Nahumu 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maulizo ya watu ( Isa 2.1-4 ) 1 Ujumbe wa Mungu juu ya Ninawe. Kitabu cha maono ya Nahumu wa Elkosi. Kasirani ya Mungu juu ya Ninawe 2 Yawe ni Mungu mwenye wivu, anayelipiza kisasi; Yawe analipiza kisasi na ni mwenye kasirani; Yawe analipiza kisasi kwa wapinzani wake, kasirani yake inawaka juu ya waadui zake. 3 Yawe hakasiriki upesi, lakini amejaa nguvu, Yawe hatawaachilia wenye makosa hata kidogo. Yawe anapopita, upepo mukali na zoruba vinatokea; mawingu ni mavumbi yanayonyanyuliwa na miguu yake. 4 Anaikaripia bahari na kuikausha, yeye anaikausha mito yote. Mbuga za Basani na mulima Karmeli zinanyauka, maua ya Lebanoni yanakauka. 5 Milima inatetemeka mbele yake, vilima vinayeyuka. Dunia inatetemeka mbele yake, ulimwengu na vyote vinavyokuwa ndani yake. 6 Nani anayeweza kusimama mbele ya kasirani ya Yawe? Nani anayeweza kuvumilia ukali wa hasira yake? Yeye anaimwanga hasira yake inayowaka kama moto, hata mawe makubwa anayapasua vipandevipande. 7 Yawe ni muzuri, yeye ni kimbilio la usalama wakati wa taabu. Yeye anawalinda wote wanaokimbilia usalama kwake. 8 Waadui wakishambulia inchi kama mafuriko, yeye anawaangamiza; anawafuatilia na kuwafukuza mpaka katika giza. 9 Mbona munafanya mipango juu ya Yawe? Yeye atawakomesha na kuwaangamiza, wala mupinzani wake hataweza kusimama tena. 10 Watateketezwa kama kichaka cha miiba, wao wanaoikalia kulewa. Watateketezwa kama vile majani yenye kukauka. 11 Ndani yako kumetoka mumoja aliyepanga maovu juu ya Yawe. Huyu mutu anafanya shauri baya sana. 12 Yawe anasema hivi: Ingawa Waasuria ni wengi na wenye nguvu, wao wataangushwa na kuangamizwa. Ingawa nimewatesa ninyi watu wangu, sitawatesa tena zaidi. 13 Sasa nitaivunja nira ya Asuria katika shingo lenu, na minyororo waliyowafungia nitaikatakata. 14 Yawe ameamuru hivi juu ya Ninawe: Hautapata wazao kwa kulidumisha jina lako. Sanamu zako za kuchonga na za chuma chenye kuyeyushwa, nitazivunjavunja katika nyumba za miungu yako. Mimi nitakuchimbia kaburi lako, maana wewe haufai kwa kitu chochote. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo