Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Waamuzi 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Abimeleki

1 Abimeleki mwana wa Gideoni, akawaendea wandugu na wana wote wa kabila za mama yake kule Sekemu, akawaambia:

2 “Museme hapa hapa mbele ya wanainchi wote wa Sekemu: Jambo gani ni jema kwenu, kwamba watoto wote makumi saba wa kiume wa Yerubali wawatawale au mutoto mumoja? Mukumbuke kwamba mimi ni damu yenu.”

3 Wandugu za mama yake wakatangaza maneno popote kule Sekemu kwa jina lake, na watu wote wa Sekemu wakaamua kumufuata maana alikuwa ndugu yao.

4 Wakamupa vikoroti makumi saba vya feza vilivyokuwa kwenye nyumba ya Bali-Beriti ambavyo alivitumia kwa kulipa watu wakorofi na watu ovyoovyo kusudi wamufuate.

5 Akafuatana nao kwenda Ofura kwa baba yake naye akawaua wandugu zake wote makumi saba juu ya jiwe moja. Lakini Yotamu, mwana mudogo wa Yerubali aliponyoka kufa, maana alijificha.

6 Wanainchi wote wa Sekemu na Beti-Milo wakakusanyika kwenye muti wa mwalo unaokuwa karibu na munara kule Sekemu, wakamufanya Abimeleki kuwa mufalme wao.

7 Yotamu alipopata habari hiyo, alikwenda kusimama juu ya mulima Gerizimu, akasema kwa sauti kubwa: “Munisikilize, enyi watu wa Sekemu kama munataka Mungu awasikilize.

8 Siku moja, miti ilikwenda kujitafutia mufalme. Basi, ikauambia muzeituni: ‘Utawale juu yetu!’

9 Lakini muzeituni ukajibu: ‘Munazani ninaweza kuacha shuguli yangu ya kuzalisha mafuta ambayo yanaheshimiwa sana na miungu na wanadamu niende kujisumbua kuitawala miti?’

10 Kisha miti ikauambia muti wa tini: ‘Ukuje wewe utawale juu yetu.’

11 Lakini muti wa tini ukajibu: ‘Munazani ninaweza kuacha shuguli yangu ya kuzalisha matunda mazuri na matamu, niende kujisumbua kuitawala miti?’

12 Halafu miti ikauambia muzabibu: ‘Ukuje wewe ukuwe mutawala juu yetu.’

13 Lakini muzabibu ukajibu: ‘Munazani ninaweza kuacha shuguli yangu ya kuzalisha divai ambayo inafurahisha miungu na wanadamu, niende kujisumbua kuitawala miti?’

14 Kwa mwisho miti yote ikauendea muti wa miiba na kuuambia: ‘Ukuje wewe utawale juu yetu.’

15 Muti wa miiba ukajibu: ‘Kama kweli munataka kunichagua kuwa mufalme, mukuje mukae chini ya kivuli changu. Lakini kama hamutaki kufanya hivyo, basi moto utoke kwenye miiba yangu na kuiteketeza hata mierezi ya Lebanoni.’ ”

16 Yotamu akaendelea kusema: “Sasa basi, munazani mumefanya Abimeleki mufalme kwa nia njema na uaminifu? Munazani mumemutendea wema Yerubali na jamaa yake kama alivyostahili kwa matendo yake?

17 Kwa maana baba yangu alihatarisha maisha yake kwa kuwapigania na kuwakomboa kutoka kwa Wamidiani!

18 Lakini leo mumeishambulia jamaa ya baba yangu na kuwaua wana makumi saba juu ya jiwe moja, halafu mumemufanya Abimeleki mutoto wa mujakazi wa baba, akuwe mufalme wa wakaaji wa Sekemu kwa sababu tu ni mutu wa ukoo wenu.

19 Sasa basi, kama mumetenda hayo kwa nia njema na kwa kumuheshimu Yerubali na jamaa yake, basi, mufurahi pamoja na Abimeleki, naye afurahi pamoja nanyi.

20 Lakini, kama sivyo, moto utoke kwa Abimeleki na kuwateketeza wanainchi wa Sekemu na Beti-Milo, tena moto utoke kwa wanainchi wa Sekemu na Beti-Milo na kumuteketeza Abimeleki.”

21 Kisha Yotamu akatoroka, akakimbilia Beri, akakaa kule, kwa maana alimwogopa ndugu yake Abimeleki.

22 Abimeleki akatawala juu ya Israeli kwa muda wa miaka mitatu.

23 Kisha Mungu akaleta roho ya uadui kati ya Abimeleki na watu wa Sekemu, nao wakamwasi.

24 Ndivyo watu wa Sekemu pamoja na ndugu yao Abimeleki walivyoazibiwa kwa sababu waliwatendea kwa ukali wana makumi saba wa Yerubali. Azabu ya mauaji hayo iliwapata maana Abimeleki aliwaua akisaidiwa na hao watu wa Sekemu.

25 Watu wa Sekemu waliweka washambulizi wamuvizie Abimeleki kutoka vilele vya mulima. Watu hao waliwanyanganya mali zao wote waliopita kule. Abimeleki alipata habari hii.

26 Siku moja, Gali mwana wa Ebedi alikwenda pamoja na wandugu zake kukaa Sekemu. Watu wa Sekemu wakamuwekea tumaini.

27 Wakatoka na kwenda kwenye mashamba yao ya mizabibu, wakachuma zabibu halafu wakazikamua, wakatengeneza divai wakafanya sikukuu. Wakaingia kwenye nyumba ya mungu wao wakakula na kunywa, kisha wakamutukana Abimeleki.

28 Gali mwana wa Ebedi, akasema: “Abimeleki ni nani? Sisi hapa Sekemu ni watu wa aina gani hata tumutumikie Abimeleki? Gideoni na Zebuli jemadari wake walimutumikia Hamori baba wa Sekemu, lakini kwa nini basi, sisi tumutumikie Abimeleki?

29 Kama watu hawa wangekuwa chini yangu, ningemwondoa Abimeleki. Ningemwambia Abimeleki: ‘Ongeza jeshi lako, kisha, ukuje mbele ya watu wote tupigane.’ ”

30 Zebuli, mutawala wa muji, aliposikia maneno ya Gali mwana wa Ebedi, akakasirika sana.

31 Basi akamupelekea Abimeleki ujumbe kule Aruma akasema: “Gali, mwana wa Ebedi, pamoja na wandugu zake wameingia katika muji wa Sekemu na kuchochea uasi juu yako.

32 Basi, rudi wewe na watu unaokuwa nao, wakati wa usiku, uvizie katika mashamba karibu na muji.

33 Mara jua litakapotoka wakati wa asubui, ushambulie muji. Gali akitoka pamoja na watu wake kuja kupigana nawe, uwatendee sawa unavyoweza.”

34 Abimeleki akaondoka na watu waliokuwa pamoja naye kuja Sekemu wakati wa usiku. Aliwagawanya watu wake katika vikundi vine na kuvizia kule karibu na muji.

35 Gali mwana wa Ebedi akatoka inje na kusimama kwenye mulango wa muji. Wakati ule Abimeleki na watu wake walitoka pahali walipokuwa wanavizia.

36 Gali alipowaona, akamwambia Zebuli: “Angalia, watu wanashuka kutoka vilele vya mulima.” Zebuli akamwambia: “Wewe unaona vivuli vya milima sawa vile ni watu.”

37 Gali akasema tena: “Angalia! Watu wanashuka katikati ya inchi na kikundi kingine kinatoka upande wa muti wa Mwalo wa Waaguzi.”

38 Kisha Zebuli akamwambia: “Majivuno yako yako wapi sasa? Si ni wewe uliyesema: ‘Abimeleki ni nani? Kwa nini tumutumikie?’ Sasa, hao ndio watu uliowazarau. Kwenda upigane nao.”

39 Gali akatoka akiwaongoza watu wa Sekemu na kupigana na Abimeleki.

40 Kisha, Gali akakimbia mbele yake. Naye Abimeleki akamufuatilia. Watu wengi waliumizwa na kuanguka katika njia mpaka kwenye mulango wa muji.

41 Abimeleki akakaa Aruma na Zebuli akamufukuza Gali na wandugu zake kutoka katika muji wa Sekemu.

42 Siku iliyofuata, Abimeleki akapata habari kwamba watu wa Sekemu wametoka katika muji na kwenda katika mashamba.

43 Akatwaa watu wake akawagawanya katika vikundi vine, kusudi waende kuvizia katika mashamba. Alipowaona watu wanatoka katika muji, akatoka alikojificha akawaua.

44 Abimeleki na kundi lake wakaenda mbio kwenda kulinda mulango wa muji. Makundi yake mawili mengine yaliwashambulia wale waliokuwa katika mashamba na kuwaua.

45 Abimeleki akapigana na wakaaji wa muji ule siku nzima. Akauteka muji na kuwaua watu wote waliokuwa humo. Akauteketeza muji kwa moto na kuutia chumvi.

46 Watu wote waliokuwa katika munara wa Sekemu waliposikia habari hiyo, wakakimbilia kwenye chumba cha ndani cha nyumba ya mungu aliyeitwa Eli-Beriti.

47 Abimeleki alipata habari kwamba watu wote waliokuwa kwenye munara wa Sekemu wamejikusanya pamoja.

48 Abimeleki na watu wake wakaenda kwenye mulima Salmoni, akatwaa shoka, akakata tawi la muti na kuliweka juu ya bega lake. Halafu akawaambia wale watu aliokuwa nao waharakishe kufanya kama alivyofanya.

49 Kila mumoja akakata tawi kama lile la Abimeleki. Wakabeba matawi yao na kuyaegemeza kwenye kuta za chumba kile, wakayatia moto na kuchoma chumba. Watu wote wanaume na wanawake yapata elfu moja waliokuwa katika munara wa Sekemu wakakufa.

50 Kisha Abimeleki akaenda Tebesi, akazunguka muji ule na kuuteka.

51 Lakini kulikuwa munara imara katikati ya muji. Basi, wakaaji wote wa muji huo wanaume na wanawake wakakimbilia humo na kujifungia ndani. Wakapanda kwenye paa la munara huo.

52 Abimeleki akafika kwenye munara na kuushambulia. Kisha, akakaribia mulango wa munara autie moto.

53 Mwanamuke mumoja akatupa jiwe la kusagia, akamuponda Abimeleki kichwa.

54 Kisha Abimeleki akamwita haraka kijana wake aliyemubebea silaha akamwambia: “Twaa upanga wako uniue, watu wasipate kusema kwamba niliuawa na mwanamuke.” Kijana akatwaa upanga wake, akamuchoma na kumwua.

55 Waisraeli walipoona kwamba Abimeleki amekufa, wakaondoka na kurudi kila mumoja kwake.

56 Hivi ndivyo Mungu alivyomwazibu Abimeleki kwa kosa lake juu ya baba yake kwa kuwaua wandugu zake makumi saba.

57 Vilevile Mungu akawafanya watu wa Sekemu waazibiwe kwa uovu wao walioufanya. Hivyo, laana ya Yotamu mwana wa Yerubali ikawapata.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan