Mwanzo 39 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Muke wa Potifari na Yosefu 1 Basi, Yosefu aliposhushwa kwenda mpaka Misri, Mumisri mumoja anayeitwa Potifari ambaye alikuwa jemadari wa mufalme wa Misri na mukubwa wa waaskari walinzi, akamununua kutoka kwa Waisimaeli waliomuleta Misri. 2 Yawe alikuwa pamoja na Yosefu, akamufanikisha sana. Yosefu akakuwa anakaa katika nyumba ya bwana wake Mumisri. 3 Yule bwana wake akatambua kwamba Yawe alikuwa pamoja na Yosefu, na kwamba ndiye aliyefanikisha mambo yote Yosefu aliyofanya. 4 Basi, Yosefu akapata kukubaliwa mbele ya Potifari, hata akakuwa mutumishi wake wa pekee. Akamufanya musimamizi wa nyumba yake na mwangalizi wa mali yake yote. 5 Tokea wakati Potifari alipomufanya Yosefu kuwa musimamizi wa nyumba yake na mwangalizi wa mali yake, Yawe akabariki nyumba ya yule Mumisri kwa ajili ya Yosefu. Baraka za Yawe zikakuwa juu ya kila kitu alichokuwa nacho, ndani ya nyumba na katika shamba. 6 Kwa sababu hiyo Potifari alimupa Yosefu mamlaka juu ya mambo yake yote, naye Potifari akaacha kushugulika na chochote isipokuwa tu chakula chake mwenyewe. Yosefu alikuwa kijana muzuri na wa kupendeza. 7 Basi, nyuma ya muda fulani, muke wa Potifari akamutamani Yosefu na kumwambia: “Lala na mimi”. 8 Lakini Yosefu akakataa na kumwambia yule muke wa bwana wake: “Sikiliza! Bwana wangu amenipa mamlaka juu ya kila kitu hapa ndani ya nyumba na hajishugulishi na kitu chochote tena. 9 Hapa ndani ya nyumba yeye hana madaraka kuliko mimi. Yeye hakunikataza kushika chochote isipokuwa wewe tu kwa sababu wewe ni muke wake. Nitaweza namna gani basi kufanya uovu mubaya kama ule na kumukosea Mungu?” 10 Yule mwanamuke akaendelea kumushawishi Yosefu siku kwa siku, lakini Yosefu hakumusikiliza wala kukubali kulala naye. 11 Siku moja, Yosefu akaingia ndani ya nyumba kufanya kazi yake kama kawaida, na watumishi wengine hawakukuwa ndani ya nyumba. 12 Basi, muke wa Potifari akamushika nguo yake na kumwambia: “Lala na mimi!” Lakini Yosefu akamwachia nguo yake katika mikono yake, akakimbilia inje. 13 Kwa hiyo, yule mwanamuke alipoona kwamba Yosefu ameacha nguo yake katika mikono yake na kukimbilia inje, 14 akaita watumishi wa nyumba yake na kuwaambia: “Huyu Mwebrania tuliyeletewa anatuzarau. Alikuja kwangu akitaka kunishika kwa nguvu, lakini nikapiga kelele. 15 Aliposikia ninapiga kelele, akaacha nguo yake, akakimbilia inje!” 16 Basi, yule mwanamuke akaweka nguo ile mpaka wakati mume wake aliporudi ndani ya nyumba. 17 Akamwelezea jambo lile akisema: “Huyu mutumishi Mwebrania uliyemuleta kwetu alinifikia kwa kunizarau. 18 Lakini mara tu nilipopiga kelele, akaacha nguo yake na kukimbilia inje.” 19 Basi, bwana wa Yosefu aliposikia maneno ya muke wake, kwamba ndivyo mutumishi wake alivyomutendea, akawaka hasira. 20 Akamutwaa Yosefu na kumutia katika kifungo, pahali wafungwa wa mufalme walipokuwa. Lakini hata mule katika kifungo, 21 Yawe alikuwa pamoja na Yosefu na kumutendea mema, hata kumufanya apate kukubaliwa mbele ya mukubwa wa kifungo. 22 Hivyo mukubwa wa kifungo akamuweka Yosefu akuwe mukubwa wa wafungwa wote mule katika kifungo. Kila kitu kilichofanyika mule kilifanywa kwa mamlaka yake. 23 Yule mukubwa wa kifungo hakujishugulisha tena na kitu chochote Yosefu alichopewa kwa maana Yawe alikuwa pamoja na Yosefu na kufanikisha kila kitu alichofanya. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo