Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Waefeso 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mwili mumoja

1 Kwa hivi basi, mimi ninayekuwa mufungwa kwa sababu ninamutumikia Bwana, ninawasihi muishi sawa inavyostahili kufuatana na mwito Mungu aliowatolea.

2 Mukuwe wanyenyekevu kabisa, wapole na wavumilivu. Muvumiliane ninyi kwa ninyi kwa upendo.

3 Mujikaze sana kuchunga umoja wa Roho, kwa amani inayowaunganisha.

4 Kuna mwili mumoja na Roho mumoja, vilevile kuna tumaini moja la mwito muliotolewa na Mungu.

5 Kuna Bwana mumoja, imani moja, ubatizo mumoja;

6 Mungu mumoja, Baba ya watu wote, anayekuwa juu ya wote, anayetumika kwa njia ya wote, na anayekaa ndani ya wote.

7 Lakini kila mutu kati yetu alipokea neema kadiri ya kipimo alichojaliwa na Kristo.

8 Kama vile Maandiko Matakatifu yanavyosema: “Alipopanda juu, alikamata wafungwa, aliwapatia watu zawadi.”

9 Basi, neno hili “alipanda juu,” lina maana gani? Maana yake ni kusema kwamba alishuka kwanza mpaka chini katika dunia.

10 Yule aliyeshuka ndiye yule yule aliyepanda juu sana kupita mbingu zote kusudi akamilike katika ulimwengu wote.

11 Ni yeye ndiye aliwapatia watu zawadi za kipekee. Amewaweka wamoja kuwa mitume, wengine kuwa manabii, wengine kuwa watangazaji wa Habari Njema, wengine kuwa wachungaji na walimu.

12 Yeye amefanya vile kwa kuwatayarisha watu wa Mungu kwa kazi ya utumishi kusudi mwili wa Kristo upate kujengwa.

13 Hivi, sisi wote tutafikia umoja wa imani yetu na wa kumujua kabisa Mwana wa Mungu; tutapata kukomaa na kufikia kipimo cha utimilifu wa Kristo.

14 Basi, hatutakuwa tena kama watoto, tukipeperushwa na kuvutwa na mafundisho ya kila aina yanayoletwa na watu wanaodanganya wengine na kuwapotosha kwa mayele yao.

15 Lakini tukitangaza ukweli kwa upendo, tutakomaa katika mambo yote na kufikia kuwa kama Kristo, ambaye ni kichwa.

16 Kwa uongozi wake, viungo vyote vya mwili vinashikamana kabisa, nao mwili wote muzima unashikamana vizuri kwa nguvu ya maunganio yake. Halafu, kila kiungo kinapotumika kama kinavyopaswa, mwili wote unakomaa na kujijenga katika upendo.

17 Basi, kwa jina la Bwana ninawaonya hivi: musiishi tena kama watu wa mataifa mengine, wanaofuata mawazo yao ya bure

18 na wenye mafikiri yaliyotiwa katika giza. Watu hawa hawashiriki katika uzima ule unaoletwa na Mungu, kwa sababu wao ni wapumbafu na wenye mioyo migumu.

19 Hawasikii tena haya hata kidogo nao wamejitoa katika mambo ya ovyo na kufanya bila kujizuiza mambo yote mabaya.

20 Lakini ninyi hamukujifunza vile juu ya Kristo!

21 Hakika mumesikia habari zake, nanyi mukiwa waamini mumefundishwa kufuatana na ukweli unaokuwa ndani ya Kristo.

22 Basi munapaswa kutupilia mbali ile hali yenu ya zamani, ule utu wenu wa zamani unaopotoka kufuatana na tamaa zake za udanganyifu.

23 Inafaa mufanywe upya katika roho zenu na katika nia zenu.

24 Mukuwe na hali mupya, inayoumbwa kwa mufano wa Mungu na inayoonekana katika maisha ya haki na utakatifu wa kweli.

25 Kwa hivi, muache uongo! Kila mumoja aseme ukweli kwa mwenzake, kwa maana sisi wote ni viungo vya mwili mumoja.

26 Kama mukikasirika, musianguke katika zambi, kasirani yenu isidumu muchana kutwa,

27 wala musimufungulie Shetani mulango.

28 Yule aliyekuwa akiiba, asiibe tena, lakini ajikaze kufanya kazi peke yake kwa usawa kusudi apate kuwasaidia wakosefu.

29 Musiseme neno lolote baya, lakini kama ni lazima museme tu maneno mazuri na ambayo yanasaidia kuwajenga wengine na yanayoleta neema kwa wale wanaoyasikia.

30 Musihuzunishe Roho Mutakatifu wa Mungu; kwa maana Roho ni kitambulisho kilichowekwa juu yenu kwa kuhakikisha kwamba ninyi ni watu wake mpaka siku Mungu atakapowakomboa.

31 Mutupilie mbali nanyi nia zote za uadui, chuki, kasirani, fujo na masingizio. Mutupilie mbali ubaya wa kila namna!

32 Lakini mutendeane wema ninyi kwa ninyi; musameheane kama Mungu alivyowasamehe ninyi kwa njia ya Kristo.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan