Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mwanzo 28 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Hivyo Isaka akamwita Yakobo, akamubariki, akamwagiza akisema: “Usioe mwanamuke yeyote Mukanana.

2 Kwenda Padani-Aramu, kwa nyumba ya babu yako Betueli, uoe mumoja kati ya wabinti za mujomba wako Labani.

3 Mungu Mwenye Nguvu akubariki upate wazao wengi na kuongezeka, kusudi ukuwe jamii kubwa ya watu.

4 Akubariki wewe pamoja na wazao wako kama alivyomubariki Abrahamu, upate kurizi inchi ambamo unakaa kama mugeni, inchi ambayo Mungu alimupa Abrahamu!”

5 Basi, Isaka akamutuma Yakobo, naye akakwenda Padani-Aramu kwa Labani, mwana wa Betueli wa Aramu, kaka ya Rebeka, mama ya Yakobo na Esau.


Esau anaoa muke wa tatu

6 Esau akatambua kwamba Isaka alibariki Yakobo na kumutuma aende kuoa kule Padani-Aramu, na kwamba alipomubariki, alimukataza asioe mwanamuke Mukanana.

7 Akatambua vilevile kwamba Yakobo alimutii mama yake na baba yake, akakwenda Padani-Aramu.

8 Basi, Esau akafahamu kwamba baba yake hapendezwi na wanawake wa Kanana.

9 Hivyo, Esau akakwenda kwa Isimaeli, mwana wa Abrahamu, akaoa Mahalati binti ya Isimaeli, dada ya Nebayoti.


Ndoto ya Yakobo kule Beteli

10 Yakobo aliondoka Beri-Seba, akaelekea Harani.

11 Alipofika pahali fulani, akalala pale kwa sababu jua lilikuwa limetua. Akatwaa jiwe moja la pahali pale, akaliweka chini ya kichwa chake, akalala.

12 Akaota ndoto, na katika ndoto hiyo, aliona ngazi iliyosimamishwa juu ya dunia na incha yake inafika mbinguni. Wamalaika wa Mungu walikuwa wakipanda na kushuka katika ngazi hiyo.

13 Yawe alisimama juu ya ngazi hiyo, akamwambia: “Mimi ni Yawe, Mungu wa Abrahamu baba yako, na Mungu wa Isaka. Nitakupa inchi unayoilalia wewe na wazao wako.

14 Wazao wako watakuwa wengi kama mavumbi ya dunia, na urizi wao utaenea kila pahali: upande wa magaribi, mashariki, kaskazini na kusini. Kwa njia yako na ya wazao wako, jamaa zote katika dunia zitabarikiwa.

15 Mimi niko pamoja nawe, nitakulinda popote utakapoenda na kukurudisha katika inchi hii. Sitakuacha mpaka nitakapotimiza ahadi niliyokupa.”

16 Kisha Yakobo akaamuka toka usingizi, akasema: “Hakika, Yawe yuko pahali hapa, nami sikujua!”

17 Yakobo akaogopa na kusema: “Pahali hapa panatisha sana! Bila shaka hapa ni nyumba ya Mungu na mulango wa mbinguni.”

18 Yakobo akaamuka asubui mapema, akatwaa lile jiwe alilokuwa ameliweka chini ya kichwa chake, akalisimika kama nguzo na kulitakasa kwa kulimiminia mafuta.

19 Akaita pahali hapo Beteli, ni kusema “Nyumba ya Mungu”. Jina la mbele la muji ule lilikuwa Luzi.

20 Kisha Yakobo akafanya kiapo akisema: “Ikiwa, ee Mungu, utakuwa pamoja nami na kunilinda katika safari yangu, ukinipa chakula na nguo

21 kusudi nirudi katika nyumba ya baba yangu salama, basi, wewe Yawe utakuwa ndiwe Mungu wangu.

22 Nalo jiwe hili nililosimika hapa kama nguzo, litakuwa nyumba yako Mungu, nami nitakupa sehemu ya kumi ya vitu vyote utakavyonipa.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan