Nahumu 2 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Enyi watu wa Yuda muangalie: Mutu anakuja kutoka milima anayeleta habari njema, anayetangaza amani. Mufanye sikukuu zenu, mutimize viapo vyenu, maana waovu hawatawashambulia, kwa sababu wameangamizwa kabisa. Kuanguka kwa Ninawe 2 Mwangamizaji amekuja kukushambulia, ee Ninawe. Chunga kuta zako! Weka ulinzi katika barabara! Ujiweke tayari! Kusanya nguvu zako zote! 3 Yawe anamurudishia Yakobo utukufu wake, anawapa tena Waisraeli utukufu wao, ingawa washambulizi hawakuwaachia kitu, hata matawi yao ya mizabibu waliyakata. 4 Ngao za mashujaa wake ni nyekundu, waaskari wake wamevaa nguo nyekundu sana. Magari yao ya vita yanametameta kama ndimi za moto, yamepangwa tayari kwa kushambulia; farasi hawatulii kwa hamu ya kushambulia. 5 Magari ya vita yanakimbia mbio katika barabara, yanakwenda huko na huko katika uwanja. Yanametameta kama ndimi za moto! Yanakwenda mbio kama umeme. 6 Sasa anawaita wakubwa wake, nao wanajikwaa wanapomwendea; wanakwenda kwenye ukuta kwa haraka kutayarisha ukingo. 7 Vikingio vya mito vimefunguliwa, nyumba ya kifalme imejaa hofu. 8 Muji uko wazi kabisa, watu wamekamatwa mateka. Wanawake wake wanaomboleza, wanalia kama njiwa, na kujipigapiga kwenye vifua. 9 Muji Ninawe ni kama birika lililobomoka, watu wake wanaukimbia ovyo. Musimame! Musimame! Sauti inaita, lakini hakuna anayerudi nyuma. 10 Munyanganye feza, munyanganye zahabu! Mali yake haina mwisho! Kuna wingi wa kila kitu cha bei kali! 11 Muji wa Ninawe ni maangamizi matupu na uharibifu! Watu wamekufa moyo, magoti yanagongana, nguvu zimewaishia, nyuso zimebadilika! 12 Basi lile pango la simba limekuwa namna gani, lile lililokuwa maficho ya simba wakali? Ile nafasi ya simba imekuwa namna gani, nafasi ya wana-simba ambayo hakuna aliyeweza kuwashitua? 13 Simba dume amewararulia watoto wake nyama ya kutosha, akiwakamatia simba dike nyama zao; ameyajaza mapango yake na nyama, na makao yake vipande vya nyama. 14 Mimi Yawe wa majeshi nitakushambulia: nitayateketeza kwa moto magari yako ya vita, nitawamaliza kwa upanga hao simba wako wakali, vitu ulivyonyanganya nitavikomesha kutoka katika inchi, na sauti ya wajumbe wako haitasikilika tena. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo