Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Wafilipi 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Unyenyekevu na ukubwa wa Kristo

1 Maisha yenu katika kuungana kwenu na Kristo si yanawatia ninyi nguvu? Nao upendo wake si unawafariji ninyi? Si munaishi katika ushirika na Roho Mutakatifu? Si muko na moyo mwema na wa huruma?

2 Basi munijaze na furaha tele, mukiwa na nia moja, na upendo mumoja, roho moja na wazo moja.

3 Musifanye jambo lolote kwa roho ya mapingano wala kwa kujivuna bure, lakini munyenyekeane kila mutu akimuhesabu mwenzake kuwa muzuri kuliko yeye mwenyewe.

4 Kila mutu asitafute faida yake mwenyewe, lakini atafute faida ya watu wengine.

5 Ndani yenu mukuwe na nia kama hii iliyokuwa ndani ya Kristo Yesu:

6 Tangu mwanzo yeye alikuwa na hali ya Mungu, lakini hakuona kwamba kuwa sawa na Mungu ni kitu cha kushikamana nacho.

7 Alitupilia hivi vyote, akatwaa hali ya mutumwa. Akatwaa mufano wa mutu, naye akaonekana katika hali ya kimutu.

8 Alijinyenyekeza na kutii mpaka kufa, ndiko kufa kwake juu ya musalaba.

9 Kwa hiyo Mungu naye akamwinua juu zaidi, akamupa jina lenye ukubwa kuliko majina yote,

10 kusudi kwa kuheshimu jina la Yesu, viumbe vyote vinavyokuwa katika mbingu, katika dunia na katika kuzimu, vipige magoti mbele yake,

11 na kila mutu akubali kwamba Yesu ni Bwana, naye Mungu Baba atatukuzwa kwa njia hiyo.


Kuwa kama mwangaza katika dunia

12 Basi wapendwa wangu, mulionyesha utii wenu siku zote wakati nilipokuwa kwenu, na sasa ingekuwa vema muendelee kufanya vile katika siku hizi ninapokuwa mbali nanyi. Mutumike kwa ajili ya wokovu wenu kwa woga na kutetemeka,

13 kwa maana Mungu anafanya kazi ndani yenu na kuwapa moyo wa kutaka na kutimiza mambo yanayolingana na mupango wake mwema.

14 Mufanye kila kitu bila manunguniko wala mabishano,

15 kusudi mupate kuwa bila kosa na kuwa na maisha safi. Hivi mutakuwa watoto wakamilifu wa Mungu wasiokuwa na kilema kati ya watu waovu na wapotovu wa dunia hii. Munapaswa kuangaza kati ya watu hawa kama vile nyota zinavyoangaza katika mbingu,

16 mukiwatangazia habari inayoleta uzima. Hivi nitapata sababu ya kujivuna Siku ile ya kurudia kwa Kristo kwa maana itakuwa kitambulisho cha kuhakikisha kwamba bidii yangu na kazi yangu havikupotea bure.

17 Hata nikitoa maisha yangu kuwa sadaka pamoja na imani yenu inayokuwa sadaka mbele ya Mungu, mimi ninafurahi na kushiriki pamoja nanyi wote.

18 Nanyi vilevile mufurahi na kushiriki pamoja nami katika furaha yenu.


Timoteo na Epafrodito

19 Kama Bwana Yesu akitaka, ninangojea kisha muda kidogo kuwatumia Timoteo, kusudi nipate kutiwa moyo na habari nitakazopata kutoka kwenu.

20 Ni yeye tu ndiye mafikiri yake yanapatana na yangu, naye anashugulika kweli na mambo yanayowaelekea.

21 Watu wengine wote wanatafuta faida yao wenyewe, lakini hawashuguliki na Yesu Kristo.

22 Munajua ninyi wenyewe namna Timoteo alivyojionyesha kwamba anastahili, kwa maana alitumika kazi ya kueleza Habari Njema pamoja nami kama vile mwana anavyotumika na baba yake.

23 Ninatumaini kumutuma kwenu pale pale nitakapojua yale yatakayonitokea juu ya kufungwa kwangu.

24 Nami ninamutumainia Bwana kwamba mimi mwenyewe nitakuja kuwaona bado kidogo.

25 Niliona vema kuwatumia ndugu yetu Epafrodito, anayeshiriki pamoja nami katika kazi na katika vita ya Habari Njema. Ni yeye ndiye muliyetumia kwa kunisaidia kufuatana na mahitaji niliyokuwa nayo.

26 Yeye yuko na hamu sana kuwaona ninyi wote, naye anahuzunika sana kwa sababu mulisikia kwamba alikuwa mugonjwa.

27 Alikuwa mugonjwa karibu kufa, lakini Mungu akamuhurumia, na si yeye peke yake, lakini mimi vilevile kusudi nisikuwe na huzuni juu ya ingine.

28 Hivi ninamutuma kwenu kwa haraka kusudi mupate kufurahi wakati mutakapomwona tena na huzuni yangu ipate kupunguka.

29 Basi mumupokee kwa furaha kubwa sana kwa jina la Bwana. Munapaswa kuwapa watu wa namna hii heshima,

30 kwa sababu yeye alikuwa karibu kufa kwa ajili ya kazi ya Kristo. Alihatarisha maisha yake kwa kuja kuniletea musaada ule ambao ninyi wenyewe musingeweza kunipatia.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan