Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mwanzo 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Uasi wa mwanadamu

1 Nyoka alikuwa mwerevu kuliko nyama wote wa pori walioumbwa na Yawe Mungu. Basi, nyoka akamwambia yule mwanamuke: “Ni kweli Mungu alisema musikule matunda ya muti wowote katika bustani?”

2 Mwanamuke akamujibu yule nyoka: “Tunaweza kula matunda ya miti katika bustani

3 lakini Mungu alisema: ‘Musikule matunda ya muti unaokuwa katikati ya bustani, wala musiuguse. Kama sivyo, mutakufa.’ ”

4 Nyoka akamwambia mwanamuke: “Hamutakufa!

5 Mungu alisema hivyo kwa sababu anajua kwamba mukikula matunda ya muti ule mutafumbuliwa macho, nanyi mutakuwa kama Mungu, mukijua mazuri na mabaya.”

6 Basi, mwanamuke alipoona kwamba muti ule ni muzuri kwa chakula, unavutia macho, na kwamba unafaa kwa kupata hekima, akachuma tunda lake, akakula, akamupa mume wake aliyekuwa pamoja naye, naye vilevile akakula.

7 Mara moja macho yao yakafumbuliwa, wakatambua kwamba wako uchi. Kwa hiyo wakashona majani ya muti wa tini, wakajifanyia nguo.

8 Magaribi mwanaume na muke wake wakasikia Yawe Mungu akitembea katika bustani, nao wakajificha kati ya miti ya bustani, Yawe Mungu asipate kuwaona.

9 Lakini Yawe Mungu akamwita yule mwanaume: “Uko wapi?”

10 Naye akamujibu: “Nilisikia sauti yako katika bustani, nikaogopa maana nilikuwa uchi. Nikajificha.”

11 Yawe akamwuliza: “Nani aliyekuambia kwamba uko uchi? Umekula tunda la muti nililokuamuru usikule?”

12 Yule mwanaume akajibu: “Mwanamuke uliyenipa akae pamoja nami ndiye aliyenipa tunda la muti ule, nami nikakula.”

13 Yawe Mungu akamwuliza yule mwanamuke: “Umefanya nini wewe?” Mwanamuke akamujibu: “Nyoka alinidanganya, nami nikakula.”


Azabu

14 Kisha Yawe akamwambia nyoka: “Kwa sababu umefanya hivyo, umelaaniwa kuliko nyama wote wa kufugwa, na kuliko nyama wote wa pori. Utatambaa kwa tumbo lako na kula mavumbi siku zote za maisha yako.

15 Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamuke, kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye ataponda kichwa chako, nawe utamwuma kisigino chake.”

16 Kisha akamwambia mwanamuke: “Nitakuzidishia uchungu wa kuzaa, Utazaa watoto kwa uchungu. Utakuwa na hamu na mume wako, naye atakutawala.”

17 Kisha akamwambia yule mwanaume: “Wewe umemusikiliza muke wako na kula matunda ya muti ambayo nilikuamuru usikule. Basi, udongo umelaaniwa kwa sababu yako. Kwa jasho utajipatia toka humo chakula chako, siku zote za maisha yako.

18 Udongo utakuzalia miiba na magugu, nawe utakula majani ya shamba.

19 Kwa jasho la uso wako utajipatia chakula, mpaka utakaporudi katika udongo, maana ulitwaliwa katika udongo. Wewe ni mavumbi na utarudi katika mavumbi.”

20 Adamu akamupa muke wake jina “Eva”, maana alikuwa mama wa wanadamu wote.

21 Yawe Mungu akawatengenezea Adamu na muke wake nguo za ngozi, akawavalisha.


Adamu na Eva wanafukuzwa katika bustani

22 Kisha Yawe Mungu akasema: “Sasa, mwanadamu amekuwa kama mumoja wetu, anajua mazuri na mabaya. Inafaa kumuzuia kula lile tunda la muti wa uzima, maana akilikula ataishi milele.”

23 Basi, Yawe Mungu akamufukuza Adamu inje ya bustani ya Edeni, kusudi alime udongo ambamo alitwaliwa.

24 Alimufukuza inje. Akaweka makerubi upande wa mashariki wa bustani ya Edeni wakiwa na upanga wa moto uliogeuka huku na kule, kwa kulinda njia inayokwenda kwenye muti wa uzima.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan