Mwanzo 44 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kikombe kinapatikana kwa Benjamina 1 Kisha Yosefu akamwagiza musimamizi wa nyumba yake akisema: “Ujaze mifuko ya watu hawa ngano kipimo watakachoweza kubeba. Halafu, weka feza ya kila mumoja wao kwenye kinywa cha mifuko wake. 2 Katika mufuko wa yule mudogo kabisa, uweke kile kikombe changu cha feza, pamoja na feza yake.” Yule musimamizi akafanya kama vile alivyoamuriwa na Yosefu. 3 Kulipopambazuka wakaruhusiwa kuondoka pamoja na punda wao. 4 Walipokuwa wamesafiri mwendo mufupi tu kutoka muji, Yosefu akamwambia musimamizi wa nyumba yake: “Haraka! Ufuate wale watu, na utakapowakuta, uwaulize: ‘Kwa nini mumelipa mema muliyotendewa kwa maovu? Kwa nini mumeiba kikombe cha bwana wangu ambacho 5 yeye anakunywa nacho na kukitumia kwa kuaguza? Mumekosa sana kwa kufanya hivyo!’ ” 6 Yule musimamizi alipowakuta akawaambia maneno hayo. 7 Lakini wao wakamwuliza: “Bwana, una maana gani kutuambia maneno kama hayo? Sisi watumishi wako hatuwezi kufanya jambo kama hilo! 8 Kumbuka, bwana, feza tuliyokuta katika kinywa cha mifuko yetu tuliirudisha kutoka katika inchi ya Kanana. Itawezekana namna gani tena tuibe feza au zahabu kutoka nyumba ya bwana wako? 9 Basi, kama akipatikana mumoja wetu ana kikombe hicho, auawe na sisi wengine wote tutakuwa watumwa wako.” 10 Huyo musimamizi akasema: “Sawa. Ikuwe kama mulivyosema. Yeyote atakayepatikana na kikombe hicho, atakuwa mutumwa wangu, lakini wengine wote hamutakuwa na kosa.” 11 Basi, kila mumoja akashusha mufuko wake chini haraka na kuufungua. 12 Yule musimamizi akapekua mifuko yote, akianza na wakubwa wao na kumalizia na mudogo kabisa. Kikombe kikapatikana katika mufuko wa Benjamina. 13 Kwa hiyo wakararua nguo zao kwa huzuni. Kila mumoja wao akamubebesha punda wake muzigo wake, wakarudi kwa muji. 14 Yuda na wandugu zake wakafika kwa Yosefu naye Yosefu alikuwa bado katika nyumba. Basi, wakainama mbele yake kwa heshima, 15 naye Yosefu akawauliza: “Kwa nini mumefanya hivyo? Hamujui kwamba mutu kama mimi nina uwezo wa kuaguza?” 16 Yuda akamujibu: “Tukuambie nini bwana? Tuseme nini kwa kuonyesha kwamba hatuna kosa? Mungu ameyafichua makosa yetu, sisi watumishi wako. Sasa sisi wote tuko watumwa wako, sisi pamoja na yule aliyepatikana na kikombe chako.” 17 Lakini Yosefu akasema: “Hapana! Mimi siwezi kufanya hivyo! Yule tu aliyepatikana na kikombe changu ndiye atakayekuwa mutumwa wangu. Ninyi wengine wote murudi kwa amani kwa baba yenu.” Yuda anamutetea Benjamina 18 Halafu Yuda akamukaribia Yosefu na kumwambia: “Bwana, ninakuomba uniruhusu mimi mutumishi wako, nijitetee mbele yako kwa maneno machache. Ninakusihi usinikasirikie, maana wewe ni kama mufalme wa Misri mwenyewe. 19 Bwana, wewe ulituuliza kama tuna baba au ndugu, 20 nasi tukakuelezea kwamba tuko na baba, naye ni muzee, na kwamba tuko na ndugu mwingine mudogo aliyezaliwa wakati wa uzee wa baba yetu. Kaka yake na yule kijana amekwisha kufa, na yule mudogo ndiye peke yake aliyebaki wa mama yake; na muzee wetu anamupenda sana kijana yule. 21 Bwana, ulituagiza sisi watumishi wako kumuleta yule mudogo wetu upate kumwona. 22 Tukakuelezea kwamba yule kijana hawezi kuachana na baba yake, kwa sababu akifanya hivyo baba yake atakufa. 23 Lakini wewe bwana ukatuambia kwamba kama hatutakuja na ndugu yetu mudogo, hautatupokea tena. 24 “Tuliporudi kwa mutumishi wako, baba yetu, tulimwarifu ulivyotuagiza, bwana. 25 Naye alipotuambia tukuje tena huku kununua chakula, 26 tukamwambia: ‘Hatuwezi kwenda, isipokuwa tu kama ndugu yetu mudogo atakwenda pamoja nasi. Kama hatakwenda pamoja nasi hatuwezi kupokelewa na yule mutu.’ 27 Basi, baba yetu, mutumishi wako, akatuambia: ‘Munajua kwamba muke wangu Rakeli alinizalia wana wawili: 28 mumoja alitoweka, nami nikasema, bila shaka ameraruliwa vipandevipande na nyama wa pori, maana sijapata kumwona tena. 29 Kama mutamupeleka huyu vilevile kutoka kwangu, akipatwa na hasara, basi mutanishusha katika kaburi nikiwa muzee mwenye huzuni.’ 30 “Kwa hiyo, bwana, siwezi kumurudilia baba yangu, mutumishi wako, bila kijana huyu. Uzima wa baba unategemea uzima wa kijana huyu, 31 na akiona kwamba kijana hayupo pamoja nasi, atakufa! Hivyo sisi watumishi wako tutamwua baba yetu kwa huzuni. 32 Zaidi ya hayo, mimi peke yangu nilijitoa kuwa rehani kwa huyu kijana kwa baba yangu, nikisema: ‘Nisipomurudisha Benjamina kwako, kosa likuwe juu yangu milele.’ 33 Sasa, ee bwana, ninakusihi, mimi mutumishi wako, nibaki, nikuwe mutumwa wako pahali pa kijana huyu. Umwache yeye arudi pamoja na wandugu zake. 34 Nitaweza namna gani kumurudilia baba yangu bila kijana huyu? Siwezi kuvumilia kuona hasara itakayomupata baba yangu.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo