Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Waamuzi 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Yawe anawagombeza watu wake

1 Malaika wa Yawe aliondoka Gilgali, akaenda Bokimu, akawaambia Waisraeli: “Niliwaondoa katika inchi ya Misri na kuwaleta katika inchi ambayo niliahidi kwa kiapo kwa babu zenu. Nilisema kwamba sitalivunja agano langu nanyi hata kidogo.

2 Na kwa upande wenu niliwaamuru musifanye agano na wenyeji wa inchi hii na kwamba mazabahu zao mutazibomoa. Lakini ninyi hamukuitii amri yangu. Kwa nini mambo haya?

3 Kwa hiyo sasa ninasema: Sitawafukuza tena wakaaji wa inchi hii lakini watawataabisha ninyi, na miungu yao itakuwa mutego kwenu.”

4 Malaika wa Yawe alipowaambia watu wote wa Israeli maneno haya, wakalalamika na kulia.

5 Wakapaita pahali pale Bokimu, ni kusema “Wanaolia”. Pale wakamutolea Yawe sadaka.


Kifo cha Yoshua

6 Yoshua aliwatuma Waisraeli wote waende kwenye maeneo yao waliyogawanyiwa kwa kurizi inchi.

7 Waisraeli walimutumikia Yawe siku zote za maisha ya Yoshua na nyuma ya kifo chake kwa muda wote wale wazee waliobaki waliishi ambao waliyaona matendo makubwa ambayo Yawe aliwatendea Waisraeli.

8 Yoshua mwana wa Nuni, na mutumishi wa Yawe, akakufa akiwa na umri wa miaka mia moja na kumi.

9 Wakamuzika katika sehemu aliyogawanyiwa ikuwe yake kule Timunati-Heresi, katika inchi ya milima ya Efuraimu upande wa kaskazini wa mulima Gasi.

10 Kisha watu wote wa kizazi chake wakakufa, kizazi kingine kikafuata ambacho hakikumujua Yawe wala matendo aliyowatendea watu wa Israeli.


Waisraeli wanamwasi Yawe

11 Basi, Waisraeli walitenda uovu mbele ya Yawe na kuabudu Mabali.

12 Walimwacha Yawe, Mungu wa wazee wao, ambaye aliwaondoa katika inchi ya Misri, wakaifuata miungu mingine, miungu iliyoabudiwa na watu walioishi kandokando yao. Waliinama mbele ya miungu hiyo, wakamukasirikisha sana Yawe.

13 Walimwacha Yawe, wakatumikia Mabali na Mastaroti.

14 Basi, hasira ya Yawe ikawaka juu ya Israeli, naye akawaacha wanyanganyi wanyanganye mali zao. Akawatoa kwa waadui zao waliowazunguka hata wasiweze tena kuwashinda.

15 Kila mara walipokwenda kupigana, mukono wa Yawe ulipambana nao kwa kuwaletea hasara, kama alivyokuwa amewaonya na kuapa. Nao wakakuwa katika huzuni kubwa.

16 Halafu Yawe akawapa waamuzi ambao waliwaokoa toka katika mikono ya watu walionyanganya mali zao.

17 Hata hivyo, Waisraeli hawakuwasikiliza waamuzi wao, maana walifanya kama wazinzi kwa kufuata miungu mingine na kuinama mbele yao. Wakaacha upesi njia ya babu zao. Babu zao walitii amri za Yawe lakini wao hawakuzitii.

18 Kila mara Yawe alipowapelekea mwamuzi, yeye mwenyewe alikuwa pamoja na mwamuzi yule, akawaokoa toka katika mikono ya waadui zao muda wote wa maisha ya mwamuzi yule. Ingawa hivyo, Yawe aliwaonea huruma aliposikia kilio chao kutokana na mateso na masumbuko yao.

19 Lakini kila mara mwamuzi alipokufa walirudilia mienendo yao ya zamani, wakaishi vibaya kuliko babu zao. Waliifuata miungu mingine, wakaitumikia na kuinama mbele yao, wala hawakuyaacha matendo yao wala uasi wao.

20 Kwa hiyo Yawe akawaka hasira juu ya Waisraeli, akasema: “Kwa sababu watu hawa wamevunja agano nililofanya na babu zao, wakakataa kutii sauti yangu,

21 sitayafukuza tena mataifa ambayo Yoshua aliyaacha, wakati alipokufa.

22 Nitayatumia mataifa hayo kuwajaribu Waisraeli nione kama watairudilia njia yangu kama babu zao au sivyo.”

23 Basi, Yawe akayaacha mataifa hayo ambayo hakumupa Yoshua ushindi juu yao, wala hakuyafukuza mara moja.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan