Waamuzi 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wimbo wa Debora 1 Siku hiyo, Debora na Baraka mwana wa Abinoamu, wakaimba wimbo huu: 2 Viongozi walijitokeza kuongoza Israeli, watu walijitolea kwa mapenzi yao. Mumushukuru Yawe! 3 Musikilize, enyi wafalme! Mutege sikio, enyi wakubwa! Nitamwimbia Yawe, Mungu wa Israeli. 4 Ee Yawe, ulipotoka kule Seiri, ulipoteremuka kwenye mulima Edomu, inchi ilitetemeka, mbingu zilidondosha maji, mawingu yakaiangusha mvua. 5 Milima ilitikisika mbele yako Yawe, mulima Sinai mbele yako Yawe, Mungu wa Israeli. 6 Katika siku za Samugari mwana wa Anati, katika wakati wa Yaeli, makundi ya watu yalikoma kupita katika inchi, wasafiri walipitia njia za pembenipembeni. 7 Walimaji walitoweka, walitoweka katika Israeli, mpaka nilipotokea mimi Debora, mimi ninayekuwa mama wa Israeli. 8 Walijichagulia miungu mipya, kukakuwa vita katika inchi. Lakini hakukupatikana mwenye upanga au ngao kati ya watu elfu makumi ine wa Israeli. 9 Ninawapa heshima viongozi wa Israeli waliojitoa kwa mapenzi yao kati ya watu. Mushukuru Yawe! 10 Enyi munaopanda juu ya punda weupe, enyi munaoikalia matandiko ya bei kali, enyi munaotembea katika njia, mutangaze jambo hilo! 11 Kwenye visima vya maji, tangaza ushindi wa Yawe, ushindi kwa walimaji wake katika Israeli. Watu wa Yawe walishuka kwenye mulango wa muji. 12 “Amuka, amuka, Debora! Amuka! Amuka uimbe wimbo! Amuka, Baraka mwana wa Abinoamu, uwakamate wafungwa wako. 13 Mashujaa waliobaki waliteremuka. Watu wa Yawe walikwenda kumupigania na wenye nguvu. 14 Kutoka Efuraimu waliteremuka katika bonde, wakafuata wandugu zao watu wa Benjamina; kutoka Makiri, majemadari walishuka, kutoka Zebuluni, wenye fimbo ya mutawala. 15 Wakubwa wa Isakari wakafuata Debora, watu wa Isakari, waaminifu kwa Baraka, wakamufuata mbio mpaka katika bonde. Lakini kati ya ukoo za Rubeni kulikuwa kusitasita kwingi. 16 Kwa nini walibaki katika mazizi? Kwa kusikiliza milio ya kondoo? Kati ya ukoo za Rubeni kulikuwa kusitasita kwingi. 17 Kabila la Gileadi lilibaki ngambo ya Yordani. Kabila la Dani, kwa nini mulibaki ndani ya mashua? Kabila la Aseri lilitulia kule pembeni ya bahari, lilikaa katika kivuko chake. 18 Watu wa Zebuluni ni watu waliohatarisha maisha yao katika kifo. Hata wa Nafutali walisogelea kifo kwenye miinuko ya mashamba. 19 “Kule Tanaki, pembeni ya chemichemi za Megido, wafalme walikuja, wakapigana; wafalme wa Kanana walipigana, lakini hawakuteka feza. 20 Nyota kutoka mbinguni zilishiriki vita, zilifuata njia zao zikapigana na Sisera. 21 Mafuriko ya muto Kisoni yaliwapeleka mbali, mafuriko makali ya muto Kisoni. Songa mbele kwa nguvu, ee nafsi yangu! 22 “Farasi walipita wakipiga udongo, walipigapiga udongo na kishindo cha kwato zao. 23 Malaika wa Yawe anasema hivi: ‘Ulaani muji wa Merosi, uwalaani vikali wakaaji wake; maana hawakukuja kumusaidia Yawe hawakumusaidia Yawe juu ya wenye nguvu’. 24 “Abarikiwe kuliko wanawake wote Yaeli, muke wa Heberi Mukeni. Amebarikiwa kuliko wanawake wote wanaokaa katika mahema. 25 Sisera alimwomba maji, naye akamupa maziwa; akamuletea siagi katika bakuli ya heshima. 26 Kwa mukono mumoja akashika musumari wa kufungia hema, na kwa mukono wake wa kuume nyundo ya fundi. Alimuponda Sisera kichwa, akavunja na kupasuapasua paji lake. 27 Sisera akainama, akaanguka; akalala kimya kwenye miguu yake. Hapo alipoinama ndipo alipoanguka amekufa! 28 “Mama ya Sisera akaangalia toka kwenye dirisha, akachungulia, kisha akalalamika: ‘Kwa nini gari lake limechelewa? Mbona vishindo vya magari yake vimechelewa kusikilika?’ 29 Jibu akalipata kwa wanawake wenye hekima: akajituliza tena na tena kwa jibu hilo: 30 ‘Bila shaka wanatafuta na kugawanyana vitu: binti mumoja au wawili kwa kila askari, nguo ya sufu ya rangi kwa ajili ya Sisera, nguo ya sufu iliyopindwa vizuri, na mikufu miwili yenye kufumwa kwa ajili ya shingo yangu!’ 31 “Ee Yawe, waangamie waadui zako wote! Lakini warafiki zako wakuwe kama jua, wakati linapochomoza kwa mwangaza mukubwa!” Inchi ya Waisraeli ikakuwa na amani kwa muda wa miaka makumi ine. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo