidi ya hii mukuwe wenye kushukuru sana. 8 Mujiangalie hata mutu asiwapotoshe kwa elimu yake ya udanganyifu mutupu inayotegemea desturi za watu na roho mbaya zinazotawala dunia, lakini haitegemei mafundisho ya Kristo. 9 Kwa maana ukamilifu wote wa Mungu uko ndani ya Kristo katika mwili wake. 10 Na kwa kuungana naye, ninyi mumepata kukamilika. Yeye ndiye anayetawala roho zote zenye mamlaka na uwezo. 11 Katika kuungana naye, mumetahiriwa wala si kwa mikono ya watu, lakini mumetahiriwa na Kristo, na kutahiriwa kule kumewakomboa toka katika hali zaifu ya kimwili. 12 Kwa maana mumezikwa pamoja na Kristo kwa njia ya ubatizo, nanyi mumefufuliwa vilevile pamoja naye, kwa sababu mumeamini uwezo wa Mungu, aliyemufufua. 13 Zamani mulikuwa mumekufa kwa sababu ya zambi zenu na kwa sababu mulikuwa watu wa mataifa mengine, wasiotahiriwa. Lakini sasa, Mungu amewapatia ninyi uzima pamoja na Kristo, naye ametusamehe zambi zetu zote. 14 Alifuta barua ya madeni yetu na sherti zilizotushitaki. Aliyafuta kabisa kwa kuyapigilia juu ya musalaba. 15 Mungu alinyanganya uwezo wa wakubwa na wenye mamlaka, naye akawaonyesha waziwazi, akiwatembeza kama wafungwa katika maandamano ya ushindi wa Mwana wake. 16 Basi, mutu asiwahukumu juu ya chakula au kinywaji, au juu ya kushika sikukuu fulani, ikiwa sikukuu ya Mwandamo wa Mwezi au siku ya Sabato. 17 Mambo hayo yote ni kivuli cha mambo yatakayokuja, lakini ukweli wa mambo yote ni Kristo mwenyewe. 18 Musikubali kuhukumiwa na mutu yeyote anayejionyesha kwa inje kuwa yeye ni munyenyekevu na mwenye kuabudu malaika. Mutu wa namna hii anatia sana maana juu ya maono anayopata, naye anajitapa bure juu ya mafikiri yake ya kimutu. 19 Mutu yule hashikamani na Kristo anayekuwa kichwa cha mwili. Chini ya uongozi wa Kristo, mwili muzima unakulishwa vizuri na kuunganishwa pamoja kwa njia ya maunganio na vifundo vyake, kusudi upate kukomaa kufuatana na mapenzi ya Mungu. Tusifuate kanuni zilizotungwa na watu 20 Ninyi mumekufa pamoja na Kristo na kukombolewa toka katika uwezo wa roho mbaya zinazotawala dunia. Kwa nini munaishi tena kama watu wa dunia mukilazimishwa kushika kanuni kama hizi: 21 “Usikule hiki”, “Usionje hiki,” “Usiguse hiki na hiki!” 22 Mambo hayo yote yanaelekea vitu vyenye kuharibika mara moja tu vinapotumiwa. Navyo vyote ni kanuni na mafundisho ya watu tu. 23 Hakika kanuni hizi zinaonekana kama za hekima kwa maana zinatokana na ibada ya kipekee ya watu wale pamoja na unyenyekevu wao na shurti zao za kuutesa mwili. Lakini hazifai kitu kwa kuzuiza tamaa za mwili. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo