Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Waamuzi 21 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kuchipuka tena kwa kabila la Benjamina

1 Waisraeli walikuwa wameapa kule Misipa kwamba hakuna hata mumoja kati yao ambaye angemwachilia binti yake aolewe kwa watu wa kabila la Benjamina.

2 Basi, wakaenda mpaka Beteli wakakaa kule mbele ya Mungu mpaka magaribi. Wakalalamika kwa sauti na kulia kwa uchungu mwingi.

3 Wakasema: “Ee Yawe, Mungu wa Israeli, kwa nini jambo hili limetukia hata tupungukiwe na kabila katika Israeli?”

4 Kesho yake watu wakaamuka mapema, wakajenga mazabahu, wakatoa sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka za amani.

5 Kisha wakaulizana: “Kati ya makabila yote ya Israeli kuna kikundi chochote ambacho hakikuhuzuria mukutano uliofanyika mbele ya Yawe?” Walikuwa wamefanya kiapo kwamba mutu yeyote ambaye hatahuzuria mbele ya Yawe kule Misipa anapaswa kuuawa.

6 Lakini Waisraeli wakawaonea huruma wandugu zao wa kabila la Benjamina, wakasema: “Leo kabila moja la Israeli limeangamia.

7 Sasa tutafanya nini kwa kuwapatia wanawake hao wanaume wa kabila la Benjamina waliobaki kwa vile tulikwisha kuapa kwa jina la Yawe kwamba hatutawapa wabinti zetu wakuwe wake zao?”

8 Wakataka kujua kama kulikuwa kikundi chochote cha makabila ya Israeli ambacho hakikuhuzuria mukutano mbele ya Yawe kule Mispa. Wakagundua kwamba hakuna mutu yeyote kutoka Yabesi-Gileadi aliyekuja kwenye mukutano ule.

9 Waisraeli walipohesabiwa kule Misipa hakuna mukaaji yeyote wa Yabesi-Gileadi aliyehuzuria.

10 Kwa hiyo Waisraeli wakapeleka watu wake elfu kumi na mbili elfu wanaokuwa hodari kabisa na kuwaamuru: “Muende muwaue wakaaji wa Yabesi-Gileadi; wanawake pamoja na watoto.

11 Mutawaua wanaume wote na wanawake wote wasiokuwa mabikira.”

12 Basi wakakuta kati ya wakaaji wa Yabesi-Gileadi wabinti mia ine ambao hawakukuwa wamekwisha kulala na mwanaume yeyote, wakawapeleka katika kambi kule Shilo katika inchi ya Kanana.

13 Kisha wote pamoja wakawapelekea ujumbe wa amani watu wa kabila la Benjamina ambao walikuwa kwenye mulima wa Rimoni.

14 Wanaume hao wa kabila la Benjamina wakawarudilia hao wenzao wakati uleule. Basi wakapewa wale wanawake ambao walikuwa wameachwa kule Yabesi-Gileadi. Lakini wanawake hao hawakuwatosha.

15 Waisraeli wakawaonea huruma watu wa kabila la Benjamina, maana Yawe alisababisha kukuwe shimo kati ya Waisraeli.

16 Kisha wazee wa Israeli wakasema: “Sasa tutafanya nini kwa kuwapatia wake hao wanaume waliobaki kwa vile wanawake wote wa kabila la Benjamina waliangamia?

17 Inafaa wanaume waliobaki wa kabila la Benjamina wapewe wanawake kusudi waendeleshe kabila, na hivyo kusipotee kabila lolote katika Israeli.

18 Lakini hatuwezi kuwatoa wabinti zetu wakuwe wake zao, maana tulikwisha kuapa kwamba mutu yeyote atakayemwoesha binti yake kwa mwanaume wa kabila la Benjamina alaaniwe.”

19 Basi wakakumbuka kwamba sikukuu ya Yawe iliyofanyika kila mwaka kule Shilo, muji unaokuwa upande wa kaskazini wa Beteli, kwenye njia kubwa inayotoka Beteli kwenda Sekemu, ilikuwa inakaribia.

20 Kwa hiyo wakawaamuru wale wanaume wa kabila la Benjamina: “Muende muvizie na kufichama katika mashamba ya mizabibu.”

21 Mukuwe macho. Wabinti wa Shilo watakapotoka inje kwa kucheza wakati wa sikukuu, mutoke kwenye mizabibu na kila mutu ajikamatie binti mumoja akuwe muke wake. Kisha murudi katika inchi ya Benjamina.

22 Baba zao au kaka zao wakikuja kutulalamikia tutawaambia: “Sisi tunawaomba muwahurumie watu wa Benjamina na kuwaacha watwae hao wanawake; maana hatukupata wanawake wa kutosha katika vita ya Yabesi-Gileadi. Na kwa sababu si ninyi wenyewe muliowapatia hao wabinti zenu, hamutahukumiwa kwamba mumevunja kiapo.”

23 Wale wanaume wa kabila la Benjamina wakafanya hivyo, kila mumoja akajichagulia binti kati ya wabinti waliotoka inje kwa kucheza kule Shilo na kumutwaa kuwa muke wake. Kisha wakarudi katika eneo lao, wakaijenga miji yao upya na kuishi mule.

24 Wakati uleule Waisraeli wakaondoka, kila mutu akarudi katika eneo la kabila lake na jamaa yake. Kila mutu akarudi katika sehemu aliyogawanyiwa.

25 Siku hizo hakukukuwa mufalme katika Israeli. Kila mutu alifanya sawa vile alivyotaka.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan