Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mwanzo 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kaina na Abeli

1 Adamu akalala na muke wake Eva, naye akapata mimba, akazaa Kaina. Eva akasema: “Nimepata mutoto mwanaume kwa musaada wa Yawe!”

2 Kisha akazaa ndugu yake Abeli. Abeli alikuwa mufugaji wa kondoo na Kaina alikuwa mulimaji.

3 Nyuma ya muda fulani, Kaina akamutolea Yawe sadaka kutoka mazao ya shamba,

4 naye Abeli akamutolea Mungu sadaka ya wazao wa kwanza wa kondoo wake na nyama nono. Yawe akapendezwa na Abeli pamoja na sadaka yake,

5 lakini hakupendezwa na Kaina wala na sadaka yake. Basi, Kaina akakasirika sana na uso wake ukakunjamana.

6 Yawe akamwambia Kaina: “Kwa nini umekasirika, na kwa nini uso wako umekunjamana?

7 Ukitenda vyema hautakubaliwa? Na usipotenda vyema, basi, zambi inajificha kwa mulango; inakutamani, lakini unapaswa kuishinda.”

8 Kisha Kaina akasemezana na ndugu yake Abeli. Basi, walipokuwa katika shamba, Kaina akamushambulia ndugu yake Abeli, akamwua.

9 Yawe akamwuliza Kaina: “Ndugu yako Abeli yuko wapi?” Kaina akamujibu: “Mimi sijui! Mimi ni mulinzi wa ndugu yangu?”

10 Yawe akasema: “Umefanya nini? Damu ya ndugu yako inanililia kutoka katika udongo.

11 Sasa wewe unalaaniwa juu ya udongo ambao ulifungua kinywa kwa kupokea damu ya ndugu yako uliyemwua.

12 Unapolima udongo, hautakupatia tena mazao yake. Utakuwa mukimbizi na mwenye kutangatanga katika dunia.”

13 Kaina akamwambia Yawe: “Azabu yangu ni kubwa sana. Siwezi kuivumilia.

14 Angalia, leo umenifukuza kutoka udongo wenye mboleo na mbali nawe. Basi, nitakuwa mukimbizi na mwenye kutangatanga katika dunia, na yeyote atakayeniona ataniua.”

15 Lakini Yawe akamujibu: “Hapana, sivyo! Atakayekuua wewe Kaina atalipizwa mara saba.” Basi, Yawe akamutia Kaina kitambulisho hata yeyote atakayemwona asimwue.

16 Kisha Kaina akaondoka mbele ya Yawe, akaenda kuishi katika inchi ya Nodi, upande wa mashariki wa Edeni.

17 Kaina akalala na muke wake, naye muke wake akapata mimba, akazaa Enoki. Kaina akajenga muji akauita kwa jina la mwana wake Enoki.

18 Enoki akazaa Iradi, naye Iradi akazaa Mehuyaeli, naye Mehuyaeli akazaa Metusaeli, naye Metusaeli akazaa Lameki.

19 Lameki akaoa wanawake wawili, mumoja aliitwa Ada na mwingine Sila.

20 Ada akazaa Yabali ambaye alikuwa baba ya wafugaji wanaoishi katika mahema.

21 Ndugu yake alikuwa Yubali; huyo alikuwa baba ya wapiga muziki wote wanaopiga zeze na filimbi.

22 Naye Sila akazaa Tubali-Kaina, ambaye alikuwa mufuaji wa vyombo vyote vya shaba na chuma. Dada ya Tubali-Kaina alikuwa Nama.

23 Lameki akawaambia wake zake: “Ada na Sila musikie sauti yangu! Musikilize maneno ninayosema enyi wake za Lameki. Maana niliua mutu kwa sababu ya kunipiga, nilimwua kijana kwa kuniumiza.

24 Ikiwa Kaina atalipizwa mara saba, kweli Lameki atalipizwa mara makumi saba na saba.”


Seti na Enosi

25 Adamu akalala tena na Eva muke wake, naye akazaa mutoto mwanaume, akamwita Seti akisema: “Mungu amenijalia mutoto pahali pa Abeli aliyeuawa na Kaina.”

26 Seti naye akapata mutoto mwanaume, akamwita Enosi. Hapo ndipo watu walipoanza kumwomba Yawe kwa jina lake.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan