Mwanzo 40 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yosefu anatafsiri ndoto 1 Wakati fulani nyuma ya mambo hayo, wakubwa wawili waliomutumikia mufalme wa Misri wakamukosea. Wakubwa wale walikuwa mutunza vinywaji mukubwa na mupishi mukubwa wa mukate wa mufalme. 2 Mufalme wa Misri akawakasirikia wale wakubwa wake wawili, 3 akawafungia ndani ya nyumba ya mukubwa wa waaskari walinzi, katika kifungo, pahali Yosefu alipofungwa. 4 Mukubwa wa waaskari walinzi akachagua Yosefu awatumikie. Nao wakakuwa katika kifungo kwa muda fulani. 5 Basi, usiku mumoja, yule mutunza vinywaji mukubwa na yule mupishi mukubwa wa mukate wa mufalme, waliota ndoto mule ndani ya gereza, kila mumoja na ndoto yake tofauti. 6 Yosefu alipokwenda kwao asubui na kuwaona, wote wawili walikuwa wenye wasiwasi. 7 Basi, Yosefu akawauliza wakubwa wale wa mufalme waliokuwa katika kifungo pamoja naye katika nyumba ya bwana wake: “Mbona leo muko na nyuso za huzuni?” 8 Wakamujibu: “Tuna huzuni kwa sababu tumeota ndoto na hakuna anayeweza kututafsiria ndoto zetu.” Yosefu akawaambia: “Kutafsiri ndoto si kazi ya Mungu? Basi, muniambie ndoto zenu.” 9 Mutunza vinywaji mukubwa wa mufalme akamwelezea Yosefu ndoto yake, akisema: “Katika ndoto yangu niliona muzabibu mbele yangu, 10 nao ulikuwa na matawi matatu. Mara tu ulipoanza kuchipuka majani, maua yake yakachanua na vishada vyake vikakuwa zabibu zenye kukomaa. 11 Katika mikono yangu nilikuwa na kikombe cha mufalme, basi, nikatwaa zabibu, nikazikamua katika kikombe kile, nikamupa mufalme.” 12 Yosefu akamwambia yule mutumishi: “Tafsiri ya ndoto yako ni hii: yale matawi matatu ni siku tatu. 13 Nyuma ya siku tatu mufalme atakunyanyua kutoka katika kifungo na kukurudisha tena katika cheo chako. Utaweza tena kumupa mufalme kikombe kwa mukono kama ulivyokuwa unafanya pale mbele. 14 Lakini tafazali usinisahau wakati mambo yatakapokuendea wewe vizuri. Unitendee mema na kusema juu yangu mbele ya mufalme, nipate kutoka humu katika kifungo. 15 Maana mimi nilitoroshwa kutoka inchi ya Waebrania na hapa Misri sijafanya kitu chochote kinachostahili nitiwe katika kifungo.” 16 Yule mupishi mukubwa wa mikate alipoona kwamba maelezo yale ni mazuri, akamwambia Yosefu: “Hata mimi niliota ndoto! Katika ndoto yangu nilikuwa nikibeba juu ya kichwa vitunga vitatu vya mikate. 17 Katika kitunga cha juu, kulikuwa aina mbalimbali za mikate kwa ajili ya mufalme. Lakini, ndege walikuwa wakikula kutoka kitunga kile juu ya kichwa changu!” 18 Yosefu akamwambia: “Tafsiri ya ndoto yako ni hii: vile vitunga tatu ni siku tatu. 19 Nyuma ya siku tatu mufalme atakunyanyua kutoka katika kifungo, atainua kichwa chako kusudi akutundike juu ya muti, nao ndege watakula mwili wako.” 20 Ilipotimia siku ya tatu, ambayo ilikuwa siku ya kufanya sikukuu ya kuzaliwa kwake, mufalme wa Misri akafanyia watumishi wake wote karamu. Akatoa katika kifungo mutunza vinywaji wake mukubwa na mupishi mukubwa wa mikate, akawaweka mbele ya wakubwa wake. 21 Kisha akamurudishia mutunza vinywaji cheo chake, apate kumupatia kikombe. 22 Lakini yule mupishi mukubwa wa mikate akamutundika juu ya muti, kama vile Yosefu alivyokuwa amewaelezea ndoto zao. 23 Hata hivyo, yule mutunza vinywaji mukubwa akamusahau Yosefu, pahali pa kumukumbuka. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo