Waebrania 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Kila Kuhani Mukubwa aliyechaguliwa kati ya watu amesimikwa kwa kumutumikia Mungu kwa ajili ya watu kusudi atolee matoleo na sadaka kwa ajili ya zambi. 2 Kwa kuwa yeye mwenyewe ni muzaifu, anaweza kuwavumilia wale waliopotoka bila kujua. 3 Na kwa sababu yeye mwenyewe ni muzaifu, anapaswa kutolea sadaka, si kwa sababu ya zambi za watu tu, lakini kwa sababu ya zambi zake mwenyewe vilevile. 4 Hakuna mutu anayejipatia heshima hii ya kuwa Kuhani Mukubwa yeye mwenyewe. Lakini anapaswa kuitwa na Mungu, kama vile Haruni alivyoitwa. 5 Hivi vilevile, Kristo hakujipatia yeye mwenyewe utukufu wa kuwa Kuhani Mukubwa, lakini ni Mungu ndiye aliyemwambia: “Wewe ni mwana wangu, mimi leo nimekuwa baba yako.” 6 Vilevile alisema pahali pengine katika Maandiko: “Wewe ni kuhani hata milele kwa mufano wa Melkisedeki.” 7 Wakati Yesu alipoishi katika dunia, aliomba na kusihi kwa malalamiko makubwa pamoja na kutoa machozi kwa Mungu ambaye angeweza kumwokoa toka katika kifo. Mungu alimusikia Yesu kwa sababu yeye alimuheshimu. 8 Ijapokuwa alikuwa Mwana wa Mungu, alijifunza kutii kwa njia ya mateso yale aliyopata. 9 Na alipokwisha kufanywa kuwa mukamilifu, akawaongoza watu wote wanaomutii wapate kuokolewa kwa milele. 10 Basi, Mungu alitangaza kwamba yeye ni Kuhani Mukubwa kwa mufano wa Melkisedeki. Hatari ya kuacha imani 11 Tuna maneno mengi ya kusema juu ya jambo hili, lakini ni vigumu kuyaeleza kwenu kwa sababu ninyi mumekuwa na masikio magumu. 12 Kweli, kwa wakati huu, ninyi mungepaswa sasa kuwa walimu, lakini mungali munahitaji kufundishwa tena mafundisho ya mwanzo ya neno la Mungu. Mumegeuka tena wenye kuhitaji kunywa maziwa, wala si chakula kigumu. 13 Kwa maana kila mutu anayeishi kwa kunyonya maziwa tu hawezi kufahamu mafundisho ya haki, maana yeye ni mutoto muchanga. 14 Lakini chakula kigumu ni kwa ajili ya watu wazima, ndio wale waliozoeza mafikiri yao hata wapate kutambua mema na mabaya. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo