Nehemia 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Watu wanaungama zambi zao 1 Siku ya makumi mbili na ine ya mwezi ule wa saba, watu wa Israeli wakakusanyika, wakifunga kula na kuvaa nguo za magunia na kujipakaa udongo juu ya kichwa kwa kuonyesha majuto juu ya zambi zao. 2 Wakati ule, walikuwa wamejitenga mbali na watu wa mataifa mengine, wakasimama na kuungama zambi zao na maovu ya babu zao. 3 Kwa muda wa yapata saa tatu, walisimama wakati Sheria ya Yawe, Mungu wao, ikisomwa. Na kwa saa tatu zilizofuata, walikuwa wakitubu na kumwabudu Yawe, Mungu wao. 4 Kuliwekwa daraja la Walawi; pale kulisimama Yesua, Bani, Kadimieli, Sebania, Buni, Serebia, Bani na Kenani. Wakamwomba kwa sauti kubwa Yawe, Mungu wao. 5 Walawi, ni kusema Yesua, Kadimieli, Bani, Hasabuea, Serebia, Hodia, Sebania na Petahia, wakawaambia watu: Musimame na kumusifu Yawe, Mungu wenu. Mumusifu milele na milele! Na watu wakasifu jina lako tukufu, ambalo linatukuka kuliko baraka na sifa zote. Maombi ya usamehe wa zambi 6 Ezra akaomba akisema: Wewe peke yako ndiwe Yawe! Ulifanya mbingu na jeshi lake lote, dunia na vyote vinavyokuwa ndani yake, bahari na vyote vinavyokuwa ndani yake. Unavipatia uzima, na jeshi lote la mbinguni linakuabudu wewe. 7 Wewe ndiwe Yawe, Mungu uliyemuchagua Abramu. Ukamutoa toka Uri ya Wakaldea na kumupa jina la Abrahamu. 8 Ukamwona kuwa wa haki mbele yako; ukafanya agano naye kuwapa wazao wake inchi ya Wakanana, Wahiti, Waamori, Waperizi, Wayebusi na Wagirgasi. Na ahadi yako ukaitimiza; maana wewe ni mwaminifu. 9 Uliyaona mateso ya babu zetu walipokuwa katika inchi ya Misri, na walipokuomba musaada kwenye bahari Nyekundu ukawasikiliza. 10 Ulifanya miujiza na maajabu mbele ya Mufalme wa Misri, watumishi wake wote na watu wote wa inchi yake; maana ulijua kwamba waliwagandamiza babu zetu. Ukajipatia utukufu unaokuwa mpaka leo. 11 Uligawanya bahari katikati mbele yao, nao wakapita katikati ya bahari, pahali pakavu. Lakini ukawatupa Wamisri waliowafuatilia kama jiwe zito ndani ya maji mengi. 12 Muchana uliwaongoza kwa nguzo la wingu, na usiku uliwaongoza kwa nguzo la moto kwa kuwaangazia njia ya kufuata. 13 Kule kwa mulima Sinai ulishuka toka mbinguni na kuzungumuza nao. Ukawapa maagizo safi, sheria za kweli, masharti mazuri na amri. 14 Kwa njia ya Musa, mutumishi wako, ukawajulisha siku zako za Sabato takatifu na ukawaagiza kuzifuata amri, masharti na sheria ulizowaamuru. 15 Walipokuwa na njaa, ukawapa chakula kutoka mbinguni. Walipokuwa na kiu, ukawapa maji kutoka katika jiwe. Ukawaagiza kurizi inchi uliyokuwa umewaahidi. 16 Lakini wao na babu zetu wakakuwa na kiburi na wakakuwa wagumu wakakataa kufuata maagizo yako. 17 Wakakataa kutii; hawakukumbuka maajabu uliyofanya kati yao. Wakakuwa wagumu, wakajichagulia kiongozi wa kuwarudisha katika utumwa katika inchi ya Misri. Lakini wewe Mungu uko mwepesi kwa kusamehe, mwenye huruma na rehema, haukasiriki upesi, uko mwema sana. Haukuwatupilia 18 hata walipojitengenezea sanamu ya mwana-ngombe na kusema: “Huyu ndiye Mungu wetu aliyetutoa kutoka katika inchi ya Misri.” Wakakuchukiza sana 19 lakini wewe kwa rehema zako nyingi haukuwatupilia kule katika jangwa. Nguzo la wingu lililowaongoza muchana, wala nguzo la moto lililowaangazia katika njia usiku, havikuondoka. 20 Ukawapa Roho wako mwema kuwashauria; ukawapa mana kuwa chakula chao, na maji ya kunywa kwa kutuliza kiu chao. 21 Ukawatunza katika jangwa kwa miaka makumi ine na hawakukosa kitu chochote; nguo zao hazikuchakaa wala miguu yao haikuvimba. 22 Ukawapatia ushindi juu ya falme na mataifa, ukawafanyia mengi kila upande. Wakashinda inchi ya Hesiboni iliyotawaliwa na mufalme Sihoni; na tena wakashinda inchi ya Basani iliyotawaliwa na mufalme Ogi. 23 Ukafanya wazao wao kuwa wengi kama nyota za mbinguni; ukawaleta katika inchi uliyowaahidi babu zao. 24 Hivyo, hao wazao wakakuja na kurizi inchi. Ulishinda Wakanana na kuwatia katika mikono yao. Watu wako waliweza kuwatendea vile walivyotaka wafalme na watu wa inchi hiyo. 25 Wakateka miji yenye kuta, wakatwaa inchi yenye utajiri, nyumba zenye vitu vingi vizuri, visima vilivyochimbwa, mashamba ya mizabibu na mizeituni pamoja na miti yenye matunda kwa wingi. Hivyo wakakula, wakashiba na kunenepa na kufurahia wema wako. 26 Lakini hawakukuwa waaminifu kwako. Wakakuasi, wakaacha sheria yako na kuwaua manabii waliowaonya kusudi wakurudilie wewe. Wakatenda zambi kubwa mbele yako. 27 Hivyo, ukawatia katika mikono ya waadui zao, nao wakawatesa. Lakini wakiwa katika mateso yao, wakakulilia, nawe ukawasikiliza kutoka mbinguni. Na kwa rehema zako nyingi, ukawatumia viongozi wa kuwaokoa; nao wakawakomboa toka katika mikono yao. 28 Lakini amani ilipopatikana wakatenda zambi tena mbele yako, nawe ukawaacha watiwe katika mikono ya waadui zao wawatawale. Hata hivyo, walipotubu na kukulilia ukawasikiliza kutoka mbinguni. Na kwa kulingana na rehema zako nyingi, ukawaokoa mara nyingi. 29 Ukawaonya kusudi warudilie Sheria yako, hata hivyo, kwa kiburi chao, wakaacha kutii amri zako. Wakaasi maagizo yako, ambayo kwa njia yake mutu akiyatii, ataishi. Wakakuwa wenye kiburi vilevile wakakuwa wagumu, na wakakataa kuwa watiifu. 30 Ukawavumilia kwa miaka mingi, na kuwaonya kwa njia ya roho wako kwa kupitia manabii wako; hata hivyo hawakusikiliza. Basi ukawaacha ukawatia katika mikono ya mataifa mengine. 31 Hata hivyo, kutokana na rehema zako nyingi, haukuwaachilia waangamie kabisa au kuwatupilia, maana wewe ni Mungu mwenye huruma na rehema. 32 Kwa hiyo, ee Mungu wetu, Mungu mukubwa, mwenye nguvu na wa kutisha, wewe unashika agano lako na kutenda wema. Mateso yaliyotupata, sisi, wafalme wetu, wakubwa wetu, makuhani wetu, manabii wetu, babu zetu na watu wako wote tangu wakati wa wafalme wa Asuria mpaka leo, usiyaone kuwa ni madogo. 33 Hata hivyo, una haki kwa kutuazibu hivyo; maana wewe umekuwa mwaminifu wakati sisi tumekuwa watenda maovu. 34 Wafalme wetu, wakubwa wetu, makuhani wetu na babu zetu hawakushika Sheria yako wala kujali amri zako na maonyo yako uliyowapa. 35 Hawakukutumikia katika ufalme wao, wala walipofurahia mema yako mengi uliyowajalia kwa wingi, katika inchi kubwa na yenye mboleo uliyowapa hawakuyaacha matendo yao maovu. 36 Na leo tumekuwa watumwa; tuko watumwa katika inchi uliyowapa babu zetu kwa kufurahia matunda yake na mazao yake mema. 37 Kwa sababu ya zambi zetu, utajiri wa inchi hii unawaendea wafalme uliowaleta kwa kututawala. Wanatutawala jinsi wanavyopenda hata na nyama wetu wa ufugo wanawatendea jinsi wanavyopenda, tuko katika taabu kubwa sana. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo