Mwanzo 26 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Isaka anahamia Gerari 1 Kisha kukatokea njaa katika inchi ile, nyuma ya ile ya kwanza iliyokuwa kwa wakati wa Abrahamu. Isaka akakwenda Gerari kwa Abimeleki mufalme wa Wafilistini. 2 Yawe akamutokea Isaka na kumwambia: “Usiende Misri, lakini ukae katika inchi nitakayokuambia. 3 Ukae katika inchi hiyo, nami nitakuwa pamoja nawe na kukubariki. Nitatimiza ahadi niliyomupa baba yako Abrahamu, maana nitakupa wewe na wazao wako inchi hizi zote. 4 Nitawazidisha wazao wako wakuwe kama nyota za mbinguni na kuwapa inchi hizi zote. Kutokana na wazao wako, mataifa yote katika dunia yatabarikiwa, 5 kwa sababu Abrahamu alinitii mimi, akashika maagizo yangu, amri zangu, masharti yangu na sheria zangu.” 6 Basi, Isaka akakaa kule Gerari. 7 Watu wa kule walipomwuliza juu ya muke wake, akajibu: “Huyu ni dada yangu.” Aliogopa kusema kwamba ni muke wake kwa kuogopa kwamba wakaaji wa inchi wangemwua kwa sababu ya Rebeka, maana Rebeka alikuwa muzuri sana. 8 Nyuma ya kukaa kule kwa muda murefu, Abimeleki mufalme wa Wafilistini akachungulia kwenye dirisha akamwona Isaka akimukumbatia muke wake Rebeka. 9 Abimeleki akamwita Isaka na kumwambia: “Hakika huyo ni muke wako! Sababu gani ulisema kwamba ni dada yako?” Isaka akajibu: “Kwa sababu niliogopa kwamba ningeuawa kwa sababu yake.” 10 Abimeleki akamwuliza: “Ni jambo gani hili ulilotutendea? Mumoja wa watu wangu angaliweza kulala na muke wako bila wasiwasi, nawe ungekuwa umeleta kosa juu yetu.” 11 Halafu Abimeleki akawaonya watu wote akisema: “Yeyote atakayemugusa mutu huyu au muke wake, atauawa.” 12 Mwaka ule Isaka akapanda mbegu katika inchi ile, akavuna mara mia zaidi, maana Yawe alimubariki, 13 naye akatajirika. Alizidi kupata mali mpaka akakuwa tajiri sana. 14 Alikuwa na makundi ya kondoo, ngombe na watumwa wengi. Kwa hiyo, Wafilistini wakamwonea wivu. 15 Wakaziba visima vyote vya maji ambavyo watumishi wa baba yake Abrahamu walikuwa wamechimba wakati alipokuwa muzima. 16 Halafu Abimeleki akamwambia Isaka: “Ondoka kwetu, maana wewe umetuzidi nguvu.” 17 Basi, Isaka akaondoka kule, akapiga kambi yake katika bonde la Gerari, akakaa kule. 18 Isaka akachimba vile visima vilivyokuwa vimechimbwa wakati Abrahamu baba yake alipokuwa muzima, visima ambavyo Wafilistini walikuwa wameziba nyuma ya kifo cha Abrahamu. Akavipa majina yaleyale baba yake aliyovipa. 19 Lakini watumishi wa Isaka walipochimba katika lile bonde na kupata kisima cha maji yanayobubujika, 20 wachungaji wa pale Gerari wakagombana na wachungaji wa Isaka wakisema: “Maji haya ni yetu.” Hivyo Isaka akakiita kisima hicho “Ugomvi” kwa sababu waligombana naye. 21 Halafu wakachimba kisima kingine, nacho vilevile wakakigombania; hivyo Isaka akakiita kisima hicho “Fitina”. 22 Kisha Isaka akakwenda pahali pengine na kuchimba kisima kingine. Lakini hicho hawakukigombania. Hivyo Isaka akakiita “Nafasi Pana”, akisema: “Sasa Yawe ametuachia nafasi, nasi tutastawi katika inchi hii.” 23 Kutoka kule, Isaka alikwenda Beri-Seba. 24 Usiku uleule Yawe alimutokea na kumwambia: “Mimi ni Mungu wa baba yako Abrahamu. Usiogope; niko pamoja nawe. Nitakubariki na kuwazidisha wazao wako kwa ajili ya Abrahamu, mutumishi wangu.” 25 Kwa hiyo, Isaka akajenga mazabahu kule na kumwabudu Yawe. Akapiga kambi kule, na watumishi wake wakachimba kisima. Isaka na Abimeleki wanapatana 26 Abimeleki alitoka Gerari akiwa pamoja na Ahuzati, mushauri wake, na Fikoli, jemadari wa jeshi lake, akamwendea Isaka. 27 Isaka akawauliza: “Kwa nini mumekuja kwangu ijapokuwa munanichukia na mulinifukuza kwenu?” 28 Wao wakamujibu: “Tumeona wazi kwamba Yawe yuko pamoja nawe. Kwa hiyo, tunafikiri inafaa tufanye kiapo pamoja nawe na kufanya agano, 29 kwamba hautatuzuru, nasi vilevile hatutakuzuru. Tulikutendea tu vizuri, tukakuacha uende kwa amani, bila kukutendea ubaya wowote. Na sasa wewe ni mubarikiwa wa Yawe.” 30 Basi, Isaka akawafanyia karamu, nao wakakula na kunywa. 31 Kesho yake wakaamuka asubui mapema na kufanya kiapo. Kisha Isaka akawasindikiza na kuagana nao kwa amani. 32 Siku ileile watumishi wa Isaka walimufikia na kumupasha habari za kile kisima walichokuwa wamechimba, wakasema: “Tumepata maji!” 33 Basi, Isaka akakiita kisima hicho Siba, ni kusema “Kiapo”. Kwa hiyo jina la muji ule ni Beri-Seba hata leo. Wake za Esau 34 Esau alipokuwa na umri wa miaka makumi ine, akaoa wake wawili Wahiti: Yuditi binti ya Beri na Basemati binti ya Eloni. 35 Wanawake hao walifanya maisha ya Isaka na Rebeka kuwa machungu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo