Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Ufunuo 14 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Wimbo wa watu waliokombolewa

1 Kisha nikaangalia, nikaona Mwana-Kondoo akisimama juu ya mulima Sayuni. Naye alikuwa pamoja na watu elfu mia moja makumi ine na ine, na juu ya paji za nyuso za watu wale kulikuwa kumeandikwa jina lake na jina la Baba yake.

2 Nikasikia sauti kutoka mbinguni ikinguruma kama uvumi wa maporomoko ya maji mengi na kama ngurumo kubwa ya radi. Sauti ile ilisikilika kama vile sauti ya wapiga vinubi wakati wanapopiga vinubi vyao.

3 Wale watu elfu mia moja makumi ine na ine waliimba wimbo mupya mbele ya kile kiti cha kifalme na mbele ya vile viumbe vine vya ajabu na ya wale wazee. Hakuna mutu aliyeweza kujifunza wimbo ule, isipokuwa wale watu elfu mia moja makumi ine na ine waliokombolewa katika dunia.

4 Watu wale ndio waliojilinda katika usafi bila kujichafua kwa kulala na wanawake, nao wanamufuata Mwana-Kondoo kila fasi anapokwenda. Wamekombolewa kati ya watu wengine kusudi wakuwe wa kwanza kutolewa kwa Mungu na kwa Mwana-Kondoo kama vile sadaka ya mavuno ya kwanza.

5 Wao hawakusema uongo hata mara moja; wako bila kosa.


Wamalaika watatu

6 Kisha nikaona malaika mwingine akiruka juu sana katika mbingu akiwa na Habari Njema ya milele ya kupasha kwa wakaaji wa dunia, kwa watu wa kila taifa, wa kila kabila, wa kila luga na kila jamaa.

7 Halafu akasema kwa sauti kubwa: “Mumuheshimu Mungu na kumutukuza, kwa sababu saa yake ya kuwahukumu watu imetimia. Mumwabudu yule aliyeumba mbingu na dunia, bahari na chemichemi za maji.”

8 Malaika wa pili akafuata yule wa kwanza akisema: “Umebomoka, umebomoka kabisa, ule muji mukubwa Babeli. Umewakunywesha mataifa yote divai yake kali, ukiwalewesha na maovu ya uasherati wake.”

9 Na malaika wa tatu akafuata wale wawili wa kwanza, akisema kwa sauti kubwa: “Kila mutu anayeabudu yule nyama na sanamu yake na kupigwa chapa juu ya paji la uso wake au juu ya mukono wake,

10 naye vilevile atakunywa divai kali ya hasira ya Mungu iliyotengenezwa pasipo kuchangwa na maji na kumimiwa ndani ya kikombe chenye kujaa kasirani yake! Na watu kama wale, watateswa ndani ya moto na ndani ya mawe ya kiberiti yanayowaka moto mbele ya wamalaika watakatifu na mbele ya Mwana- Kondoo.

11 Na moshi wa ule moto wa mateso yao utakuwa ukipanda juu kwa milele na milele. Wale walioabudu yule nyama na sanamu yake na mutu yeyote aliyepigwa chapa ya jina lake, hawatapumzika hata siku moja usiku na muchana.”

12 Kwa sababu hiyo, watu wa Mungu wanaoshika amri za Mungu na kumwamini Yesu wanapaswa kuwa wavumilivu.

13 Tena nikasikia sauti kutoka mbinguni, ikisema: “Andika maneno haya: ‘Heri tangu sasa kwa watu wanaokufa wakimwamini Bwana!’ ” Naye Roho anasema: “Ndiyo, ni kweli. Watapumzika toka katika masumbuko yao, kwa maana matendo yao yatafuatana nao.”


Mavuno ya dunia

14 Niliangalia tena, nami nikaona wingu jeupe, na juu ya wingu lile kulikuwa kukiikaa kiumbe kimoja kinachofanana na Mwana wa Mutu. Juu ya kichwa chake kulikuwa taji la zahabu, naye alikuwa akishika kisu kikali cha kuvuna katika mukono wake.

15 Malaika mwingine akatoka katika hekalu, akalalamika kwa sauti kubwa akimwambia yule aliyeikaa juu ya wingu: “Nyoosha kisu chako, uanze kuvuna, kwa maana dunia iko tayari kwa kuvunwa, nayo saa ya mavuno imetimia!”

16 Basi yule aliyeikaa juu ya wingu, akanyoosha kisu chake juu ya dunia na kuvuna dunia.

17 Malaika mwingine akatoka katika hekalu linalokuwa mbinguni, akiwa na kisu kikali cha kuvuna.

18 Kisha kukatokea malaika mwingine mwenye uwezo wa kuamuru moto, akatoka kwenye mazabahu, akamwambia kwa sauti kubwa yule aliyekuwa na kisu kikali cha kuvuna: “Nyoosha kisu chako, ukate matunda ya mizabibu yanayokuwa katika dunia kwa maana zabibu zimekomaa.”

19 Yule malaika akanyoosha kisu chake juu ya dunia, akachuma mizabibu ya dunia, akaitupa katika kikamulio kikubwa cha zabibu chenye kujaa kasirani ya Mungu.

20 Zile zabibu zikakamuliwa mbali na muji, damu ikatiririka toka ndani ya kile kikamulio mpaka ikafika kwenye umbali wa kilometre yapata mia tatu. Nao urefu kwenda chini wa ile damu ulikuwa yapata metre moja na nusu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan