Ruta 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ruta anashauriwa kupata mume 1 Siku moja, Naomi mama mukwe wa Ruta akamwambia: “Inanipasa kwangu kukutafutia mume kusudi upate uheri. 2 Sasa huyu Boazi, ambaye ulifanya kazi na wajakazi wake, si ni wa ukoo wetu? Basi sikiliza, magaribi hii atakuwa katika kiwanja akipepeta shayiri. 3 Kwa hiyo, nawa, ujipake mafuta na kuvaa vizuri, kisha uende kule katika kiwanja pahali anapopepetea. Lakini angalia usijionyeshe kwake mpaka atakapomaliza kula na kunywa. 4 Vilevile, ujue pahali atakapolala, na akisha kusinzia, umwendee polepole uifunue miguu yake ulale pale. Yeye atakuelezea la kufanya.” 5 Ruta akajibu: “Nitafanya yote uliyoniambia.” 6 Kwa hiyo, Ruta akakwenda kule katika kiwanja cha kupepetea, akafanya jinsi mama mukwe wake alivyomwamuru. 7 Boazi alipomaliza kula na kunywa, akachangamuka. Akakwenda karibu na lundo la shayiri, akalala. Ruta akakwenda polepole akafunua miguu yake na kulala pale. 8 Katikati ya usiku, Boazi akasisimuka, akageuka, akashituka kumukuta mwanamuke amelala kwenye miguu yake. 9 Akauliza: “Wewe ni nani?” Ruta akajibu: “Ni mimi Ruta, mujakazi wako. Kwa sababu wewe ni wa jamaa yangu wa karibu, uitande nguo yako juu ya mujakazi wako.” 10 Boazi akasema: “Yawe akubariki, kwa maana kwa yote unayofanya unaonyesha heshima zaidi kuliko uliyoyafanya pale mbele, kwa maana haukuwatafuta vijana wamasikini au tajiri wakuoe. 11 Sasa binti yangu usifazaike, nitakufanyia lolote utakaloomba kwa sababu kila mutu katika muji huu anajua wema wako. 12 Ni kweli kwamba ni mapaswa yangu kukutunza, lakini kuna vilevile mwenye mapaswa ya kukutunza na ambaye ni wa karibu zaidi kuliko mimi. 13 Kwa hiyo, kaa hapa usiku wote, na kesho asubui tutaona kama atakubali kukutunza au hapana. Ikiwa atakutunza ni vizuri. Kama vile Yawe anavyoishi, akikataa, mimi nitakutunza. Lala hapa mpaka asubui.” 14 Basi Ruta akalala pale kwenye miguu yake mpaka asubui, lakini akaamuka asubui mapema kusudi asionekane, kwa sababu Boazi hakutaka mutu ajue kwamba Ruta alikuwa kwenye kiwanja cha kupepetea. 15 Boazi akamwambia: “Tandika nguo yako chini.” Ruta akafanya hivyo. Boazi akamwanga shayiri yapata kilo kumi na tano, akamubebesha, naye akarudi katika muji. 16 Alipofika katika muji, mama mukwe wake akamwuliza: “Ilikuwa namna gani binti yangu?” Ruta akamwelezea yote ambayo Boazi alimutendea. 17 Halafu akaendelea kusema: “Akaniambia nisirudi kwa nyumba ya mama mukwe wangu mikono mitupu na kwa hiyo akanipa shayiri hii yapata kilo kumi na tano.” 18 Naye Naomi akasema: “Sasa tulia binti yangu Ruta, mpaka uone litakalotokea. Boazi hatatulia leo mpaka ameyatimiza yote.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo