Waebrania 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maagizo mbalimbali 1 Muendelee kuishi katika upendo wa kindugu. 2 Musisahau kuwakaribisha wageni, maana kwa kufanya hivi wamoja wamewakaribisha wamalaika pasipo kujua. 3 Muwakumbuke wale wanaofungwa, mukijisikia sawa vile wenye kufungwa pamoja nao. Vilevile muwakumbuke wale wanaoteswa, mukijisikia sawa vile wenye kuteswa kama wao. 4 Ndoa inapaswa kuheshimiwa na watu wote, mume na muke wake wanapaswa kujikinga na uchafu, kwa sababu Mungu atawahukumu wazinzi na waasherati. 5 Musijiachilie kutawaliwa na tamaa ya mali katika maisha yenu, lakini mutoshelewe na vitu munavyokuwa navyo, kwa maana Mungu mwenyewe amesema: “Sitakusahau wala kukuachilia.” 6 Kwa sababu hii tunaweza kusema kwa uhodari: “Bwana ndiye musaidizi wangu; sitaogopa kitu. Mwanadamu ataweza kunifanya nini?” 7 Muwakumbuke waongozi wenu waliowatangazia neno la Mungu. Muangalie vizuri namna walivyoishi na kufa. Mufuate imani yao. 8 Yesu Kristo ni yule yule, jana, leo na hata milele. 9 Musidanganywe na mafundisho mengine ya kigeni ya kila namna. Kwa maana mioyo yetu inapaswa kutiwa nguvu kwa njia ya neema ya Mungu, wala si kwa njia ya kushika kanuni zinazoagizwa juu ya vyakula. Kanuni hizo haziwafalii kitu wale wanaozishika. 10 Sisi tuko na mazabahu yetu, nao makuhani Wayuda wanaotumika katika Pahali Patakatifu hawana ruhusa ya kula sehemu ya vitu vinavyotolewa sadaka juu ya mazabahu ile. 11 Kuhani Mukubwa anapeleka damu ya nyama ndani ya Pahali Patakatifu Sana kwa ajili ya kuitoa kuwa sadaka ya kusamehewa zambi lakini viungo vyote vya nyama wale vinateketezwa kwa moto mbali na kambi. 12 Kwa sababu hii Yesu vilevile aliuawa mbali na muji kusudi awatakase watu wake kwa njia ya damu yake mwenyewe. 13 Basi tumwendee mbali na kambi, tukikubali kuzarauliwa kama vile yeye alivyozarauliwa. 14 Kwa maana hapa katika dunia hatuna muji unaodumu, lakini tunatazamia muji ule unaokuja. 15 Basi kwa njia ya Yesu, tumutolee Mungu sadaka za kumusifu siku zote, maana yake kutangaza kwamba tunaaminia jina lake. 16 Tena, musisahau kutenda mema na kusaidiana, maana sadaka za namna hii zinamupendeza Mungu. 17 Mutii waongozi wenu na kushika maagizo yao. Kwa maana wao wanashugulika kila mara kwa ajili ya roho zenu, na wao wanapaswa kutoa habari ya kazi yao mbele ya Mungu. Kwa kufanya vile mutawaruhusu kufanya kazi yao kwa furaha wala si kwa huzuni, kwa maana haitawafalia kitu kama wakitumika katika huzuni. 18 Muzidi kutuombea. Tuna uhakika kwamba tuko na zamiri safi, kwa maana tunataka kuwa na mwenendo mwema katika mambo yote. 19 Ninawasihi sana kuomba Mungu, kusudi nipate kurudishwa kwenu upesi. Maombi 20 Mungu wa amani, aliyemufufua Bwana wetu Yesu ambaye ni Muchungaji mukubwa wa kondoo kwa njia ya kumwanga damu yake inayohakikisha agano la milele, 21 awakamilishe katika kila tendo jema kusudi mupate kutimiza mapenzi yake; yeye atimize ndani yetu yale yanayomupendeza, kwa njia ya Yesu Kristo. Yesu atukuzwe milele na milele. Amina. Maneno ya mwisho na salamu 22 Wandugu, ninawasihi kupokea kwa uvumilivu haya maonyo ninayowatolea kwa maana nimewaandikia kwa kifupi. 23 Ninapenda kuwajulisha kwamba ndugu yetu Timoteo amekwisha kufunguliwa. Kama akikuja upesi, nitafika kuwaona pamoja naye. 24 Muwasalimie waongozi wenu wote na watu wote wa Mungu. Wandugu wa Italia wanawasalimia. 25 Tunawatakia ninyi wote neema ya Mungu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo