Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Waebrania 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Basi kwa kuwa tungali na ahadi ya kuingia kwenye mapumziko yale, basi tufanye angalisho kusudi katikati yenu kusikuwe hata mutu mumoja atakayekosa kuingia.

2 Kwa maana sisi vilevile tumehubiriwa Habari Njema kama vile watu wale. Walisikia habari lakini haikuwafalia kitu, kwa maana wale walioisikia hawakuipokea kwa imani.

3 Lakini sasa sisi tulioamini, tutaingia kwenye mapumziko ambayo Mungu alitaja aliposema: “Halafu nikaapa kwa kasirani kwamba hawataingia hata kidogo kwenye mapumziko niliyowatayarishia!” Mungu alisema vile ingawa alikuwa amemaliza kazi zake tangu pale alipoumba dunia.

4 Kwa maana imesemwa pahali fulani katika Maandiko Matakatifu juu ya siku ya saba: “Siku ya saba, Mungu akapumzika kwa maana alikuwa amemaliza kazi zake zote.”

5 Na tena, katika Maandiko tuliyotaja hapa juu, Mungu anasema: “Hawataingia hata kidogo kwenye mapumziko niliyowatayarishia.”

6 Wale waliokuwa wa kwanza kuhubiriwa Habari Njema hawakuingia kwenye mapumziko yale kwa sababu ya kutokuamini kwao. Ingawa vile ingali inawezekana kwa wengine kuingia.

7 Kwa sababu hii Mungu anaweka tena siku ingine inayoitwa “Leo”. Naye alisema juu ya siku ile nyuma ya miaka mingi kwa njia ya Daudi, kufuatana na Maandiko haya yaliyokwisha kutajwa mbele: “Leo kama munasikiliza sauti ya Mungu musifanye mioyo yenu kuwa migumu.”

8 Kwa maana kama Yoshua angekuwa amewafikisha watu kwenye mapumziko, Mungu hangesema tena nyuma ya pale juu ya siku ingine.

9 Kwa hiyo kungali mapumziko ambayo Mungu anawatayarishia watu wake.

10 Kwa maana yule anayeingia kwenye mapumziko anayotayarisha, anapumzika kwa kuwa amemaliza kazi zake zote kama vile Mungu alivyopumzika alipomaliza kazi zake.

11 Basi tufanye bidii ya kuingia kwenye mapumziko yale, kusudi hata mutu mumoja asianguke sawa vile wale walioasi katika jangwa.

12 Kwa maana Neno la Mungu ni lenye uzima, na lina nguvu; ni kali kupita upanga unaokata ngambo mbili. Linapenya hata linatenga moyo na roho na hata viungo na ubongo. Nalo linatambua nia na mawazo ya mutu.

13 Hakuna kitu kinachoweza kufichwa mbele ya Mungu, lakini vitu vyote vinafunuliwa na viko wazi mbele ya macho yake, yeye tutakayemutolea hesabu ya maneno yetu.


Yesu ni Kuhani Mukubwa zaidi

14 Basi, kwa kuwa tuko na Kuhani Mukubwa zaidi aliyeingia mbinguni, ndiye Yesu Mwana wa Mungu, tushikamane sana na imani tunayotangaza.

15 Kwa maana tuko na Kuhani Mukubwa asiyekosa kujua mwenyewe uzaifu wetu. Maana yeye alijaribiwa katika njia zote sawasawa na sisi, lakini hakufanya zambi.

16 Kwa sababu hii, tujongelee kwa uhodari kiti cha kifalme cha Mungu pahali anapowajalia watu neema kusudi apate kutuhurumia na kutujalia neema ya kutusaidia kwa wakati unaofaa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan