Nehemia 13 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kujitenga na watu wengine 1 Katika siku ile ya sherehe, kitabu cha Musa kikasomwa na ikajulikana kwamba Waamoni na Wamoabu hawaruhusiwi kuingia katika mukutano wa watu wa Mungu. 2 Kwa sababu watu wa Israeli, walipokuwa wanasafiri toka Misri, wao hawakuwapa chakula wala maji ya kunywa, pahali pake wakamulipa Balamu kwa kuwalaani watu wa Israeli, lakini Mungu wetu akageuza laana yao kuwa baraka. 3 Watu wa Israeli waliposikia Sheria hiyo wakawatenga watu wa mataifa mengine. Nehemia anafanya mapinduzi 4 Mbele ya siku ya sherehe, kuhani Eliasibu aliyekuwa amechaguliwa kwa kulinda vyumba vya nyumba ya Mungu wetu, na mwenye ushirika mwema na Tobia, 5 alimuruhusu Tobia kutumia chumba kikubwa ambamo pale mbele walikuwa wakiweka sadaka za unga, ubani, vyombo, zaka za unga, divai, mafuta; vitu hivyo vyote Waisraeli walivyoagizwa kutoa kwa Walawi, waimbaji, walinzi wa milango, na matoleo kwa makuhani. 6 Wakati mambo haya yalipokuwa yanatendeka mimi sikukuwa Yerusalema; maana katika mwaka wa makumi tatu na mbili wa utawala wa mufalme Artasasta wa Babeli, nilikuwa nimeomba ruhusa; nami nikaenda kwake. 7 Niliporudi Yerusalema ndipo nikagundua uovu wa Eliasibu wa kumutayarishia Tobia chumba katika kiwanja cha nyumba ya Mungu. 8 Nikakasirika sana na nikavitupilia inje vyombo vyote vya Tobia. 9 Nikaamuru watu, nao wakatakasa vyombo hivyo halafu nikarudisha mule vifaa vya nyumba ya Mungu, pamoja na sadaka ya unga na ubani. 10 Tena nikagundua kwamba Walawi hawakupewa haki zao; na matokeo yake ni kwamba Walawi na waimbaji waliokuwa wakifanya kazi pale mbele, sasa walikwisha kurudilia mashamba yao. 11 Nikawakaripia viongozi, nikisema: “Kwa nini nyumba ya Mungu imeachwa?” Nikawakusanya pamoja na kuwarudisha katika kazi. 12 Kisha, watu wote wa Israeli, wakaanza tena kuleta zaka zao za unga, divai na mafuta kwenye gala. 13 Nikachagua watu hawa kuwa walinzi wa gala: kuhani Selemia, Zadoki mwandishi na Pedaya, Mulawi. Hanani mwana wa Zakuri mujukuu wa Matania akakuwa musaidizi wao. Walikuwa waaminifu na kazi yao ilikuwa kuwagawanyia wandugu zao mahitaji yao. 14 Ee Mungu wangu, unikumbuke kwa ajili ya haya yote na usiyasahau matendo yangu mema niliyofanya kwa ajili ya nyumba yako na kwa ajili ya kazi yako. 15 Wakati uleule, nikawaona watu wa Yuda wakikamua zabibu katika vikamulio siku za Sabato. Tena wengine walikuwa wakiwabebesha punda wao ngano, divai, zabibu, tini na vitu vingine wakivipeleka Yerusalema. Nikawaonya kwamba hawana ruhusa ya kuuzisha katika siku hiyo. 16 Watu wengine toka muji wa Tiro walileta samaki na biashara nyingine Yerusalema na kuwauzishia watu wetu siku ya Sabato. 17 Nikawakaripia viongozi wa watu wa Yuda, nikisema: “Uovu gani huu munaofanya, kuichafua siku ya Sabato? 18 Babu zetu hawakufanya uovu wa namna hiihii na kumusukuma Mungu wetu kutuletea hasara pamoja na muji huu? Na munazidi kuamusha kasirani yake juu ya watu wa Israeli kwa kuchafua siku ya Sabato.” 19 Halafu, nikaamuru kwamba milango ya Yerusalema ifungwe wakati siku ya Sabato inapoanza magaribi, wakati giza linapoanza kuingia, na isifunguliwe mpaka Sabato imekwisha. Nikaweka watumishi wangu wamoja kwenye milango na kuwaagiza kwamba kitu chochote kisiletwe katika muji siku ya Sabato. 20 Mara mbili au tatu hivi wachuuzi waliokuwa wakiuzisha biashara ya aina mbalimbali walipaswa kulala inje ya muji. 21 Nikawaonya na kuwaambia: “Hakuna maana kulala inje ya muji. Mukijaribu tena nitatumia nguvu.” Hivyo tangu wakati ule hawakurudi tena siku ya Sabato. 22 Nikaagiza Walawi kujitakasa na kwenda kulinda milango kwa kutakasa siku ya Sabato. Ee, Mungu wangu, unikumbuke hata na kwa hili vilevile unihurumie kutokana na rehema zako kubwa. 23 Tena wakati ule nikaona Wayuda waliooa wanawake toka Asidodi, Amoni na Moabu; 24 na nusu ya watoto wao waliosema luga ya Kiasidodi au luga nyingine na hawakuweza kusema luga ya inchi ya Yuda. 25 Nikawakaripia na kuwalaani, hata nikawapiga wamoja kati yao na kuwaongoa nywele zao. Nikawalazimisha kuapa kwa jina la Mungu, nikisema: “Wabinti zenu musiwaoeshe kwa vijana wao, wala wabinti zao wasiolewe na vijana wenu au na ninyi wenyewe. 26 Si Solomono alitenda zambi kwa sababu ya wanawake wa namna hiyo? Yeye alikuwa mufalme mukubwa kuliko wafalme wa mataifa mengine. Mungu akamupenda na akamufanya kuwa mufalme juu ya watu wote wa Israeli, hata hivyo wanawake wa mataifa mengine, wakamusukuma kutenda zambi. 27 Basi, sasa tufuate mufano wenu na tutende zambi hii kubwa ya kutomutii Mungu wetu kwa kuoa wanawake wa kigeni?” 28 Mumoja kati ya wana wa Yoyada mwana wa Kuhani Mukubwa Eliasibu, alioa binti wa Sanibalati kutoka muji wa Beti-Horoni, kwa sababu hiyo nikamufukuza kutoka mbele yangu. 29 Ee Mungu, kumbuka jinsi watu walivyochafua ukuhani na agano la kikuhani na la Walawi. 30 Nikawatakasa watu kutokana na chochote kilichokuwa cha kigeni. Nikatayarisha utaratibu kwa ajili ya makuhani na Walawi juu ya kazi ya kila mumoja wao. 31 Nikaagiza matoleo ya kuni kufanyika katika wakati unaopaswa na malimbuko wakati wake. Ee Mungu wangu, unikumbuke kwa ajili ya haya yote na unijalie mema. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo