Mwanzo 45 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yosefu anajitambulisha 1 Halafu Yosefu akashindwa kujizuia mbele ya wote waliokuwa pamoja naye, akawaamuru watoke inje. Hivyo Yosefu alikuwa peke yake alipojitambulisha kwa wandugu zake. 2 Lakini akalia kwa sauti kubwa hata Wamisri wakamusikia. Vilevile watu wa jamaa ya mufalme nao wakamusikia. 3 Yosefu akawaambia wandugu zake: “Mimi ni Yosefu. Baba yangu angali muzima?” Lakini wandugu zake wakapigwa na bumbuazi mbele yake, hata wakashindwa kumujibu. 4 Yosefu akawaambia wandugu zake: “Tafazali, musogee karibu nami.” Walipomukaribia, akawaambia: “Mimi ndiye ndugu yenu Yosefu, muliyemwuzisha Misri. 5 Lakini sasa musifazaike wala kuhuzunika kwa kuniuzisha. Mungu ndiye aliyenileta huku niwatangulie, kusudi niyaokoe maisha ya watu. 6 Huu ni mwaka wa pili tu wa njaa katika inchi, na kungali miaka mitano zaidi ambapo watu hawataweza kulima wala kuvuna mavuno. 7 Mungu alinileta huku niwatangulie ninyi, kwa kuokoa maisha yenu mubaki wazima katika inchi na kuwakomboa kwa ukombozi mukubwa. 8 Kwa hiyo, si ninyi mulionileta huku, lakini ni Mungu. Ndiye aliyenifanya kama baba kwa mufalme wa Misri, musimamizi wa nyumba yake yote na mutawala wa inchi yote ya Misri. 9 “Basi, mufanye haraka! Muende kwa baba na kumwambia: ‘Mwana wako Yosefu anasema: Mungu amenifanya kuwa mukubwa wa inchi yote ya Misri. Basi, usikawie kuja kwangu. 10 Utakaa karibu nami katika eneo la Goseni: wewe, wana wako na wajukuu wako, nyama wako wa kufugwa na mali yako yote. 11 Utakapokuwa Goseni, mimi nitakutunza wewe na jamaa yako pamoja na nyama wako kusudi musikufe na njaa, maana kungali miaka mitano zaidi ya njaa.’ ” 12 Kisha Yosefu akasema: “Ninyi wenyewe mumeona kwa macho yenu na hata ndugu yangu Benjamina ameona kwa macho yake kwamba ni mimi mwenyewe Yosefu ninayezungumuza nanyi. 13 Ni lazima kumwambia baba yangu juu ya utukufu wangu huku Misri na yote muliyoyaona. Basi, mufanye haraka, mumulete baba yangu huku.” 14 Kisha Yosefu akamukumbatia Benjamina, ndugu yake, akalia. Benjamina naye akalia, wakiwa wanakumbatiana. 15 Akiwa angali analia, Yosefu akawakumbatia wandugu zake na kuwabusu. Hapo ndipo wandugu zake walipoweza kuzungumuza naye. Mufalme wa Misri anamwalika Yakobo akuje Misri 16 Habari zile zilipofika kwa nyumba ya mufalme, kwamba wandugu za Yosefu wamekuja, zikamufurahisha sana na watumishi wake. 17 Kwa hiyo, mufalme akamwambia Yosefu: “Uwaambie wandugu zako wawapakie punda wao mizigo, warudi kwa inchi ya Kanana, 18 wamulete hapa baba yao na jamaa zao wote. Mimi nitawapa sehemu nzuri kabisa ya inchi ya Misri, ambako wataweza kufurahia matunda yote ya inchi hii. 19 Uwaambie vilevile wapeleke kutoka hapa magari ya kukokotwa ya kuwaleta watoto wao wachanga na wake zao. Wala wasikose kumuleta baba yao. 20 Uwaambie wasijali juu ya mali zao, maana sehemu nzuri kuliko zote katika inchi ya Misri itakuwa yao.” 21 Basi, wana wa Israeli wakafanya kama vile walivyoagizwa. Yosefu akawapa magari kulingana na maagizo ya mufalme na chakula cha njia. 22 Aliwapa kila mumoja wao nguo za kubadilisha, lakini akamupa Benjamina vikoroti mia tatu vya feza na nguo tano za kubadilisha. 23 Tena alimupelekea baba yake zawadi hizi kwa ajili ya safari yake: punda kumi waliobeba vitu bora vya Misri, na punda dike kumi waliobeba ngano, mikate na vyakula vingine. 24 Basi, Yosefu akaagana na wandugu zake. Walipokuwa wanaondoka akawaonya akisema: “Musigombane katika njia!” 25 Basi, wakatoka Misri na kurudi kwa baba yao Yakobo, katika inchi ya Kanana. 26 Wakamwambia baba yao: “Yosefu iko muzima! Yeye ndiye mutawala wa inchi yote ya Misri!” Hapo baba yao akapigwa na bumbuazi, maana hakuweza kuyasadiki maneno yao. 27 Lakini, walipomwelezea yote waliagizwa na Yosefu na alipoona magari aliyopelekewa na Yosefu kwa kumubeba, moyo wake ukajaa furaha kupita kiasi. 28 Israeli akasema: “Sasa inatosha! Mwana wangu Yosefu yuko muzima! Nitakwenda nimwone mbele ya kufa kwangu.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo