Wakolosayi 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Salamu 1 Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo na kwa ndugu yetu Timoteo. Mimi niliitwa na Mungu kwa mapenzi yake kuwa mutume wa Yesu Kristo. 2 Tunawaandikia ninyi watu wa Mungu munaokaa katika muji Kolosayi, ninyi wandugu munaoungana na Kristo kwa uaminifu. Tunawatakia neema na amani toka kwa Mungu Baba yetu. Maombi ya kushukuru 3 Tunamushukuru Mungu, Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo kila mara tunapowaombea ninyi. 4 Hayo yote ni kwa maana tumesikia namna munavyomwamini Yesu Kristo na namna munavyowapenda watu wote wa Mungu. 5 Imani yenu na upendo wenu vinakuwa na musingi katika tumaini mulilowekewa mbinguni. Mulisikia juu ya tumaini lile mara ya kwanza wakati mulipohubiriwa ujumbe wa ukweli ni kusema Habari Njema. 6 Habari Njema ile inatoa matunda na kuenea katika dunia yote sawa vile ilivyofanya kwenu tangu siku ile muliposikia wakisema juu ya neema ya Mungu na kupata kuitambua inavyokuwa kweli. 7 Ni Epafra mutumishi mwenzetu mupenzi, ndiye aliyewafundisha ninyi habari zile. Yeye ni mutumishi mwaminifu wa Kristo kwa ajili yetu. 8 Yeye ndiye aliyetupatia habari za upendo wenu muliojaliwa na Roho. 9 Kwa sababu hii hatuchoki kuwaombea ninyi, tangu siku tuliposikia habari zenu. Tunamwomba Mungu awawezeshe kujua kabisa mapenzi yake na kuwajaza hekima na akili inayotoka kwa Roho wake. 10 Hivi, mutaweza kuishi sawa Bwana anavyotaka na kumupendeza katika mambo yote. Kwa njia hiyo mutafikia kufanya matendo mema ya kila namna na kuzidi kumujua Mungu. 11 Mungu atawatia nguvu kwa uwezo wake wenye utukufu, kusudi mupate kuvumilia kila kitu pasipo kuchoka. Basi kwa furaha, 12 mumushukuru Mungu Baba aliyewawezesha ninyi kuwa wenye kustahili kupokea sehemu yenu ya urizi aliowawekea watu wake katika ufalme wa mwangaza. 13 Kwa maana yeye ametuokoa toka katika uwezo wa giza, na kutuingiza katika ufalme wa Mwana wake mupendwa, 14 ambaye katika yeye tumekombolewa na kusamehewa zambi zetu. Kristo na kazi yake 15 Kristo ni mufano kamili wa Mungu asiyeonekana. Yeye ni muzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. 16 Kwa njia yake, Mungu aliumba vitu vyote vinavyokuwa mbinguni na katika dunia, vyenye kuonekana na visivyoonekana; ikiwa ni ufalme, ukubwa, utawala au mamlaka. Mungu aliumba vyote kwa njia yake na kwa ajili yake. 17 Kristo alikuwa yuko mbele vitu vyote havijakuwa, na kwa njia ya kuungana naye vyote vinashikamana. 18 Yeye ni kichwa cha kanisa linalokuwa mwili wake. Naye ndiye asili ya uzima wa mwili ule. Yeye ndiye mwanzo, muzaliwa wa kwanza, na ndiye aliyefufuka wa kwanza, kusudi akuwe wa kwanza juu ya vyote. 19 Kwa maana Mungu mwenyewe alitaka ukamilifu wake uonekane ndani ya mwana wake. 20 Kwa njia ya Mwana wake alitaka kupatanisha ulimwengu muzima naye. Kwa njia ya damu ya Mwana wake iliyomwangika juu ya musalaba, Mungu ameleta amani, hivi akapatanisha vitu vyote naye mwenyewe, vinavyokuwa katika dunia na katika mbingu. 21 Na ninyi zamani mulikuwa mbali na Mungu, mulikuwa waadui zake kwa sababu ya mafikiri na matendo yenu mabaya. 22 Sasa, Mungu amewapatanisha ninyi naye, kwa njia ya kufa kwa Mwana wake kimwili, kusudi awawezeshe kuonekana mbele yake mukiwa watakatifu, bila kilema wala kosa lolote. 23 Lakini, inawapasa ninyi kuendelea na musingi imara katika imani, musitikiswe na kupoteza lile tumaini mulilopata wakati muliposikia Habari Njema. Mimi Paulo nimewekwa kuwa mutumishi wa kuhubiri Habari Njema ile iliyokwisha kutangazwa kwa watu wote katika dunia. Kazi ya Paulo katika kanisa 24 Sasa ninafurahi kwa ajili ya mateso ninayopata juu yenu. Kwa njia ya kuteseka kwangu kimwili, ninatimiza mateso yaliyomubakilia Kristo kwa ajili ya mwili wake, maana yake kanisa. 25 Mimi nimekuwa mutumishi wa kanisa kufuatana na kazi ile Mungu aliyonipa kwa ajili yenu. Kazi yenyewe ni kutangaza Neno lake kwa ukamilifu. 26 Neno lile ndio ile siri aliyoificha tangu zamani za kale, lakini sasa ameifunua kwa watu wake. 27 Kwa maana Mungu alitaka kuwafunulia watu hao siri ya mupango wake wenye utajiri mukubwa alioufanya kwa ajili ya mataifa yote. Nayo siri ile ni kwamba Kristo ni ndani yenu, naye ndiye anayetuletea tumaini kwamba tutashiriki katika utukufu wa Mungu. 28 Ni kwa hiyo tunamutangaza Kristo kwa watu wote. Tunaonya na kufundisha kila mutu kwa hekima yote, kusudi tuwasaidie watu wote wapate kufikia kuwa wakamilifu katika kuungana kwao na Kristo. 29 Ni kwa sababu hiyo ninatumika na kupigana kwa uwezo ninaopewa na Kristo, unaoniwezesha kufanya kazi kwa nguvu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo