Ruta 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Elimeleki na jamaa yake wanakwenda Moabu 1 Hapo zamani, wakati waamuzi walipokuwa wanatawala Waisraeli, kulitokea njaa katika inchi. Mutu mumoja kutoka Betelehemu katika Yuda pamoja na muke wake na watoto wao wanaume wawili walikwenda kuishi kwa muda katika inchi ya Moabu kwa kuishi kama wageni. 2 Mutu yule aliitwa Elimeleki na muke wake aliitwa Naomi. Watoto wao wawili wanaume, mumoja aliitwa Malona na mwingine Kiliona. Mutu yule na jamaa yake walikuwa wa kabila la Efuraimu kule Betelehemu katika Yuda. Walikwenda katika inchi ya Moabu, wakakaa kule. 3 Lakini Elimeleki, mume wa Naomi, akakufa na Naomi akaachwa na wana wake. 4 Vijana hao walioa wabinti wa Kimoabu, Orupa na Ruta. Nyuma ya miaka kumi hivi, 5 Malona na Kiliona nao vilevile wakakufa. Naomi na Ruta wanarudi Betelehemu 6 Kisha, Naomi akapata habari kwamba Yawe alikuwa amewabariki watu wake kwa kuwapa chakula. Basi, akaondoka kutoka Moabu kurudi kwao, pamoja na wakwe zake. 7 Akaondoka pahali pale alipoishi pamoja na wakwe zake, wakashika njia ya kurudi Yuda. 8 Naomi akawaambia hao wakwe zake wawili: “Murudi kila mumoja kwa mama yake. Ninaomba Yawe awatendee mema kama vile mulivyonitendea mema mimi na wale watu wangu waliokufa. 9 Yawe awajalie, kila mumoja wenu apate mume na nyumba yake.” Kisha Naomi akawaaga kwa kuwabusu. Lakini wao walianza kulia kwa sauti 10 na kumwambia: “Hapana hata kidogo! Tutakwenda pamoja nawe kwa watu wako.” 11 Naye Naomi akawasihi: “Murudi, wabinti zangu. Kwa nini kunifuata? Munafikiri ninaweza kupata tena watoto watakaokuwa waume zenu? 12 Murudi kwenu wabinti zangu, kwa maana mimi ni muzee sana, siwezi kuolewa tena. Hata kama ningesema nina tumaini, na hata kama ningepata mume usiku huu na kupata watoto, 13 mungeweza kungoja mpaka wakomae? Mungeweza kujizuia musiolewe na wanaume wengine? Sivyo, wabinti zangu! Mambo yangu ni magumu sana kwa ajili yenu, maana Yawe amenipiga pigo.” 14 Kwa hiyo wakalalamika wakaanza kulia tena. Halafu Orupa akamukumbatia mama mukwe wake, akamwaga na kurudi kwao. Lakini Ruta, akashikamana naye. 15 Basi Naomi akamwambia: “Ruta, angalia dada yako amerudi kwao na kwa mungu wake; basi, nawe vilevile urudi, umufuate dada yako.” 16 Lakini Ruta akamujibu: “Usinisihi nikuache wewe, wala usinizuie kufuatana nawe. Popote utakapokwenda ndipo nami nitakapokwenda, na pale utakapokaa mimi nitakaa, watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu. 17 Pale utakapokufia ni pale nitakufia nami, na ni palepale nitazikwa. Yawe anipe azabu kali kama nikitenganishwa nawe isipokuwa tu kwa kifo.” 18 Naomi alipoona kwamba Ruta ameamua kwenda pamoja naye, aliacha kumushawishi. 19 Halafu wote wawili wakaendelea na safari mpaka Betelehemu. Walipofika kule, watu wote wakashangaa, hata wanawake wakaulizana: “Huyu ni Naomi?” 20 Naomi akasema: “Musiniite tena Naomi muniite Mara, kwa maana Mungu Mwenye Nguvu ameyafanya maisha yangu yakuwe machungu sana. 21 Nilipoondoka hapa, nilikuwa na vitu vingi, lakini sasa Yawe amenirudisha mikono mitupu. Mbona munaniita Naomi ijapokuwa Yawe ameniazibu, naye Mungu Mwenye Nguvu amenitesa?” 22 Hivi ndivyo Naomi pamoja na mukwe wake Ruta wa Moabu walivyorudia kutoka Moabu, na wakafika Betelehemu wakati mavuno ya shayiri yalipokuwa yanaanza. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo