Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mwanzo 20 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Abrahamu na Abimeleki

1 Abrahamu alisafiri toka kule na kuelekea eneo la Negebu, akafanya makao yake kati ya Kadesi na Suri, kisha akakwenda kukaa kwa muda kule Gerari.

2 Akiwa kule, Abrahamu alisema kwamba muke wake Sara ni dada yake. Kwa hiyo, mufalme Abimeleki wa Gerari akamutwaa Sara.

3 Lakini Mungu akamufikia Abimeleki katika ndoto usiku, akamwambia: “Wewe utakufa kwa sababu ya mwanamuke uliyemutwaa, maana yuko na mume wake.”

4 Abimeleki ambaye bado hakukuwa amelala na Sara, akajibu: “Bwana, utawaua watu wasiokuwa na kosa?

5 Si ni Abrahamu mwenyewe ndiye aliyesema kwamba huyu ni dada yake? Tena hata Sara mwenyewe alisema kwamba Abrahamu ni kaka yake! Mimi nimefanya nilivyofanya kwa moyo safi na sina kosa.”

6 Basi, Mungu akamwambia katika hiyo ndoto: “Sawa. Ninajua kwamba umefanya hivyo kwa moyo safi. Mimi ndiye niliyekuzuia kutenda zambi mbele yangu. Ndiyo maana sikukuruhusu umuguse huyo mwanamuke.

7 Sasa umurudishe yule mwanamuke kwa mume wake. Abrahamu ni nabii. Atakuombea nawe utaishi. Lakini usipomurudisha, ujue kwa hakika kwamba wewe utakufa pamoja na watu wako wote.”

8 Basi, Abimeleki akaamuka asubui mapema, akawaita watumishi wake wote na kuwaelezea mambo aliyoona katika ndoto. Nao wakaogopa sana.

9 Kwa hiyo Abimeleki akamwita Abrahamu, akamwuliza: “Umetutendea nini? Nimekukosea nini hata ukaniletea zambi kubwa, mimi na ufalme wangu? Umenitendea mambo yasiyostahili kutendwa.”

10 Tena Abimeleki akazidi kumwuliza: “Ni kitu gani kimekusukuma kufanya hivyo?”

11 Abrahamu akamujibu: “Nilifanya hivyo kwa sababu hakuna anayemwogopa Mungu pahali hapa na kwamba mungeniua kusudi mumutwae muke wangu.

12 Zaidi ya hayo, kwa kweli, yeye ni dada yangu: baba yake na baba yangu ni mumoja, lakini mama tofauti; ndiyo maana aliweza kuwa muke wangu.

13 Wakati Mungu aliponifanya niache nyumba ya baba yangu na kwenda kutangatanga, nilimwambia muke wangu: ‘Popote tutakapokwenda, tafazali useme kwamba mimi ni kaka yako!’ ”

14 Abimeleki akamurudishia Abrahamu muke wake Sara, akamupa kondoo, ngombe na watumwa na wajakazi.

15 Tena Abimeleki akamwambia Abrahamu: “Angalia, inchi hii yote ni yangu! Basi, chagua popote unapopenda, ukae.”

16 Kisha, akamwambia Sara: “Mimi nimemupa ndugu yako vikoroti elfu moja vya feza kwa kuwaonyesha wote wanaokuwa pamoja nawe kwamba hauna kosa. Umehakikishwa kwamba hauna kosa.”

17 Kisha Abrahamu akamwomba Mungu, naye akamuponyesha Abimeleki, muke wake na wajakazi wake, hata wakaweza kupata tena watoto.

18 Hapo mbele Yawe alikuwa amewazuia wanawake wote wa nyumba ya Abimeleki kupata watoto kwa sababu ya Sara, muke wa Abrahamu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan