Ufunuo 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Kisha mambo hayo, nikasikia kelele kutoka mbinguni linalosikilika kama vile sauti kubwa ya kundi kubwa la watu ikisema: “Mungu asifiwe! Wokovu, utukufu na uwezo ni vya Mungu wetu. Yeye anastahili utukufu na uwezo. 2 Hukumu zake ni za kweli na za haki. Amehukumu yule kahaba mukubwa ambaye alikuwa akipotosha dunia kwa vitendo vyake vya uasherati. Mungu amemulipiza kisasi cha damu ya watumishi wake!” 3 Nao wakasema tena: “Mungu asifiwe! Moshi wa moto unaoteketeza ule muji mukubwa unapanda juu kwa milele na milele!” 4 Na wale wazee makumi mbili na wane na vile viumbe vine vya ajabu wakainama chini na kumwabudu Mungu, anayeikaa juu ya kiti cha kifalme, wakisema: “Amina! Mungu asifiwe!” Karamu ya ndoa ya Mwana-Kondoo 5 Kisha sauti ikasikilika toka kwenye kiti cha kifalme ikasema: “Mumusifu Mungu wetu ninyi watumishi wake wote, ninyi wote munaomuheshimu, wakubwa na wadogo!” 6 Kisha nikasikia sauti inayosikilika kama kelele la kundi kubwa la watu, na kama ngurumo ya maporomoko ya maji mengi na kama ngurumo kubwa ya radi ikisema: “Mungu asifiwe! Kwa maana yeye Bwana wetu, Mungu wetu Mwenye Uwezo anatawala. 7 Tufurahi na kushangilia na kumutukuza, kwa sababu saa ya ndoa ya Mwana-Kondoo imetimia, naye bibi arusi wake amejitayarisha.” 8 Yule bibi amepewa nguo ya kuvaa iliyofumwa na nyuzi nzuri zenye kungaa. (Nguo ile ni mufano wa matendo ya haki ya watu wa Mungu.) 9 Halafu malaika akaniambia: “Andika maneno haya: Heri wale wanaoalikwa kwa karamu ya ndoa ya Mwana-Kondoo.” Naye akasema tena: “Maneno haya ni ya kweli yanayotoka kwa Mungu.” 10 Nikaanguka mbele yake kusudi nimwabudu, lakini akaniambia: “Angalia, usifanye vile! Kwa maana mimi ni mutumishi kama vile wewe na wandugu zako wanaoshika ukweli ulioshuhudiwa na Yesu. Ni Mungu ndiye unayepaswa kumwabudu! Maana ukweli ambao Yesu alishuhudia, ndio uwezo unaowaongoza manabii.” Mwenye kupanda juu ya farasi mweupe 11 Kisha nikaona mbingu imefunguka na kukatokea farasi mweupe. Yule aliyepanda juu yake anaitwa Mwaminifu na Mwenye Ukweli, kwa maana anahukumu na kupigana vita kwa haki. 12 Macho yake yalimetameta kama ndimi za moto, na juu ya kichwa chake kulikuwa taji nyingi. Alikuwa na jina lililoandikwa juu yake, wala hakuna mutu aliyejua, isipokuwa yeye mwenyewe tu. 13 Alikuwa amevaa nguo iliyochovywa ndani ya damu. Jina lake ni: “Neno la Mungu.” 14 Makundi ya wakaaji wa mbinguni wakamufuata, nao walikuwa wakipanda juu ya farasi weupe na kuvaa nguo safi nyeupe za kitani. 15 Ndani ya kinywa chake mulitoka upanga mukali kwa kushinda mataifa. Naye atatawala kwa fimbo ya chuma na kukamua zabibu ndani ya kikamulio cha divai kinachojaa kasirani kali ya Mungu Mwenye Uwezo. 16 Na juu ya nguo yake na paja la muguu wake kulikuwa kumeandikwa jina hili: “Mufalme wa wafalme na Bwana wa wabwana.” 17 Kisha nikaona malaika mumoja amesimama katika jua. Alikuwa akilalamikia ndege wote waliokuwa wakiruka juu katika anga akiwaambia: “Mukuje mukutane pamoja kwa karamu kubwa ya Mungu! 18 Hivi mutakula nyama za miili ya wafalme, za majemadari, za watu wenye uwezo, nyama za farasi pamoja na za watu wanaopanda juu yao na nyama za watu wote wanaokuwa huru na za watumwa, wakubwa kama vile wadogo.” 19 Nikaona yule nyama wa ajabu pamoja na wafalme wa dunia na makundi yao ya waaskari wamekusanyika pamoja kupigana vita na yule anayepanda juu ya farasi na kundi la waaskari wake. 20 Yule nyama akakamatwa pamoja na yule nabii wa uongo aliyeonyesha vitambulisho mbele yake. (Ni kwa njia ya vitambulisho vile aliwadanganya wale waliopigwa chapa ya yule nyama na wale walioabudu sanamu yake.) Nyama yule pamoja na nabii wa uongo wakatupwa wangali wazima katika ziwa la moto munamowaka mawe ya kiberiti. 21 Na wale waliobaki wakauawa kwa upanga uliotoka katika kinywa cha yule aliyepanda juu ya yule farasi. Ndege wote wakashibishwa na kula nyama za miili yao. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo