Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Waamuzi 18 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mika na kabila la Dani

1 Katika siku zile hakukukuwa mufalme katika Israeli. Basi kabila la Dani lilikuwa linatafuta eneo lake lenyewe la kuishi ndani yake, maana mpaka wakati ule, halikukuwa limegawanyiwa sehemu yake lenyewe kati ya makabila ya Israeli.

2 Kwa hiyo watu wa kabila la Dani wakachagua kati yao watu hodari, wakawatuma kutoka kule Estaoli na Zora, wakawaamuru waende kuipeleleza inchi. Basi watu hao wakafika katika inchi ya milima ya Efuraimu katika nyumba ya Mika, wakaenda na kukaa mule.

3 Walipokuwa kwa Mika, wakaitambua sauti ya yule kijana Mulawi. Wakamugeukia na kumwuliza: “Nani amekuleta huku? Una shuguli gani hapa?”

4 Yeye akawajibu: “Mika amefanya nami mupango. Amenipa kazi nami nimekuwa kuhani wake.”

5 Nao wakamwambia: “Tafazali utuulizie kwa Yawe kama tutafanikiwa katika safari yetu.”

6 Yule kuhani akawaambia: “Muende kwa amani. Yawe anaichunga safari yenu.”

7 Basi, watu hao watano wakaondoka, wakaenda Laisi. Waliwaona watu walioishi kule, na jinsi walivyokaa kwa usalama kama vile watu wa Sidona. Walikuwa watu watulivu wasiokuwa na wasiwasi na hawakupungukiwa mahitaji yoyote katika inchi. Walikuwa mbali na watu wa Sidona, na hawakukuwa na shuguli yoyote na watu wengine.

8 Basi hao wapelelezi wakarudi kwa wandugu zao huko Zora na Estaoli, nao wakawauliza: “Mumetuletea habari gani?”

9 Wao wakasema: “Musimame tuende na kuishambulia inchi hiyo. Tumeiona na kweli ni inchi yenye mboleo. Mutakaa hapa tu bila kufanya kitu? Musikawie kwenda kuirizi inchi hiyo.

10 Mutakapofika kule mutakuta watu wasiokuwa na wasiwasi wowote. Inchi hiyo ni kubwa, haikupungukiwa chochote, na Mungu ameitia katika mikono yetu.”

11 Basi, watu mia sita wa kabila la Dani wakiwa na silaha zao za vita wakaondoka kutoka Zora na Estaoli,

12 wakaenda kupiga kambi yao kule Kiriati-Yearimu katika inchi ya Yuda. Ndiyo maana pahali pale, upande wa magaribi wa Kiriati-Yearimu pameitwa Kambi ya Dani mpaka leo.

13 Kutoka kule wakaelekea inchi ya milima ya Efuraimu, wakafika katika nyumba ya Mika.

14 Watu wale watano waliokwenda kuipeleleza inchi ya Laisi wakawaambia wandugu zao: “Munajua kwamba katika nyumba moja kati ya hizi kuna kizibao, sanamu ya kuchongwa na sanamu yenye kuyeyushwa? Basi, mufikiri namna ya kufanya.”

15 Basi wale wapelelezi wakaelekea kwenye nyumba ya Mika, wakaingia ndani na kumwuliza habari za yule kijana Mulawi.

16 Wakati ule, wale watu mia sita wa kabila la Dani wakiwa na silaha zao za vita wakasimama kwenye mulango.

17 Wale watu watano waliokwenda kuipeleleza inchi wakaingia ndani, wakabeba ile sanamu ya mungu yenye kuyeyushwa, kile kizibao na sanamu ya ibada. Wakati ule yule kuhani alikuwa akisimama kwenye mulango pamoja na wale watu mia sita wenye silaha.

18 Basi, alipowaona wale wapelelezi wanaingia ndani ya nyumba ya Mika na kutwaa sanamu ya kuchonga, kifuko cha kuomba shauri, sanamu ya kuchongwa na sanamu ile yenye kuyeyushwa, akawauliza: “Munafanya nini?”

19 Nao wakamwambia: “Nyamaza, funga kinywa chako, ukuje pamoja nasi, ukuwe kuhani wetu na kama baba yetu. Au unaona namna gani? Inafaa kwako zaidi kuwa kuhani wa mutu mumoja au kuwa kuhani wa kabila moja la Israeli?”

20 Yule kuhani akafurahi sana akatwaa kile kifuko, ile sanamu ya ibada, na ile sanamu ya mungu yenye kuyeyushwa, akafuatana nao.

21 Basi, wakaanza safari yao, na walikuwa wanatanguliwa na watoto wao na nyama wao na mali zao.

22 Walipokuwa wamefika mbali na nyumba ya Mika, watu waliokuwa jirani na Mika wakaitwa, wakawafuatilia watu wa kabila la Dani, wakawafikia.

23 Kisha wakawapigia kelele, nao watu wa kabila la Dani wakageuka, wakamwuliza Mika: “Una shida gani hata umetufuatilia pamoja na kundi hili lote?”

24 Mika akasema: “Ninyi mumebeba miungu yangu niliyojitengenezea, mukamutwaa na kuhani wangu, mukaniacha bila kitu chochote. Munaweza namna gani basi kuniuliza nina shida gani?”

25 Watu wa kabila la Dani wakamwambia: “Afazali uache kelele zako, kama sivyo wengine wetu wenye hasira wanaweza kukushambulia, nawe utapoteza maisha yako na maisha ya jamaa yako.”

26 Mika alipoona kwamba wamemuzidia nguvu, akageuka, akarudi kwake; nao watu wa kabila la Dani wakaenda zao.

27 Hao watu wa kabila la Dani walivitwaa vitu vile ambavyo Mika alikuwa amevitengeneza, na kumupeleka yule kuhani aliyemutumikia. Basi wakaenda kushambulia muji wa Laisi, wakawaua wakaaji wake ambao waliishi mule kwa utulivu na bila wasiwasi, wakauteketeza muji ule.

28 Wakaaji wa muji ule hawakukuwa na mutu wa kuwaokoa kwa sababu walikuwa mbali na muji wa Sidona, tena hawakukuwa na ushirika na watu wengine. Muji ule ulikuwa kwenye bonde la Beti-Rehobu. Watu wa kabila la Dani wakaujenga upya, wakaishi mule.

29 Walibadilisha jina la muji ule, wakauita Dani, kufuata jina la babu yao aliyekuwa mwana wa Israeli. Lakini muji ule pale mbele uliitwa Laisi.

30 Watu wa kabila la Dani wakaisimika ile sanamu ya kuchonga, naye Yonatani mwana wa Gersoni, mujukuu wa Musa, akakuwa kuhani wao. Wazao wake vilevile walikuwa makuhani wa kabila la Dani mpaka wanainchi wa inchi hiyo walipopelekwa katika uhamisho.

31 Wakati wote nyumba ya Mungu ilipokuwa kule Shilo, watu wa kabila la Dani waliiabudu sanamu ya kuchonga ambayo Mika aliitengeneza.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan