Mwanzo 25 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wazao wengine wa Abrahamu ( 1 Sik 1.32-33 ) 1 Abrahamu akaoa muke mwingine, jina lake Ketura. 2 Ketura alimuzalia Abrahamu: Zimurani, Yokisani, Medani, Midiani, Isibaki na Sua. 3 Yokisani alizaa Seba na Dedani. Wazao wa Dedani walikuwa Waashuri, Waletusi na Waleumi. 4 Wana wa Midiani walikuwa Efa, Eferi, Hanoki, Abida na Elda. Wote hao walikuwa wazao wa Ketura. 5 Abrahamu akamurizisha Isaka mali yake yote. 6 Lakini akawapa wana wa habara zake zawadi. Na wakati alipokuwa bado muzima, akawapeleka katika inchi ya upande wa mashariki, mbali na mwana wake Isaka. Kifo cha Abrahamu 7 Abrahamu aliishi miaka mia moja makumi saba na mitano. 8 Kisha kuishi maisha marefu na ya fanaka, akakufa na kukutana na wazee wake. 9 Isaka na Isimaeli, wana wa Abrahamu, wakamuzika baba yao katika pango la Makipela, upande wa mashariki wa Mamure kwenye shamba lililokuwa la Efuroni mwana wa Sohari Muhiti. 10 Abrahamu alikuwa amenunua shamba lile kwa Wahiti. Kule ndiko Abrahamu na muke wake Sara walizikwa. 11 Nyuma ya kifo cha Abrahamu, Mungu alimubariki mwana wake Isaka. Naye Isaka akaishi karibu na kisima cha Beri-Lahai-Roi. Wazao wa Isimaeli ( 1 Sik 1.28-31 ) 12 Hawa ndio wazao wa Isimaeli mwana wa Abrahamu ambaye Hagari Mumisri aliyekuwa mujakazi wa Sara alimuzalia Abrahamu. 13 Haya ni majina yao kufuatana na kuzaliwa kwao: Nebayoti, muzaliwa wa kwanza, Kedari, Adibeli, Mibusamu, 14 Misima, Duma, Masa, 15 Hadadi, Tema, Yeturi, Nafisi na Kedema. 16 Hao ndio wana wa Isimaeli, waliokuwa shina ya makabila kumi na mawili. Makao na vijiji vyao vilijulikana kwa majina yao. 17 Isimaeli alikuwa na umri wa miaka mia moja makumi tatu na saba alipokufa na kukutana na wazee wake. 18 Wazao wa Isimaeli walikaa katika eneo lililokuwa kati ya Havila na Shuri, upande wa mashariki wa Misri, kuelekea Ashuri. Walikaa kwa utengano na wazao wengine wa Abrahamu. Kuzaliwa kwa Esau na Yakobo 19 Hawa ndio wazao wa Isaka mwana wa Abrahamu. 20 Isaka alipokuwa na umri wa miaka makumi ine akamwoa Rebeka, binti ya Betueli, Musuria wa Padani-Aramu. Rebeka alikuwa dada ya Labani. 21 Rebeka alikuwa tasa, kwa hiyo Isaka akamwomba Yawe. Naye Yawe akakubali ombi lake, Rebeka akapata mimba. 22 Mimba hiyo ilikuwa ya mapacha. Watoto hao waligongana ndani ya tumbo la Rebeka, naye akasema: “Kama hivi ndivyo mambo yanavyokuwa, kwa nini kuishi?” Basi, akakwenda kumwuliza Yawe. 23 Yawe akamwambia: “Mataifa mawili yako ndani ya tumbo lako; makabila mawili yatakayozaliwa nawe, yatatengana. Moja litakuwa lenye nguvu kuliko lingine, mukubwa atamutumikia mudogo.” 24 Siku zake za kuzaa zilipotimia, Rebeka akazaa mapacha. 25 Wa kwanza alikuwa mwekundu, mwenye nywele mwili wote; hivyo wakamwita Esau. 26 Wa pili alizaliwa akiwa amemushika Esau kisigino, hivyo wakamupa jina Yakobo. Isaka alikuwa na umri wa miaka makumi sita wakati Esau na Yakobo walipozaliwa. Esau anauzisha haki yake 27 Watoto hao wakakomaa. Esau alikuwa mwindaji hodari. Alipenda maisha ya pori. Yakobo alikuwa mutu mutulivu. Alipenda maisha ya nyumba. 28 Basi, Isaka akamupenda Esau kwa sababu alipenda kula nyama wa mawindo yake, lakini Rebeka akamupenda Yakobo. 29 Siku moja, Yakobo alipokuwa anapika muchuzi, Esau akarudi kwa nyumba kutoka katika mawindo akiwa na njaa sana. 30 Kwa hiyo Esau akamwambia Yakobo: “Ninasikia njaa. Tafazali, unigawanyie muchuzi huo mwekundu nikule.” Ndiyo maana walimupanga jina Edomu, maana yake “mwekundu”. 31 Yakobo akajibu: “Kwanza uniuzishie haki yako ya muzaliwa wa kwanza.” 32 Esau akasema: “Sawa! Niko karibu kufa. Haki yangu ya muzaliwa wa kwanza itanifaa nini?” 33 Yakobo akamwambia: “Uniapie kwanza.” Basi, Esau akamwapia na kumwuzishia Yakobo haki yake ya muzaliwa wa kwanza. 34 Halafu Yakobo akamupa Esau mukate na muchuzi wa manjegere. Esau akakula, akakunywa, kisha akaondoka, akajiendea. Hivi ndivyo Esau alivyoizarau haki yake ya muzaliwa wa kwanza. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo