Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Waefeso 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Salamu

1 Barua hii inatoka kwangu mimi Paulo. Mimi niliyeitwa kwa mapenzi ya Mungu kuwa mutume wa Yesu Kristo. Ninawaandikia ninyi watu wa Mungu munaokaa Efeso, munaokuwa waaminifu katika kuungana na Yesu Kristo.

2 Ninawatakia neema na amani toka kwa Mungu Baba yetu na kwa Bwana Yesu Kristo.


Baraka tunazopewa kwa njia ya Kristo

3 Asifiwe Mungu, Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo! Yeye ndiye aliyetupatia baraka za kiroho za kila namna kutoka katika eneo la mbingu kwa njia ya kuungana kwetu na Kristo.

4 Mbele ya kuumbwa kwa dunia, Mungu alituchagua kuwa watu wake kwa njia ya kuungana kwetu na Kristo, kusudi tukuwe watakatifu na pasipo kilema mbele yake. Kwa sababu ya upendo wake,

5 Mungu amekusudia tangu zamani kutukubali sisi kuwa watoto wake kwa njia ya Yesu Kristo. Alifanya vile kufuatana na mapenzi yake.

6 Basi tumusifu Mungu kwa sababu ya utukufu wa neema yake aliyotujalia kwa njia ya Mwana wake mupendwa.

7 Kwa njia ya damu ya Kristo, sisi tumekombolewa, maana yake zambi zetu zimesamehewa. Hivi Mungu ameonyesha uwingi wa neema yake

8 akitupatia hekima na akili kamili.

9 Ametujulisha mipango yake iliyokuwa imefichwa; ndiyo ile aliyokusudia kwa mapenzi yake tangu mbele kwamba ataitimiza kwa njia ya Kristo.

10 Kusudi la mupango ule utakaotimia kwa wakati uliowekwa, ni kukusanya viumbe vyote vinavyokuwa mbinguni na katika dunia chini ya utawala wa Kristo.

11 Mungu amefanya kila kitu kufuatana na kusudi na mapenzi yake. Yeye ametuchagua kwa njia ya kuungana kwetu na Kristo, kusudi tukuwe watu wake.

12 Kwa hiyo sisi tuliotangulia kumutumainia Kristo, tumusifu Mungu kwa ajili ya utukufu wake!

13 Ninyi vilevile, wakati muliposikia ujumbe wa kweli, maana yake Habari Njema iliyowaletea wokovu, mukamwamini Kristo. Naye Mungu akawapatia Roho Mutakatifu aliyeahidi kuwa kitambulisho cha kuhakikisha kwamba ninyi ni watu wake kabisa.

14 Yule Roho ni rehani ya urizi aliowawekea watu wake. Na jambo hili linahakikisha kwamba Mungu atakomboa kabisa wote wanaokuwa wake. Tumusifu kwa ajili ya utukufu wake.


Maombi ya Paulo

15 Kwa sababu hiyo, tangu niliposikia namna munavyomwamini Bwana Yesu na namna munavyowapenda watu wote wa Mungu,

16 mimi sichoki kumushukuru Mungu kwa ajili yenu. Ninawakumbuka katika maombi yangu.

17 Ninamwomba Mungu wa Bwana wetu Yesu Kristo, Baba mwenye utukufu, awapatie Roho wake kusudi mukuwe na hekima na ufunuo hata muweze kumujua.

18 Ninaomba Mungu aifungue mioyo yenu ipate kuona mwangaza wake. Kwa hiyo mutapata kujua tumaini munalokuwa nalo kutokana na mwito wa Mungu. Vilevile mupate kujua utajiri mukubwa wa urizi anaouwekea watu wake,

19 na kutambua jinsi uwezo wake unavyokuwa mukubwa sana kwa ajili yetu sisi waamini, akizitumia nguvu zake kubwa sana.

20 Alifanya vile wakati alipomufufua Kristo na kumwikalisha na mamlaka kwa kuume kwake mbinguni.

21 Na kule anatawala juu ya wakubwa wote, wenye mamlaka wote, wenye uwezo wote na wasultani wote na juu ya kila cheo kinachoweza kuwa katika dunia hii na katika dunia itakayokuja.

22 Mungu amemupatia Kristo mamlaka juu ya vitu vyote na kumuweka kuwa kichwa cha kanisa.

23 Kanisa ni mwili wa Kristo, nalo ni utimilifu wa Kristo anayetimiza vitu vyote.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan