Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mwanzo 24 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Isaka anaoa

1 Sasa Abrahamu alikuwa muzee wa miaka mingi, naye Yawe alikuwa amemubariki katika kila hali.

2 Siku moja Abrahamu akamwambia mutumishi wake aliyekuwa muzee kuliko wengine na musimamizi wa mali yake yote: “Weka mukono wako chini ya paja yangu,

3 nami nitakuapisha kwa jina la Yawe, Mungu wa mbingu na dunia, kwamba hautamwoea mwana wangu binti yeyote kati ya wabinti za Wakanana ninaoishi nao.

4 Uniapie kwamba utakwenda mpaka katika inchi yangu, kwa jamaa zangu, umutafutie mwana wangu Isaka muke.”

5 Mutumishi akamwambia: “Labda mwanamuke yule atakataa kunifuata kuja huku, ikiwa hivyo, ni lazima nimurudishe mwana wako katika inchi ulikotoka?”

6 Abrahamu akamwambia: “Hapana! Angalia sana usimurudishe mwana wangu kule.

7 Yawe, Mungu wa mbingu, aliyenitoa katika nyumba ya baba yangu na kutoka katika inchi nilimozaliwa, na ambaye alisema nami, aliniapia kwamba atawapa wazao wangu inchi hii. Yeye atamutuma malaika wake mbele yako kusudi umuletee mwana wangu muke kutoka kule.

8 Ikiwa mwanamuke yule hatapenda kukufuata mpaka huku, basi kiapo changu hakitakufunga, lakini kwa vyovyote vile usimurudishe mwana wangu kule.”

9 Basi, mutumishi yule akaweka mukono wake chini ya paja la Abrahamu, bwana wake, akaapa juu ya jambo hilo.

10 Kisha, yule mutumishi akatwaa ngamia kumi wa bwana wake akaondoka akiwa na zawadi nzuri za kila aina. Akasafiri kwenda katika muji Nahori alimokaa, katika inchi ya Mesopotamia.

11 Alipofika, alipigisha ngamia wake magoti kando ya kisima kilichokuwa inje ya muji. Ilikuwa magaribi wakati ambapo wanawake wanakwenda kwenye kisima kuteka maji.

12 Naye akaomba: “Ee Yawe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ninakuomba unisaidie leo na umutendee mema bwana wangu Abrahamu.

13 Niko hapa kando ya kisima ambapo wabinti za wenyeji wa muji wanakuja kuteka maji.

14 Basi, binti nitakayemwambia atue mutungi wake wa maji anipatie maji nikunywe, naye akinipa mimi na kuwakunywesha ngamia wangu, akuwe ndiye uliyemuchagulia mutumishi wako Isaka. Jambo hilo litanionyesha kwamba umemutendea mema bwana wangu.”

15 Mbele hajamaliza kuomba, mara moja Rebeka, binti ya Betueli mwana wa Milka, muke wa Nahori, ndugu ya Abrahamu, akafika akibeba mutungi wake kwenye bega.

16 Binti yule alikuwa na sura ya kuvutia sana na alikuwa angali bikira. Basi, akateremuka kwenye kisima, akaujaza mutungi wake maji na kupanda.

17 Halafu yule mutumishi akaharakisha kukutana naye, akamwambia: “Tafazali, unipatie maji ya kunywa kutoka mutungi wako.”

18 Binti akamujibu: “Kunywa, ee bwana wangu.” Na palepale akatua mutungi wake, akiushikilia kusudi amukunyweshe.

19 Alipokwisha kumupatia maji, akamwambia: “Nitatekea ngamia wako maji vilevile, wakunywe mpaka watosheke.”

20 Basi, akafanya haraka, akawamiminia ngamia maji ya mutungi wake katika birika, akakimbia kwenye kisima kuteka maji mengine na kuwakunywesha ngamia wake wote.

21 Yule mutu akakuwa anamwangalia kwa uangalifu bila kusema lolote, apate kufahamu kama Yawe amefanikisha safari yake au sivyo.

22 Ngamia walipotosheka kunywa maji, yule mutu akamupa yule binti pete ya zahabu yenye uzito wa yapata grama sita, na vikomo viwili vya zahabu za grama kumi kila moja.

23 Akamwuliza: “Uniambie tafazali, wewe ni binti ya nani? Kuna nafasi ya kulala katika nyumba ya baba yako?”

24 Rebeka akajibu: “Mimi ni binti ya Betueli mwana wa Milka, muke wa Nahori.

25 Kwetu kuna majani na malisho ya kutosha na pahali pa kulala kwa wageni.”

26 Halafu yule mutu akainamisha kichwa chake, akamwabudu Yawe

27 akisema: “Atukuzwe Yawe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ambaye hajasahau wema na uaminifu wake kwa bwana wangu. Yawe ameniongoza mimi mwenyewe moja kwa moja mpaka kwa jamaa ya bwana wangu!”

28 Kisha yule binti akakimbia kwenda kuwapa wandugu za mama yake habari.

29 Rebeka alikuwa na kaka yake anayeitwa Labani. Labani akatoka mbio kukutana na yule mutu kwenye kisima.

30 Labani alikuwa ameona ile pete na vikomo kwa mikono ya dada yake na kusikia mambo Rebeka aliyoambiwa na yule mutu. Labani akamukuta yule mutu akisimama karibu na ngamia wake kando ya kisima.

31 Labani akamwambia: “Karibu kwetu wewe uliyebarikiwa na Yawe. Mbona unasimama inje? Mimi mwenyewe nimekwisha tayarisha nyumba na pahali kwa ajili ya hawa ngamia wako!”

32 Basi, mutumishi yule wa Abrahamu akaingia ndani ya nyumba. Labani akafungua ngamia na kuwapatia majani, akamupa yeye na watu wake maji ya kunawa miguu.

33 Basi, wakamutayarishia chakula, lakini yeye akasema: “Sitakula mpaka niseme ninachotaka kusema.” Labani akamwambia: “Basi, sema.”

34 Yule mutu akasema: “Mimi ni mutumishi wa Abrahamu.

35 Yawe amemubariki sana bwana wangu, naye amekuwa mutu mukubwa. Amemupa makundi ya kondoo na nyama wengi, feza na zahabu, watumishi wanaume na wanawake, ngamia na punda!

36 Sara, muke wa bwana wangu katika uzee wake, alimuzalia bwana wangu mutoto; na bwana wangu amemupa yule mutoto mali yake yote.

37 Bwana wangu aliniapisha mimi akisema: ‘Hautamwoea mwana wangu binti yeyote kati ya wabinti za Wakanana ambao ninaishi katika inchi yao.

38 Lakini utakwenda mpaka katika inchi yangu, kwa jamaa zangu, kusudi umutafutie mwana wangu Isaka muke.’

39 Nami nikamwambia bwana wangu: ‘Labda mwanamuke yule atakataa kunifuata kuja huku.’

40 Lakini yeye akasema: ‘Yawe aliyeniongoza katika maisha yangu, atamutuma malaika wake aende pamoja nawe na kukufanikisha katika safari yako. Nawe utamutwalia mwana wangu muke kutoka kwa jamaa yangu na nyumba ya baba yangu.

41 Utakapofika kwa jamaa yangu, nao wasipokupa yule binti, basi, hautafungwa na kiapo changu.’

42 “Leo nilipofika kwenye kisima nikaomba: ‘Ee Yawe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ninakuomba unisaidie leo katika safari yangu na umutendee Abrahamu bwana wangu mema.

43 Niko hapa kando ya kisima. Binti atakayekuja kuteka maji ambaye nitamwomba anipatie maji kidogo ya kunywa kutoka mutungi wake,

44 naye akinipa na kuwatekea ngamia wangu maji, basi yule akuwe ndiye uliyemuchagua kuwa muke wa mwana wa bwana wangu.’

45 “Mbele sijamaliza kuomba ndani ya moyo wangu, mara tu Rebeka akafika na mutungi wake wa maji juu ya bega, akateremuka kwenye kisima na kuteka maji. Nami nikamwambia: ‘Tafazali unipe maji ya kunywa.’

46 Naye akatua mutungi wake haraka toka juu ya bega lake, akasema: ‘Basi, kunywa bwana wangu. Nitatekea ngamia wako maji vilevile.’ Basi, mimi nikakunywa naye akawapa ngamia wangu maji vilevile.

47 Halafu nilimwuliza: ‘Wewe ni binti ya nani?’ Akaniambia: ‘Mimi ni binti ya Betueli mwana wa Milka, muke wa Nahori.’ Halafu nikamupa pete na kumuvalisha vikomo kwa mikono.

48 Kisha nikainama na kumwabudu Yawe. Nikamutukuza Yawe, Mungu wa bwana wangu Abrahamu, ambaye ameniongoza moja kwa moja kwa binti wa ukoo wa bwana wangu kwa ajili ya mwana wake.

49 Sasa, basi, muniambie kama muko tayari kumutendea bwana wangu kwa wema na uaminifu. Kama sivyo, basi museme, nami nitajua cha kufanya.”

50 Kisha kusikia hayo, Labani na Betueli wakamujibu: “Jambo hili limetoka kwa Yawe, sisi hatuwezi kuamua lolote.

51 Rebeka huyu hapa. Umutwae uende. Akuwe muke wa mwana wa bwana wako kama vile Yawe alivyosema.”

52 Mutumishi wa Abrahamu aliposikia maneno hayo, akamwabudu Yawe.

53 Kisha akatoa vyombo vya feza na zahabu na nguo, akamupa Rebeka. Vilevile aliwapa wandugu na mama ya Rebeka mapambo ya bei kubwa.

54 Mutumishi wa Abrahamu na watu aliokuja nao wakakula, wakakunywa na kulala kule. Walipoamuka asubui, mutumishi yule akasema: “Ninaomba kurudi kwa bwana wangu.”

55 Lakini wandugu na mama ya Rebeka wakasema: “Umwache binti akae nasi muda mufupi, kama siku kumi hivi; kisha anaweza kwenda.”

56 Lakini yeye akasema: “Tafazali, musinicheleweshe, kwa sababu Yawe amekwisha kufanikisha katika safari yangu. Ninaomba muniruhusu kurudi kwa bwana wangu.”

57 Nao wakasema: “Basi, tumwite binti mwenyewe, tumwulize.”

58 Wakamwita Rebeka na kumwuliza: “Utakwenda na mutu huyu?” Naye akajibu: “Nitakwenda.”

59 Basi, wakamwacha Rebeka aende na mutumishi wa Abrahamu na watu wake. Mulezi wa Rebeka vilevile alikwenda naye.

60 Basi, wakamubariki Rebeka wakisema: “Ewe dada yetu! Ukuwe mama wa maelfu kwa maelfu; wazao wako warizi miji ya waadui zao.”

61 Kisha, Rebeka na wajakazi wake wakapanda juu ya ngamia na kumufuata yule mutumishi wa Abrahamu, nao wote wakaondoka.

62 Wakati ule, Isaka alikuwa ameondoka Beri-Lahai-Roi, akakaa pande za Negebu.

63 Siku moja magaribi, Isaka akakwenda kwenye mashamba kwa kufikiri. Basi, akainua macho akaona ngamia wanakuja.

64 Naye Rebeka alipoinua macho na kumwona Isaka, akashuka chini

65 na kumwuliza mutumishi wa Abrahamu: “Ni nani yule mutu anayetembea kule katika shamba, anakuja kutupokea?” Yule mutumishi akasema: “Ni bwana wangu.” Basi, Rebeka akatwaa kitambaa chake, akajifunika uso.

66 Yule mutumishi akamwelezea Isaka yote aliyokuwa ameyafanya.

67 Basi, Isaka akamutwaa Rebeka ndani ya hema iliyokuwa ya mama yake Sara, naye akakuwa muke wake. Isaka akamupenda Rebeka na kupata kufarijika nyuma ya kifo cha mama yake.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan