Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Waebrania 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Wokovu mukubwa

1 Kwa sababu hiyo, tunapaswa kushikamana zaidi na habari tuliyosikia, kusudi tusipotee mbali.

2 Ujumbe wa Sheria uliotangazwa na malaika ulitimizwa, na hata kila mutu aliyekosa kuufuata na kuasi aliazibiwa sawa inavyostahili.

3 Basi, namna gani sisi tutaponyoka azabu kama hatushuguliki na wokovu mukubwa kama huu? Ni Bwana mwenyewe aliyetangaza kwanza habari za wokovu huu, na wale waliomusikia walihakikisha kwetu kwamba ni za kweli.

4 Mungu vilevile alihakikisha ushuhuda wao kwa njia ya maajabu, ya miujiza mbalimbali, na ya vitambulisho, na kwa njia ya zawadi za Roho Mutakatifu alizowapa watu kama anavyopenda.


Mwongozi wa wokovu

5 Mungu hakuwapa wamalaika uwezo wa kutawala ulimwengu unaokuja, ndio ule tunaosema juu yake.

6 Tena maneno haya yanahakikishwa na pahali pengine katika Maandiko Matakatifu: “Mutu ni nini hata umukumbuke, mwanadamu ni nini hata umushugulikie?

7 Umemufanya kuwa mwenye cheo chini kidogo ya malaika. Umemujaza utukufu na heshima.

8 Umemupa mamlaka juu ya vitu vyote.” Wakati inaposemwa ya kama Mungu amemupa mutu mamlaka juu ya vitu vyote, maana yake hakuacha hata kitu kimoja. Ingawa hivi, hata sasa hatuoni kwamba amepewa mamlaka juu ya vitu vyote.

9 Lakini mambo tunayoona ndiyo haya: Yesu alifanywa kuwa mwenye cheo chini kidogo ya malaika kusudi kwa neema ya Mungu, Yesu akufe kwa ajili ya watu wote. Na sasa kwa njia ya kile kifo kilichomufikia, amepata utukufu na heshima.

10 Kwa hiyo ilifaa kwamba Mungu aliyeumba vitu vyote na kuvilinda imara, amufanye Yesu kuwa mukamilifu kwa njia ya mateso, kusudi awalete watoto wengi kuwa washiriki wa utukufu wa Mungu. Kwa maana Yesu ndiye anayewaongoza watu wapate kuokoka.

11 Yeye anawatakasa watu toka katika zambi, na wale wanaotakaswa naye, wote ni watoto wa Baba mumoja. Ni kwa sababu hiyo Yesu hasikii haya ya kuwaita wandugu zake.

12 Kwa maana anasema: “Ee Mungu, nitatangaza jina lako kwa wandugu zangu, nitakusifu katikati ya mukutano.”

13 Tena anasema: “Nitamutumainia Mungu.” Na tena anasema: “Mimi ni hapa pamoja na watoto Mungu alionipatia.”

14 Basi kwa kuwa hao watoto ni wanadamu, wenye mwili na damu, Yesu vilevile alitwaa ile hali ya mwanadamu. Alifanya hivi kusudi kwa njia ya kufa kwake amwangamize Shetani aliyekuwa na uwezo wa kuleta lufu.

15 Vilevile aliwafungua wale wote walioishi kama watumwa katika maisha yao yote kwa sababu ya kuogopa lufu.

16 Kwa maana hakika hakukuja kuwasaidia wamalaika, lakini alikuja kuwasaidia wazao wa Abrahamu.

17 Kwa hiyo ilimupasa afanane na wandugu zake katika mambo yote, kusudi apate kuwa Kuhani Mukubwa anayekuwa mwenye huruma na mwaminifu katika kazi yake mbele ya Mungu, na kwa njia hiyo zambi za watu zisamehewe.

18 Na kwa sababu yeye mwenyewe alijaribiwa na kuteswa, anaweza kuwasaidia wale wanaojaribiwa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan