Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Mwanzo 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Uovu wa watu wa Sodoma

1 Wale wamalaika wawili wakafika katika muji wa Sodoma magaribi. Loti alikuwa ameketi kwenye mulango wa muji wa Sodoma. Alipowaona, akasimama kwenda kuwapokea, akainama kwa heshima.

2 Akasema: “Bwana zangu, karibu katika nyumba yangu mimi mutumishi wenu. Munaweza kunawa miguu na kulala kwangu usiku wa leo. Asubui mapema mutaweza kuendelea na safari yenu.” Lakini, wao wakasema: “Hapana! Sisi tutalala huku katika barabara.”

3 Loti akawasihi sana, kwa mwisho wakakubali, wakageuka na kuingia katika nyumba yake. Loti akatayarisha karamu, akachoma mikate isiyotiwa chachu, wakakula.

4 Lakini mbele ya kulala usiku, wanaume wote wa muji wa Sodoma, vijana na wazee, bila kubaki hata mumoja, wakazunguka nyumba ya Loti.

5 Wakamwita Loti na kumwuliza: “Wako wapi wale wanaume waliokuja kwako? Uwatoshe inje. Tunataka kulala nao.”

6 Loti akatoka inje, akafunga mulango nyuma yake,

7 akawaambia: “Wandugu zangu, ninawasihi musitende uovu ule.

8 Angalia, nina wabinti wawili ambao bado hawajalala na mwanaume. Muniruhusu niwape hao wabinti muwatendee kama vile munavyopenda. Lakini musiwatendee lolote wanaume hawa kwa sababu ni wageni wangu.”

9 Lakini wao wakasema: “Utupitishe! Wewe ulikuja huku ukiwa mugeni na sasa unajifanya kuwa mwamuzi! Basi, tutakutendea mabaya zaidi ya wale wageni wako.” Halafu wakamusukuma Loti nyuma hata karibu wavunje mulango wake.

10 Lakini wale wageni wakanyoosha mikono yao, wakamukokotea Loti ndani ya nyumba na kufunga mulango.

11 Kisha wakawapiga kwa kuwapofusha macho wanaume wote waliokuwa kwa mulango, wakubwa na wadogo, hata wakataabika kwa kutafuta ule mulango, nao hawakuupata.


Loti anatoka Sodoma

12 Wale watu wawili wakamwambia Loti: “Uko na mutu mwingine hapa, pengine wana wako, wabinti, wachumba wa wabinti zako au watu wengine wa jamaa yako wanaoishi katika muji huu? Uwatoshe pahali hapa haraka,

13 kwa maana kilio kilichomufikia Yawe juu ya wakaaji wa hapa ni kikubwa sana, naye ametutuma tukuje kuwaangamiza.”

14 Basi, Loti akawaendea wachumba wa wabinti zake, akawaambia: “Haraka! Mutoke pahali hapa, maana Yawe atauangamiza muji huu.” Lakini wao wakamwona kama mutu mwenye kuchekesha tu.

15 Kulipokucha, wamalaika wakamusihi Loti wakisema: “Amuka, utwae muke wako na hawa wabinti zako wawili musipate kuangamia wakati muji huu unapoazibiwa.”

16 Loti akakuwa anasitasita. Lakini kwa vile Yawe alivyomuhurumia Loti, wale wamalaika wakamushika yeye, muke wake na wabinti zake wawili, wakamutosha inje ya muji.

17 Walipowatosha inje ya muji, malaika mumoja wao akawaambia: “Mukimbie kwa ajili ya usalama wenu. Musiangalie nyuma wala kusimama popote katika bonde. Mukimbilie kwenye milima, musipate kuangamia.”

18 Loti akamwambia: “Hapana vile, ee bwana wangu!

19 Ni kweli kwamba mimi mutumishi wako nimepata kukubaliwa mbele yako, nawe umenitendea mema sana kwa kuokoa maisha yangu. Lakini kwenye milima ni mbali sana. Maangamizi haya yatanikuta mbele sijafika kule, nami nitakufa.

20 Tafazali, kule kuna muji mudogo ambao ninaweza kukimbilia maana uko karibu. Basi, uniruhusu nikimbilie kule. Ule ni muji mudogo tu, na kule nitaponyoka.”

21 Naye akamujibu: “Sawa, nimekubali ombi lako. Sitaangamiza muji uliotaja.

22 Harakisha! Kimbilia kule, nami sitafanya lolote mpaka utakapofika kule.” Hivyo muji ule ukaitwa Soari.


Kuangamizwa kwa Sodoma na Gomora

23 Jua lilikuwa limekwisha kupanda juu wakati Loti alipofika katika muji wa Soari.

24 Halafu Yawe akateremusha moto mukali wa kiberiti kutoka mbinguni juu ya Sodoma na Gomora,

25 akaiangamiza miji hiyo, bonde lote, wakaaji wake wote na mimea yote katika inchi hiyo.

26 Lakini muke wa Loti aliyekuwa nyuma ya Loti, akatazama nyuma, akageuka nguzo ya chumvi.

27 Asubui mapema, Abrahamu alikwenda pahali alipokuwa akisimama mbele ya Yawe.

28 Akiwa pale, akatazama chini pande za Sodoma na Gomora na eneo lote la bonde, akashangaa kuona moshi ukipanda, moshi kama wa furu kubwa.

29 Mungu alipoangamiza miji katika bonde ambamo Loti alikuwa anakaa, alimukumbuka Abrahamu kwa kumutosha Loti katika miji hiyo, kusudi Loti asiangamizwe pamoja nayo.


Mwanzo wa Wamoabu na Waamoni

30 Loti aliogopa kuishi katika muji wa Soari, kwa hiyo akahama toka muji ule, yeye pamoja na wabinti zake wawili, wakakwenda kuishi ndani ya pango kwenye milima.

31 Wakiwa kule, binti mukubwa akamwambia dada yake: “Baba yetu ni muzee na hakuna mwanaume katika inchi wa kutuoa tupate watoto.

32 Basi, tumuleweshe baba kwa divai, kusudi tupate kulala naye na kudumisha uzao kwa kupata watoto kwa njia yake.”

33 Usiku ule wakamulewesha baba yao kwa divai. Yule binti wa kwanza akakwenda akalala naye. Lakini baba yake hakujua wakati binti yake alipolala naye, wala wakati alipoondoka.

34 Kesho yake, yule binti wa kwanza akamwambia yule mudogo: “Jana usiku mimi nililala na baba. Leo vilevile tumuleweshe kwa divai, kisha wewe utalala naye, na hivyo sisi wote tutadumisha uzao kwa kupata watoto.”

35 Basi, usiku ule vilevile wakamulewesha baba yao kwa divai, kisha yule binti mudogo akakwenda akalala naye. Lakini baba yake hakujua wakati binti yake alipolala naye, wala wakati alipoondoka.

36 Hivyo, wabinti wote wawili za Loti wakapata mimba kutokana na baba yao.

37 Yule binti wa kwanza akazaa mutoto mwanaume, akamwita Moabu. Huyo ndiye baba wa Wamoabu mpaka leo.

38 Yule mudogo vilevile akazaa mutoto mwanaume, akamwita Beni-Ami. Huyo ndiye baba wa Waamoni mpaka leo.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan