Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mwanzo 34 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Simeoni na Lawi wanalipiza kisasi kwa ajili ya dada yao

1 Siku moja Dina, binti ya Yakobo na Lea, akakwenda kuwatembelea wanawake wa inchi hiyo.

2 Basi, Sekemu mwana wa Hamori Muhivi, aliyekuwa mukubwa wa inchi hiyo, alipomwona Dina, akamushika, akalala naye kwa nguvu.

3 Lakini Sekemu akavutiwa sana na yule binti, akamupenda hata akaanza kumubembeleza.

4 Kwa hiyo, Sekemu akazungumuza na Hamori baba yake, akamwambia: “Unitwalie binti huyo kuwa muke wangu.”

5 Yakobo akapata habari kwamba Sekemu amemuchafua binti yake Dina; lakini kwa sababu wana wake walikuwa pamoja na nyama kwenye malisho, akanyamaza mpaka waliporudi.

6 Hamori, baba ya Sekemu, akakwenda kwa Yakobo kusudi azungumuze naye,

7 na wakati uleule wana wa Yakobo walirudi kwa nyumba kutoka kwenye malisho. Waliposikia hayo, vijana wale wakaona uchungu mwingi na kukasirika sana, kwa vile Sekemu alikuwa amewafanyia watu wa Israeli ovu hilo la kulala na binti ya Yakobo; maana jambo hilo halipaswi kutendwa.

8 Lakini Hamori akawaambia: “Mwana wangu Sekemu anamupenda sana binti yenu. Basi, tafazali mumuruhusu amwoe.

9 Muache tuoeane: ninyi mutuoeshee wabinti zenu, nanyi muoe wabinti zetu.

10 Kwa hiyo mutaishi pamoja nasi; mutakuwa huru katika inchi hii. Mutaishi humu, mufanye biashara na kujipatia mali.”

11 Vilevile, Sekemu akawaambia baba na wandugu za Dina: “Ninataka kukubaliwa mbele yenu, nami nitawapa ninyi chochote mutakachosema.

12 Muniombe mali na zawadi, hata ikiwa kikubwa namna gani, nami nitatoa, kufuatana na jinsi mutakavyoniambia. Lakini munipatie tu binti huyu kuwa muke wangu.”

13 Basi, wana wa Yakobo wakamujibu Sekemu na baba yake Hamori kwa udanganyifu, kwa sababu Sekemu alikuwa amekwisha kumuchafua dada yao Dina.

14 Wakawaambia: “Hatuwezi kumwoesha dada yetu kwa mutu asiyetahiriwa. Kufanya hivyo ni haya kwetu.

15 Tutakubaliana nanyi tu kwa sharti hili: kwamba mutakuwa kama sisi kwa kumutahiri kila mwanaume kati yenu.

16 Kwa hiyo tutawaoeshea wabinti zetu na kuwaoa wabinti zenu. Tutaishi pamoja nanyi na kuwa jamaa moja.

17 Lakini musipokubaliana nasi na kutahiriwa, basi, sisi tutamutwaa binti yetu na kujiendea yetu.”

18 Pendekezo lao likapendeza Hamori na mwana wake Sekemu.

19 Kijana yule hakusita hata kidogo kutimiza sharti hilo, kwa vile alivyomupenda binti ya Yakobo, ingawa ni yeye ndiye aliyeheshimika kuliko wote katika nyumba yao.

20 Basi, Hamori na mwana wake Sekemu, wakakwenda kwenye mulango wa muji, pahali pa mikutano, wakaongea na watu wao wakisema:

21 “Watu hawa ni warafiki zetu. Tuwakaribishe waishi katika inchi yetu na kufanya biashara, kwa sababu tuko na inchi ya kututosha sisi na wao vilevile; kisha tutaoa wabinti zao na kuwaoshea binti wetu.

22 Lakini wao watakubali kuishi nasi na tutakuwa jamaa moja kwa sharti hili: kwamba tutamutahiri kila mwanaume kati yetu kama vile wao walivyotahiriwa.

23 Hamuoni kwamba nyama wao wa kufugwa na mali yao yote itakuwa mali yetu? Basi, tukubaliane nao kusudi wakae pamoja nasi.”

24 Wanaume wote waliokusanyika kwenye mulango wa muji ule wakakubaliana na Hamori na mwana wake Sekemu. Kisha, wanaume wote wakatahiriwa.

25 Kisha siku tatu, waliotahiriwa wakiwa wangali na maumivu makali, wana wawili wa Yakobo, Simeoni na Lawi, kaka za Dina, wakatwaa panga zao, wakashambulia muji kwa rafla na kuwaua wanaume wote.

26 Wakawaua kwa upanga Hamori na mwana wake Sekemu, wakamutoa Dina katika nyumba ya Sekemu, wakajiendea.

27 Nyuma ya mauaji hayo, wana wengine wa Yakobo wakaingia katika muji na kunyanganya mali yote katika muji ule, kwa sababu dada yao alikuwa amechafuliwa.

28 Walitwaa kondoo na mbuzi, ngombe, punda na chochote kilichokuwa katika muji au katika shamba.

29 Walitwaa mali yote, watoto na wanawake wote na chochote kilichokuwa ndani ya nyumba zao.

30 Basi, Yakobo akamwambia Simeoni na Lawi: “Ninyi mumeniletea taabu kwa kunifanya nichukiwe na wakaaji wa inchi hii ya Wakanana na Waperizi. Mimi sina watu wengi, na kama wakikusanyika kwa kunishambulia wataniangamiza mimi pamoja na jamaa yangu.”

31 Hao wandugu wawili wakajibu: “Ana haki gani ya kumutendea dada yetu kama kahaba?”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan