Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Waebrania 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Melkisedeki, Mufalme na Kuhani

1 Huyu Melkisedeki alikuwa mufalme wa Salemu na kuhani wa Mungu Mukubwa. Abrahamu alipokuwa akirudi toka katika vita nyuma ya kuwashinda wafalme wane, Melkisedeki alikutana naye na kumubariki,

2 naye Abrahamu akamupa fungu moja la kumi la vitu vyote alivyoteka. Maana ya jina la Melkisedeki, kwanza ni “Mufalme wa haki,” tena ni mufalme wa Salemu, ni kusema “Mufalme wa amani.”

3 Hakuna mambo yaliyoandikwa juu ya baba ya Melkisedeki, wala mama yake, wala majina ya babu zake. Tena, habari za kuzaliwa kwake na za kufa kwake hazijulikani. Anafanana na Mwana wa Mungu kwa kuwa yeye ni kuhani kwa milele.

4 Basi muangalie namna mutu huyu alivyokuwa mukubwa, hata babu yetu mukubwa Abrahamu alimupa fungu moja la kumi la vitu vyote alivyoteka katika vita.

5 Wazao wa Lawi wanaopewa kazi ya ukuhani wanaamriwa na Sheria kukongoa fungu moja la kumi la mapato toka kwa wandugu zao Waisraeli, ijapokuwa wao vilevile ni wa uzao wa Abrahamu.

6 Lakini huyu Melkisedeki asiyekuwa wa uzao wa Lawi, alipokea fungu moja la kumi la vitu toka kwa Abrahamu. Na zaidi ya ile akamubariki Abrahamu, ambaye Mungu alikuwa amemutolea ahadi.

7 Lakini bila shaka, yule anayebarikiwa ni mudogo kuliko yule anayebariki.

8 Wale makuhani wanaopokea fungu la kumi ni watu wanaokufa; lakini Melkisedeki aliyepokea fungu la kumi anashuhudiwa kwamba anaishi.

9 Basi tunaweza kusema hivi: wakati Abrahamu alipotoa fungu la kumi la mali yake, Lawi vilevile alilitoa kupitia yeye.

10 Kwa maana ingawa Lawi alikuwa hajazaliwa bado, alikuwa yuko ndani ya damu ya babu yake Abrahamu, wakati Melkisedeki alipokutana naye.

11 Ukuhani ndio ulikuwa musingi wa Sheria iliyotolewa kwa Waisraeli. Basi ikiwa ukamilifu ulipatikana kwa njia ya kazi ya ukuhani wa uzao wa Lawi, hakungekuwa tena lazima kutokee kuhani mwingine anayekuwa sawa na Melkisedeki, kwa pahali pa kuhani anayekuwa sawa na Haruni.

12 Kwa maana wakati ukuhani unapobadilika, Sheria nayo inapaswa kubadilika vilevile.

13 Naye Bwana wetu ambaye maneno haya yanamwelekea, alikuwa mutu wa kabila lingine, wala hakuna hata mutu mumoja wa kabila lake aliyefanya kazi ya ukuhani kwenye mazabahu.

14 Kwa maana inajulikana wazi kwamba Bwana wetu alitoka katika kabila la Yuda, na juu ya kabila lile Musa hakusema hata neno moja linaloelekea ukuhani.


Kuhani mwingine anayefanana na Melkisedeki

15 Tena jambo hili linaloonyesha wazi zaidi maneno haya: kumetokea kuhani mwingine anayefanana na Melkisedeki.

16 Huyu mwingine hakuwekwa kuwa kuhani kwa amri ya kimutu kufuatana na ukoo wake, lakini kufuatana na uwezo wa uzima usiokuwa na mwisho.

17 Maana Maandiko Matakatifu yanashuhudia: “Wewe ni kuhani kwa milele kwa mufano wa Melkisedeki.”

18 Kwa hiyo, ile amri ya zamani imevunjwa, kwa sababu ilikuwa zaifu nayo haikufaa kitu,

19 kwa maana Sheria ya Musa haikuleta ukamilifu. Lakini sasa kumeletwa tumaini nzuri zaidi, na kwa njia ya tumaini hili tunaweza kumukaribia Mungu.

20 Zaidi ya hii, mambo yale yalifanyika kufuatana na kiapo cha Mungu. Wale makuhani wengine wa uzao wa Lawi waliwekwa kwa kazi yao pasipo kiapo.

21 Lakini Yesu amewekwa kuwa kuhani kwa njia ya kiapo, wakati Mungu alipomwambia: “Bwana ameapa, naye hatageuka: ‘Wewe ni kuhani kwa milele.’ ”

22 Kwa sababu ya kiapo hiki, Yesu amekuwa kihakikisho kwetu cha agano linalokuwa zuri zaidi.

23 Kuna tofauti ingine vilevile: wale makuhani wengine walipaswa kuwa wengi, kwa sababu walikuwa wakikufa hawakuweza kuendelea na kudumu katika kazi yao.

24 Lakini Yesu hawezi kukombolewa kwa kazi yake ya ukuhani, kwa sababu yeye anaishi kwa milele.

25 Ni kwa sababu hii anaweza kuwaokoa kabisa wao wanaokuja kwa Mungu kwa njia yake, kwa maana yeye anaishi siku zote kusudi akuwe mwombezi mbele ya Mungu.

26 Basi Yesu ndiye Kuhani Mukubwa anayefaa kwa ajili yetu. Yeye ni mutakatifu, hana kosa wala alama ya uchafu. Ametengwa mbali na wenye zambi, naye amenyanyuliwa juu sana mbinguni.

27 Yeye hahitaji kutoa sadaka kila siku kama vile Makuhani wengine Wakubwa, kwanza kwa ajili ya zambi zake mwenyewe na kisha kwa ajili ya zambi za watu. Kwa maana amefanya vile mara moja tu wakati alipojitoa mwenyewe kufa.

28 Sheria ya Musa inawaweka watu wenye uzaifu kuwa Makuhani Wakubwa, lakini kufuatana na kiapo kilichokuja nyuma ya Sheria ile, Mwana anayekuwa mukamilifu kwa milele aliwekwa kuwa Kuhani Mukubwa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan