Mwanzo 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu anafanya agano na Noa 1 Mungu akamubariki Noa na wana wake, akiwaambia: “Muzae, muongezeke, mujaze inchi. 2 Nyama wote, ndege wote wa anga, viumbe vyote vinavyotambaa juu ya inchi na samaki wote wa bahari watakuwa na hofu na kuwaogopa ninyi. Wote wamewekwa chini ya mamlaka yenu. 3 Nyama wote wenye uzima watakuwa chakula chenu; ninawapa nyama hao kama vile nilivyowapa mimea kuwa chakula chenu. 4 Lakini musikule nyama wenye damu, maana uzima uko katika damu. 5 Damu ya uzima wenu nitaidai. Nitaidai kutoka kwa kila nyama na mwanadamu. Atakayemwua mwanadamu mwenzake, nitamudai uzima wake. 6 Anayemwanga damu ya mwanadamu, damu yake itamwangwa na mwanadamu; maana mwanadamu aliumbwa kwa mufano wa Mungu. 7 Nanyi muzae, mwongezeke, muzae kwa wingi, mwongezeke katika inchi.” Upinde wa mvua 8 Kisha Mungu akamwambia Noa na wana wake: 9 “Ninasimamisha agano langu nanyi na wazao wenu 10 na viumbe vyote vyenye uzima, ndege, nyama wa kufugwa na wa pori, wote waliotoka katika chombo pamoja nanyi. 11 Ninasimamisha agano langu nanyi, kwamba hakutatokea tena mafuriko ya maji kwa kuangamiza inchi nzima au viumbe vyote vyenye uzima.” 12 Tena Mungu akasema: “Hiki ndicho kitambulisho cha agano ninalofanya kati yangu nanyi na kila kiumbe chenye uzima kinachokuwa pamoja nanyi kwa vizazi vyote vinavyokuja: 13 ninaweka upinde wangu katika mawingu, nao utakuwa kitambulisho cha agano kati yangu na dunia. 14 Kila mara nitakapofunika dunia kwa mawingu, na huo upinde wa mvua utakapoonekana katika mawingu, 15 nitakumbuka agano langu nanyi na viumbe vyote vyenye uzima. Maji hayatageuka hata kidogo kuwa mafuriko ya kuangamiza viumbe vyote vyenye uzima. 16 Huo upinde utakapotokea katika mawingu, nitauona na kukumbuka agano hilo la milele kati yangu na viumbe vyote vyenye uzima katika dunia.” 17 Mungu akamwambia Noa: “Hiki ndicho kitambulisho cha agano ambalo nimesimamisha na viumbe vyote vyenye uzima katika dunia.” Noa na wana wake 18 Wana wa Noa waliotoka katika chombo walikuwa Semu, Hamu na Yafeti. Hamu alikuwa baba ya Kanana. 19 Hao ndio wana watatu wa Noa na kutokana nao watu walienea katika dunia yote. 20 Noa alikuwa mulimaji wa kwanza kupanda mizabibu. 21 Akakunywa divai, akalewa, kisha akalala uchi ndani ya hema yake. 22 Hamu, baba ya Kanana, akaona uchi wa baba yake, akatoka inje na kuwaambia wandugu zake wawili. 23 Lakini Semu na Yafeti wakatwaa nguo, wakaiweka juu ya mabega yao, wakakwenda kinyumenyume na kufunika uchi wa baba yao. Waliangalia pembeni, wala hawakuuona uchi wa baba yao. 24 Ulevi wa Noa ulipokwisha naye alipojua alivyotendewa na mwana wake mudogo, 25 akasema: “Kanana alaaniwe! Atakuwa mutumwa wa watumwa kwa wandugu zake.” 26 Tena akasema: “Semu abarikiwe na Yawe, Mungu wangu! Kanana akuwe mutumwa wake. 27 Mungu amuzidishe Yafeti, aishi katika hema za Semu; Kanana akuwe mutumwa wake.” 28 Nyuma ya mafuriko ya maji, Noa aliishi miaka mia tatu na makumi tano, 29 kisha akakufa akiwa na umri wa miaka mia tisa na makumi tano. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo