Mwanzo 42 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wandugu za Yosefu wanakwenda Misri 1 Yakobo alipopata habari kwamba kulikuwa ngano kule Misri, akawaambia wana wake: “Mbona munaikaa mukiangaliana tu? 2 Nimesikia kwamba Misri kuna ngano. Muende kule mununue ngano tusikufe na njaa.” 3 Hivyo wandugu kumi za Yosefu wakaenda kwa kununua ngano. 4 Lakini Yakobo hakumwacha Benjamina, ndugu ya Yosefu, aende pamoja nao maana aliogopa kwamba angeweza kupata hasara. 5 Basi, wana wa Israeli wakafika Misri wakiwa kati ya wanunuzi wengine, maana hata katika inchi ya Kanana kulikuwa njaa. 6 Wakati ule Yosefu alikuwa mukubwa kule Misri. Yeye ndiye aliyekuwa akiwauzishia wanainchi ngano. Basi, kaka zake wakakuja na kuinama mbele ya Yosefu kwa heshima. 7 Yosefu alipoona kaka zake akawatambua, lakini akajifanya sawa vile hawafahamu, akasema nao kwa ukali. Akawauliza: “Mumetoka wapi ninyi?” Wakamujibu: “Tumetoka katika inchi ya Kanana, tumekuja kununua chakula.” 8 Ingawa Yosefu aliwatambua kaka zake, wao hawakumutambua. 9 Akakumbuka ndoto zake za zamani juu ya kaka zake, akawaambia: “Ninyi ni wapelelezi. Mumekuja kupeleleza uzaifu wa inchi yetu.” 10 Wao wakamujibu: “Sivyo, bwana wetu. Sisi watumishi wako tumekuja kununua chakula. 11 Sisi ni ndugu, wana wa baba mumoja. Sisi ni watu waaminifu, wala si wapelelezi.” 12 Lakini Yosefu akawaambia: “Sivyo! Mumekuja hapa kwa kupeleleza uzaifu wa inchi yetu.” 13 Wakamwambia: “Sisi, watumishi wako, tuko wandugu kumi na wawili, wana wa mutu mumoja, mwenyeji wa inchi ya Kanana. Mudogo wetu amebaki na baba kwa nyumba na ndugu yetu mwingine ni marehemu.” 14 Lakini Yosefu akawaambia: “Ni kama vile nilivyosema: ninyi ni wapelelezi tu. 15 Hivi ndivyo mutakavyojaribiwa: Ninaapa kwa jina la mufalme wa Misri, kwamba hamutatoka hapa mpaka mudogo wenu atakapokuja. 16 Mutume mumoja wenu amulete yule ndugu yenu mudogo, wakati wengine wenu wanamungoja katika kifungo. Kwa hiyo ukweli wa maneno yenu utajulikana. Kama sivyo, ninaapa kwa jina la mufalme wa Misri kwamba ninyi ni wapelelezi.” 17 Kisha akawatia wote katika kifungo kwa muda wa siku tatu. 18 Siku ya tatu Yosefu akawaambia: “Kwa sababu ninamwogopa Mungu, mufanye hivi kusudi mupate kuishi: 19 kama kweli ninyi ni watu waaminifu, mumoja wenu abaki katika kifungo na wengine wapeleke ngano kwa jamaa zenu wenye njaa. 20 Kisha mumulete kwangu ndugu yenu mudogo. Hii itahakikisha ukweli wa maneno yenu, nanyi hamutauawa.” Basi, wakakubali kufanya hivyo. 21 Kisha wakasemezana wao kwa wao: “Kweli sisi tulimukosea ndugu yetu. Ingawa tulimwona katika taabu, hatukumujali hata alipotusihi. Ndiyo maana taabu hii yote inatupata.” 22 Rubeni akawaambia: “Si niliwaambia tusimuzuru kijana? Lakini ninyi hamukunisikiliza! Sasa tunaazibiwa kwa ajili ya damu yake.” 23 Wao hawakujua kwamba Yosefu alielewa yote yale waliyosema, maana alipoongea nao ilikuwa kwa njia ya mutafsiri. 24 Yosefu akakwenda pembeni, akaanza kulia. Alipotulia, akarudi kuzungumuza nao. Kisha akamukamata Simeoni na kumufunga mbele ya macho yao. Wandugu za Yosefu wanarudi kwao 25 Yosefu akatoa amri wajaze mifuko yao na ngano na kumurudishia kila mumoja feza yake katika mufuko wake, na kuwapa chakula cha njia. Wakafanyiwa mambo hayo yote. 26 Wakabebesha punda wao mizigo yao ya ngano, wakaondoka. 27 Ikakuwa walipofika pahali pa kulala wageni kwa njia, mumoja wao akafungua mufuko wake kusudi apate kumukulisha punda wake, akashangaa kukuta feza yake kwenye kinywa cha mufuko wake. 28 Akawaambia wandugu zake: “Feza yangu imerudishwa. Ndio hii hapa kwenye kinywa cha mufuko wangu!” Waliposikia hayo, wakavunjika moyo. Wakaangalia wakiwa wanatetemeka na kuulizana: “Ni jambo gani hili Mungu alilotutendea?” 29 Walipofika katika inchi ya Kanana kwa baba yao Yakobo, wakamwelezea yote yaliyowapata, wakamwambia: 30 “Mukubwa wa inchi ile alisema nasi kwa ukali, na kutuona kwamba sisi ni wapelelezi katika inchi yake. 31 Lakini sisi tukamwelezea kwamba sisi ni watu waaminifu na wala si wapelelezi. 32 Tukamwelezea kwamba sisi tuko wandugu kumi na wawili wa baba mumoja. Mumoja wetu ni marehemu na yule mudogo yuko kwetu katika inchi ya Kanana pamoja na baba yetu. 33 Halafu mukubwa wa inchi hiyo akatuambia: ‘Hivi ndivyo nitakavyotambua kwamba kweli ninyi ni watu waaminifu. Muniachie kwangu ndugu yenu mumoja, nanyi wengine mupeleke ngano kwa jamaa zenu wenye njaa. 34 Kisha muniletee yule ndugu yenu mudogo, na hapo nitajua kwamba ninyi si wapelelezi lakini ni watu waaminifu. Mukifanya hivyo nitamwacha huru ndugu yenu, nanyi mutaruhusiwa kufanya biashara katika inchi hii.’ ” 35 Walipokuwa wanamimina ngano kutoka mifuko yao, wakashangaa kuona kila mumoja wao amerudishiwa kifuko chake na feza ndani ya mufuko wake. Walipoona hayo, wote pamoja na baba yao, wakashikwa na hofu. 36 Baba yao Yakobo, akawaambia: “Munaniondolea watoto wangu! Yosefu hayuko, Simeoni hayuko, sasa munataka kumutwaa Benjamina. Hayo yote yanaanguka juu yangu!” 37 Hapo Rubeni akamwambia baba yake: “Nisipomurudisha Benjamina, uwaue wana wangu wawili. Muache Benjamina katika mikono yangu, nami nitamulinda na kumurudisha kwako.” 38 Lakini baba yake akamujibu: “Mwana wangu hatakwenda nanyi. Ndugu yake amekwisha kufa, naye peke yake ndiye aliyebaki. Mimi ni muzee mwenye imvi. Ikiwa kijana huyu atapatwa na hasara yoyote katika safari mutakayofanya basi, mutaniua kwa huzuni.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo