Waebrania 10 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Sheria ya Kiyuda ni mufano wa mema yatakayotokea, lakini si kitambulisho kinachoonyesha mambo yale kamili. Kwa sababu hii Sheria haiwezi hata mara moja, kwa njia ya sadaka zinazotolewa mara nyingi kila mwaka, kuwafanya wakamilifu wale wanaomwendea Mungu. 2 Wale wanaomwabudu Mungu kwa njia ile wangetakaswa kabisa kwa mara moja tu, nayo zamiri yao isingewahukumu tena hata kidogo juu ya zambi, basi sadaka zile hazingeacha kutolewa. 3 Lakini kwa njia ya sadaka zile, watu wanakumbushwa zambi zao kila mwaka, 4 kwa sababu damu ya ngombe na ya mbuzi haiwezi kuondoa zambi. 5 Kwa sababu hii, wakati Kristo alipokuja katika dunia alisema: “Wewe haukutaka sadaka wala matoleo. Lakini umeniumbia mwili. 6 Haukupendezwa na sadaka za kuteketezwa kwa moto wala sadaka za kusamehewa zambi. 7 Halafu nikasema: ‘Niko hapa, ee Mungu, nimekuja kufanya mapenzi yako, kama ilivyoandikwa juu yangu katika kitabu cha Sheria.’ ” 8 Kwanza Kristo alisema: “Haukutaka wala haukupendezwa na sadaka na matoleo, wala sadaka za kuteketezwa kwa moto wala sadaka za kusamehewa zambi.” (Alisema vile ingawa sadaka hizo zote zilitolewa kufuatana na maagizo ya Sheria.) 9 Kisha akasema: “Mimi niko hapa, ee Mungu, nimekuja kufanya mapenzi yako.” Kwa hiyo Mungu ameondoa hizo sadaka zote za kwanza na kuzikomboa na Kristo mwenyewe kama sadaka. 10 Na kwa sababu Yesu Kristo alifanya mapenzi ya Mungu, sisi tumetakaswa zambi kwa njia ya mwili wake alioutoa sadaka kwa mara moja tu. 11 Kila kuhani anasimama mbele ya Mungu kila siku kwa kufanya ibada na kutoa sadaka za namna moja mara nyingi zisizoweza hata kidogo kuondoa zambi. 12 Lakini Kristo yeye alitoa sadaka moja tu inayofaa kwa milele kwa ajili ya usamehe wa zambi. Na kisha akaikaa na mamlaka kwa kuume kwa Mungu. 13 Na kule anangoja sasa mpaka waadui zake wote watiwe chini ya miguu yake. 14 Kwa maana kwa njia ya sadaka moja aliyotoa, amewafanya wale aliowatakasa kuwa wakamilifu hata milele. 15 Naye Roho Mutakatifu anatushuhudia mambo hayo vilevile. Kwanza anasema maneno haya: 16 “Hili ndilo agano nitakalofanya nao nyuma ya siku zile. Ni Bwana wetu Mungu anayesema hivyo. Nitawawezesha kuchunga sheria zangu ndani ya mafikiri, nikiziandika ndani ya mioyo yao.” 17 Naye anaongeza kusema: “Nami sitakumbuka tena zambi wala maovu yao.” 18 Basi wakati zambi zinaposamehewa, hakuna tena hitaji la kutoa sadaka kwa ajili ya usamehe wa zambi. Tumukaribie Mungu 19 Basi wandugu, tuko na uhodari wa kuingia katika Pahali Patakatifu kwa njia ya damu ya Yesu. 20 Yeye ametufungulia njia mupya ya uzima, inayopitia katika pazia, maana yake mwili wake mwenyewe. 21 Sisi tuko na Kuhani Mukubwa anayesimamia nyumba yote ya Mungu. 22 Basi tumwendee Mungu kwa moyo wa uaminifu, kwa imani kamilifu, kwa moyo uliosafishwa toka zamiri mbaya na mwili uliosafishwa na maji safi. 23 Tuendelee kuchunga lile tumaini tuliloshuhudia bila kuchoka, kwa maana Mungu aliyetupatia ahadi ni mwaminifu. 24 Tena tushugulikiane kusudi tupate kuvutana sisi kwa sisi kuwa na upendo na kufanya mema. 25 Tusiache kukusanyika pamoja, kama vile wamoja wanavyozoea kufanya. Lakini tuonyane, na zaidi sana kufuatana na vile munavyoona kwamba Siku ya Bwana inakaribia. 26 Kwa maana tukifanya zambi kwa makusudi tukisha kutambua waziwazi ukweli, hakuna tena sadaka ingine inayoweza kutolewa kwa ajili ya usamehe wa zambi zetu. 27 Lakini inayobaki tu ni kungojea kwa woga hukumu na moto mukali wa Mungu utakaowateketeza waasi. 28 Mutu yeyote aliyevunja Sheria ya Musa, aliuawa bila huruma kisha ushuhuda wa watu wawili au watatu. 29 Basi munazania itakuwa namna gani? Hataazibiwa vikali zaidi yule anayemuzarau Mwana wa Mungu na kuihesabu kuwa bure damu ya agano la Mungu iliyomutakasa na kumutukana Roho wa neema? 30 Kwa maana tunamujua yule aliyesema: “Ni kazi yangu kulipiza kisasi. Ni mimi nitakayelipiza.” Naye alisema tena: “Bwana atawahukumu watu wake.” 31 Kuanguka katika mikono ya Mungu Mwenye Uzima ni jambo la kuogopa sana! 32 Mukumbuke mambo yaliyowatokea katika siku zilizopita. Ninyi mulipokwisha kuangaziwa na Mungu, mulipita katika mateso mengi lakini mulivumilia. 33 Kwa ngambo moja mulitukanwa na kuteswa waziwazi mbele ya watu. Na kwa ngambo ingine mulishirikiana na wale waliotendewa vibaya. 34 Muliwahurumia wale waliokuwa katika kifungo, nanyi mulikubali kwa furaha kunyanganywa mali zenu, kwa sababu mulijua kwamba muko na mali inayokuwa bora zaidi na yenye kudumu. 35 Basi musikate tumaini, kwa maana litawaletea zawadi kubwa. 36 Munapaswa kuvumilia, kusudi mutimize mapenzi ya Mungu, na kuweza hivi kupewa kile mulichoahidiwa. 37 Kwa maana, kama vile Maandiko haya Matakatifu yanavyosema: “Kunabaki wakati kidogo sana, yule anayepaswa kuja, afike wala hatakawia. 38 Mwenye haki mbele yangu ataishi kwa njia ya imani. Lakini kama akirudi nyuma, sitapendezwa naye.” 39 Lakini sisi si watu wenye kurudi nyuma na kupotea, lakini sisi ni watu wenye imani na wenye kuokoka. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo